Nyumbani

NEMC YAFUTURISHA SERENA

Mwanasheria Mkuu wa Serikali -Mgeni rasmi 

Aahidi Ushirikiano wa Kisheria katika Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira Nchini

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeungana na wadau wa mazingira katika hafla ya futari iliyoandaliwa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuendeleza mahusiano mazuri baina ya taasisi hiyo na wadau wake.

Hafla hiyo imefanyika Leo 26, 2026 katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi, watumishi wa Serikali na wadau binafsi walihudhuria tukio hilo lenye taswira ya umoja na mshikamano.

Akiongea katika hafla hiyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza S. Johari  aliipongeza NEMC kwa kuandaa tukio hilo lenye kujenga umoja na kukuza mshikamano miongoni mwa Taasisi za Serikali na wadau wa mazingira. Aidha, aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa kisheria ili kuhakikisha Sheria na Kanuni za mazingira zinatekelezwa ipasavyo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, alipozungumza alisema futari hiyo ni sehemu ya utamaduni wa Baraza katika kujenga uhusiano wa karibu na wadau wake.

Alisisitiza umuhimu wa kudumisha maadili ya utu, heshima na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya hifadhi ya mazingira nchini, akibainisha kuwa kupitia ushirikiano huo malengo ya kulinda na kuboresha mazingira yanaweza kufikiwa kwa ufanisi zaidi.

Katika hatua nyingine Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Ndg. Abdul Rajabu Mhinte, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya NEMC na Ofisi ya Mkoa katika kusimamia na kutekeleza Sheria za mazingira. Aliahidi kuwa Ofisi ya Mkoa itaendelea kuunga mkono juhudi za uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira kwa ustawi wa taifa.

Hafla hiyo imehudhuriwa pia na wadau wa mazingira wakiwemo JMAT, Bodi ya NEMC, watumishi wa Baraza, wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Taasisi za kibenki









NEMC YASHIRIKI ZIARA YA NAIBU WAZIRI DKT. FESTO DUGANGE MABWEPANDE NA PUGU KINYAMWEZI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limeshiriki ziara ya Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange ya kukagua Kiwanda cha kuzalisha mbolea ya mboji cha Mabwepande Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni na Dampo la kukusanyia taka la Pugu Kinyamwezi Wilaya ya Ilala Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya ukaguzi huo Mhe. Waziri Dkt. Festo Dugange amehimiza wananchi kuyatumia madampo kukusanyia taka ili zitumike kama malighafi pamoja na kusafisha mazingira.


Aidha, ameilelekeza NEMC kuendelea kusimamia Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ili kuhakikisha Mazingira yanalindwa na kuhifadhiwa huku akitilia mkazo eneo la Usimamizi  wa taka za plastiki na kuzuia kelele chafuzi kutoka viwandani  na sehemu  za starehe. 

Amesema taka za plastiki katika madampo zimekuwa nyingi hali inayonesha pamoja na kupigwa marufuku uzalishaji, usambazaji na uuzaji wa mifuko hiyo bado inaonekana


Aidha kutokana na kuwa asilimia 60 ya taka ni zinazozalishwa na kutupwa katika madampo ni zile zinazooza, aliwahimiza wananchi kutumia fursa hiyo kuzikusanya kwa ajili ya kutengeneza mbolea ya asili.

Pia Mhe Waziri amesisitiza  uanzishaji  wa viwanda  wa kuchakata taka  zisizooza kwa utengenezaji wa mbolea na Gesi.


Ziara hiyo imehudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Saadi Mtambule na kwa upande wa NEMC imehudhuriwa na Kanda ya Mashariki Kusini upande wa ukaguzi wa Kiwanda cha kuchakata mbolea ya mboji cha Mabwepande na Kanda ya Ilala kwa upande ukaguzi wa Dampo la Pugu Kinyamwezi jijini Dar es Salaam.




BARAZA LA WAFANYAKAZI NEMC LAKUTANA

Lajadili Rasimu ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027

Baraza la wafanyakazi la NEMC limefanya Kikao maalum cha kujadili rasimu ya Bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 kwa mujibu wa taratibu za uandaaji wa bajeti, likilenga kuimarisha uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji katika utekelezaji wake. 

Kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi kimefanyika Februari 20, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa NEMC, Jijini Dar es Salaam, kikihusisha wajumbe ili kuchangia mawazo na mapendekezo yao.

Katika majadiliano, wajumbe walijikita katika masuala ya ustawi na maslahi huku mkazo mkubwa ukiwekwa kwenye kuongeza juhudi na maarifa kazini ili kuongeza mapato ya Baraza na pia kuendelea kutoa elimu ya Uhifadhi wa Mazingira kwa jamii, kwa lengo la kuimarisha utunzaji wa mazingira na kuchochea maendeleo endelevu ya Taifa.



















NEMC YAKABIDHIWA RASMI MAABARA INAYOTEMBEA KUIMARISHA KAGUZI ZA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekabidhiwa rasmi Maabara inayotembea na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) mahususi kwa ajili ya Kaguzi za Mazingira hususan kupima sampuli za kimazingira zikijumuisha za Ubora wa maji, Kelele, udongo, kemikali, madini tembo, hewa na sampuli nyinginezo za kimazingira.

Maabara hiyo ni manufaa ya Mradi wa kujenga uwezo kwa Taasisi za Serikali na binafsi (EMA Project) unaotekelezwa na NEMC kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la watu wa Sweden (SIDA).

Akizungumza wakati wa mapokezi ya Maabara hiyo yaliyofanyika katika Ofisi za NEMC Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi amesema Maabara hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda uliokuwa ukitumika kusafirisha sampuli kwenda maabara nyingine zilizoidhinishwa, ambapo gharama ya kipimo kimoja ilikuwa inaweza kufikia kati ya Shilingi za kitanzania milioni 5 hadi 10 kulingana na aina ya sampuli.

Ameongeza kuwa "kwa sasa NEMC itaweza kufanya uchunguzi ndani ya muda mfupi na kuchukua hatua stahiki mara moja, hali itakayoongeza ufanisi katika kulinda mazingira".

Akikabidhi Maabara hiyo kwa niaba ya Shirika la SIDA, Meneja Miradi ya Nishati na Mazingira, Stephen Mwalufamba kutoka Ubalozi wa Sweden nchini Tanzania ameeleza kuwa lengo kubwa la Miradi huo ni kuchangia juhudi za Serikali katika maswala ya Maendeleo na kuchangia Mazingira endelevu Kwa ajili ya ustawi wa wananchi huku akiipongeza NEMC kwa jitihada wanazofanya katika kutekeleza jukumu la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa EMA (NEMC) Bw. Paul Kalokola amesema "Maabara hiyo inavifaa vya kisasa vinavyoweza kutoa matokeo ya kisayansi kwa usahihi. Pia Maabara hiyo ina Kamera ya juu (Drone) inayoweza kusafiri umbali mrefu na kuchukua sampuli kwa ajili ya uchunguzi".

Mradi wa huo ulianza mnamo Juni 2020 na unatarajiwa kuisha mwezi Juni 2026 ambapo ulilenga kujenga uwezo kwa Taasisi za Serikali na binafsi kutekeleza Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 sura namba 191 ipasavyo.







NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA MASHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA MAZINGIRA-ZANZIBAR

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki Kikao cha kwