Nyumbani

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th United Nations Environment Assembly – UNEA-7) unaofanyika jijini Nairobi, Kenya kuanzia 08 hadi 12 Disemba 2025 

Baadhi ya masuala yanayojadiliwa katika Mkutano huu ni pamoja na Mazingira Asilia na Mabadiliko ya Tabianchi; Uchumi Mzunguko, Chemikali, Taka na Uchafuzi wa Mazingira; Utawala na Sheria; na Bajeti.

Mkutano huu unaoongozwa na Ofisi ya Makamu wa Rais – Idara ya Mazingira, awali ulitanguliwa na mkutano wa maandalizi wa Kamati ya wawakilishi uliofanyika jijini hapo tarehe 01 hadi 05 Disemba 2025 ambapo wakuu wa nchi wanachama watatoa hotuba katika mkutano huo.

Zaidi ya NEMC, washiriki wengine ni Pamoja na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) na Wakala wa Misitu (TFS) ambapo Kilele cha mkutano huu ni tarehe 11 na 12 Disemba 2025.

𝐍𝐄𝐌𝐂 𝐘𝐀𝐇𝐀𝐌𝐀𝐒𝐈𝐒𝐇𝐀 𝐔𝐒𝐀𝐅𝐈 𝐖𝐀 𝐌𝐀𝐙𝐈𝐍𝐆𝐈𝐑𝐀 𝐒𝐇𝐈𝐌𝐌𝐔𝐓𝐀 𝟐𝟎𝟐𝟓 - 𝐌𝐎𝐑𝐎𝐆𝐎𝐑𝐎

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kupitia wanamichezo wake wanaoshiriki mashindano ya SHIMMUTA 2025 mkoani Morogoro wakichagizwa na kauli mbiu yao isemayo "𝑴𝒊𝒄𝒉𝒆𝒛𝒐 𝒏𝒊 𝑨𝒇𝒚𝒂, 𝑴𝒂𝒛𝒊𝒏𝒈𝒊𝒓𝒂 𝒏𝒊 𝑼𝒉𝒂𝒊" wameshiriki zoezi la kufanya usafi kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro siku ya kufunga mashindano hayo Disemba 6, 2025.

Wanamichezo hao wamefanya usafi huo ikiwa ni sehemu ya uhamasishaji wa usafi wa Mazingira kwa watumishi wanaoshiriki mashindano hayo pamoja na Wananchi wa Mkoa wa Morogoro.

Imekuwa ni utaratibu wa kawaida kwa wanamichezo hao kuhamasisha usafi wa Mazingira kila mwaka kwenye mashindano ya SHIMMUTA huku wakienzi maono ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi kuhakikisha Mazingira yanakuwa safi na yanaendelea kulindwa nchi nzima.

NEMC imeshiriki mashindano hayo ya SHIMMUTA 2025 ikiwa ni sehemu ya kuimarisha afya ya watumishi lakini pia kutumia fursa hiyo katika kutoa elimu kwa watumishi na Wananchi mkoani Morogoro kuhusiana na masuala ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

Katika kuhakikisha elimu inafika kwa watu wa rika zote pia wanamichezo hao wametoa elimu ya Mazingira na kukabidhi vifaa vya kuzolea na kuhifadhia taka katika Shule ya Msingi Mwere ambapo wanamichezo hao walikuwa wanatumia viwanja vya shule hiyo kwa ajili ya mazoezi kipindi chote wakiwa kwenye mashindano hayo.

Mashindano ya SHIMMUTA 2025 yenye Kauli Mbiu isemayo "𝑼𝒐𝒏𝒈𝒐𝒛𝒊 𝑰𝒎𝒂𝒓𝒂 𝒌𝒘𝒂 𝑴𝒊𝒄𝒉𝒆𝒛𝒐 𝑬𝒏𝒅𝒆𝒍𝒆𝒗𝒖: 𝑴𝒊𝒄𝒉𝒆𝒛𝒐 𝒏𝒊 𝑫𝒂𝒓𝒂𝒋𝒂 𝒍𝒂 𝑨𝒇𝒚𝒂, 𝑨𝒎𝒂𝒏𝒊, 𝑼𝒎𝒐𝒋𝒂, 𝒏𝒂 𝑴𝒔𝒉𝒊𝒌𝒂𝒎𝒂𝒏𝒐 𝒘𝒂 𝑲𝒊𝒕𝒂𝒊𝒇𝒂" yalianza rasmi Novemba 23, 2025 na kufungwa rasmi Disemba 6, 2025 kwenye Uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima.







NEMC YAKUTANA NA MAKAMU WA RAIS MHE. BALOZI DKT. EMMANUEL JOHN NCHIMBI DODOMA

Ni katika kikao kazi cha kupitishana kwenye majukumu ya Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekutana na  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi kwenye kikaokazi cha kwanza na watendaji wake tangu kuteuliwa kwake chenye lengo la kupitishana kwenye majukumu ya utekelezaji wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi yake.

Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza na watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na watumishi waliochini ya Ofisi hiyo wakiwemo NEMC katika kikaokazi cha kwanza tangu kuteuliwa kwake

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma kilihusisha Menejimenti na  watumishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Menejimenti ya Baraza pamoja na watendaji kutoka kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa masuala ya Carbon.

Akizungumza katika kikao hicho Balozi Dkt Emmanuel Nchimbi amesema ni kikao cha kukumbushana wajibu tulionao kwa watanzania wa kudumisha Muungano pamoja na kusimamia masuala mazima ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini hasa ikizingatiwa dira ya maendeleo ya 2050 kipengele cha tatu kimezingatia masuala ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira pamoja na Ustahimilivu wa masuala mazima ya mabadiliko ya Tabianchi.

 " Dhamana tuliyopewa ni kubwa, masuala ya Muungano, kutunza mazingira na uchumi wa buluu si vitu vya mchezo, ni lazima tumsaidie Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya siku miamoja (100) kutekeleza maagizo yahusuyo Muungano na Mazingira, tunao wajibu wa kuhakikisha Mazingira yanasimamiwa na kuhifadhiwa" Amesema Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi.

Ametoa maagizo yafuatayo: kila mtumishi aisome ilani ya chama kilichopo madarakani pamoja na dira ya maendeleo ya 2050 kwani ndio msingi wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali, masuala ya Muungano na Mazingira, Uchumi wa buluu, Carbon trade na nishati safi yasimamiwe na kutekelezwa kwa weledi,  malengo yote ya utekelezaji wa shughuli za Muungano na Mazingira yawe na namna sahihi ya ufuatiliaji na utekelezaji wake ili kufikia azma iliyokubaliwa.

Maagizo mengine ni kuandaa  mkakati wa mawasiliano utakaotoa muongozo wa namna ya kutangaza shughuli za mazingira, kuzingatia haki na stahiki za watumishi, kuhakikisha vijana wanaelewa maana halisi ya Muungano na kuuenzi pamoja na wakuu wa Taasisi kusimamia Sheria na  miongozo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Awali akimkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema NEMC inahitaji kupewa meno kwani kero za Mazingira zimekuwa nyingi hasa uchafuzi wa vyanzo vya maji na kelele chafuzi za Mazingira.

"Hakuna kitu kinanikera kama pale ocean road kila nikipita napakuta pachafu, panatoa harufu, matakataka yamezagaa, nikiwauliza NEMC.wanasema hawana meno" Mhe. Mhandisi Hamad Masauni.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Cyprian Luhemeja alipozungumza aliahidi kuyasimama na kuyatekeleza maagizo na maelekezo yote yaliyotolewa  kwa kushirikiana na watendaji wa Taasisi zote zilizo chini ya ofisi ya Makamu wa Rais.

Kikao kazi hicho kimehudhuriwa pia na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange, Naibu Katibu Mkuu Mazingira Profesa Peter Msoffe na Naibu Katibu Mkuu Muungano Bw. Abdallah H. Mitawi.




𝐍𝐄𝐌𝐂 𝐘𝐀𝐄𝐍𝐙𝐈 𝐌𝐀𝐀𝐃𝐇𝐈𝐌𝐈𝐒𝐇𝐎 𝐘𝐀 𝐒𝐈𝐊𝐔 𝐘𝐀 𝐖𝐀𝐋𝐄𝐌𝐀𝐕𝐔 𝐃𝐔𝐍𝐈𝐀𝐍𝐈

𝐘𝐚𝐬𝐡𝐢𝐤𝐚  𝐦𝐤𝐨𝐧𝐨 𝐊𝐢𝐭𝐮𝐨 𝐜𝐡𝐚 𝐄𝐫𝐢𝐜 𝐌𝐞𝐦𝐨𝐫𝐢𝐚𝐥 𝐌𝐨𝐫𝐨𝐠𝐨𝐫𝐨

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kupitia timu yake ya wanamichezo wanaoshiriki mashindano ya SHIMMUTA 2025 wametembelea Kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu cha Erick Memorial mkoani Morogoro Disemba 4, 2025.

Timu hiyo ya NEMC ilipata fursa ya kutembelea, kufariji na kuwapa misaada ya vyakula na vifaa vya usafi pamoja na kutoa elimu ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira ikiwa ni sehemu ya kuienzi siku maalumu ya walemavu ambapo duniani kote hufanyika tarehe 3 Disemba ya kila mwaka.

Akizungumza kwenye kituo hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Afisa Utumishi Mkuu wa NEMC Bi. Shukrani Haule amesema Baraza linaendelea kushirikiana na watu wa makundi yote katika kuhakikisha Mazingira yanakuwa safi na  salama kwa watu wote, lakini pia kihakikisha makundi haya yanawezeshwa na kujumuishwa katika maamuzi yanayozingatia Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

"Baraza katika kutekeleza majukumu yake linashirikiana na watu wote na kundi hili la watu wenye ulemavu limekuwa likilizingatiwa siku zote katika mipango yake yote" Amesema Bi. Shukrani.

Naye Mtendaji wa Taasisi hiyo ya Eric Memorial, Bw. Robert Mkalawa ametoa wito kwa Taasisi za Serikali kuona umuhimu wa siku hii kama ambayo NEMC imefanya.

"Tunashukuru kutembelewa Taasisi inayohusika na Mazingira ambao ni NEMC na hii inadhihirisha kuwa hakuna Mazingira bila watu na watu wenyewe ndio sisi bila kubagua, lakini nitoe rai kwa Taasisi nyingine za Serikali kuiga mfano wa NEMC katika kuadhikisha siku hii ya Walemavu Duniani". Amesema Bw. Robert.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Michezo NEMC Bw. Fortinatus Patrick amesema kilichofanyika ni muendelezo wa kile alichokisisitiza Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi katika kuweka Mazingira wezeshi kwa makundi yote kujumuisha jamii za watu wenye ulemavu katika kuhifadhi Mazingira nchini.



NEMC NA TAASISI YA CSE WAENDESHA MAFUNZO YA NAMNA YA KUTENGENEZA ORODHA YA TAKA ZA VIWANDANI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira- NEMC, kwa kushirikiana na Taasisi ya Centre of Science and Environment ( CSE) ya India imefanya mafunzo juu ya mbinu za kutengeneza Orodha ya Taka za Viwandani. 

Lengo ni kutengeneza orodha ya viwanda vyote nchini pamoja na taka zinazozalishwa na viwanda hivyo ili kuboresha usimamizi wa taka. 

Aidha, jambo hili linaenda kuchangia kwenye sera ya Taka ni Uchumi ( Circular economy) kwa kubaini aina ya taka na viwanda vinavyoweza kuchakata au kutumia taka hizo.

NEMC YASAINI MAKUBALIANO YA AWALI NA UPS KUANZISHA MFUMO WA KIDIGITALI WA UFUATILIAJI WA UCHAFUZI WA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesaini makubaliano ya awali na Kampuni ya United Platform Solution (UPS) kwa ajili ya kuanzisha mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji wa uchafuzi wa mazingira katika miradi yote ya maendeleo nchini.

Hafla hiyo ya kusaini makubaliano hayo imefanyika Disemba 04,2025 katika ukumbi wa mikutano wa Baraza uliopo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Bw. Dickson Mjinja ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Fedha, amesema Baraza limefikia hatua hiyo ili kurahisisha masuala mazima ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira kwani mfumo huo ukikamilika utarahisisha kubaini viashiria vya uchafuzi wa mazingira na kupata taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu hali ya mazingira.

Naye Bw Mamadou Drame kutoka UPS alipozungumza amesema imekuwa azma yao kushirikiana na NEMC katika kuhakikisha uchafuzi wa Mazingira unadhibitiwa kidigitali ili kuyalinda kwa maendeleo endelevu.

Akifafanua namna mfumo huo utakavyotenda kazi, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria wa NEMC, Bw. Jamal Baruti amesema  kwa sasa utaanza mradi wa majaribio ambapo vifaa maalum vitawekwa katika miradi ya mazingira ikijumuisha miradi iliyopo katika Kanda 13 za NEMC nchi nzima hali itakayoimarisha zaidi usimamizi na Uhifadhi wa mazingira nchini.





NEMC YAUNGANA NA WATANZANIA WOTE KUADHIMISHA SIKU YA WALEMAVU DUNIANI

Yasisitiza mazingira jumuishi kwa ustawi wa walemavu 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) leo limeungana na jumuiya ya kimataifa kuadhimisha Siku ya Walemavu Duniani kwa kutoa wito wa kuimarishwa kwa mazingira jumuishi na rafiki kwa watu wote, hususani watu wenye ulemavu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema kuwa jitihada za kulinda mazingira haziwezi kuwa endelevu pasipo kuhakikisha ushiriki wa watu wenye ulemavu katika mipango na maamuzi yahusuyo mazingira.

“Haki ya kuishi katika mazingira safi, salama na yenye afya ni ya kila mtu. Tunajivunia kuwa sehemu ya juhudi za kuhakikisha miundombinu na huduma za kimazingira zinakuwa salama na zinazofikika kwa watu wenye ulemavu,” alisema Dkt. Semesi.

 Ujenzi wa Miundombinu Rafiki 

Baraza limeendelea kuhimiza Taasisi za umma na binafsi kutekeleza ujenzi shirikishi (inclusive design) ili kuhakikisha njia za kupita, majengo, vyoo na vifaa vya kimazingira vinapatikana na kutumika na watu wote bila vikwazo.

 Ushirikishwaji Katika Maamuzi 

Kwa kutambua umuhimu wa uwakilishi, NEMC imeweka mikakati inayolenga kuwahusisha watu wenye ulemavu katika kamati na majadiliano muhimu ya usimamizi wa mazingira katika ngazi mbalimbali za Taifa.

 Ulinzi Dhidi ya Hatari za Kimazingira 

Baraza pia linaimarisha mifumo ya tahadhari dhidi ya majanga kama mafuriko, uchafuzi na taka hatarishi, likibainisha kuwa watu wenye ulemavu mara nyingi hukumbwa kwa kiwango kikubwa zaidi na madhara ya majanga hayo. Mwongozo unaotolewa kwa mamlaka za mitaa unalenga kuhakikisha mipango ya dharura inawalinda na kuwatambua kikamilifu.

Elimu na Uhamasishaji

Kupitia ushirikiano na wadau mbalimbali, Baraza linaendeleza kampeni za elimu na uhamasishaji kuhusu umuhimu wa mazingira safi na salama kwa ajili ya ustawi wa watu wenye ulemavu, sambamba na kukuza mtazamo chanya katika jamii.

Dkt. Semesi alihitimisha kwa kusisitiza dhamira ya NEMC katika kuhakikisha sera na miradi ya mazingira nchini inatekelezwa kwa kuzingatia usawa na ujumuishaji.

“Hakuna mtu anayepaswa kuachwa nyuma katika kunufaika na rasilimali za mazingira. Ustawi wa watu wenye ulemavu ni sehemu ya ustawi wa Taifa,” alisema.

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...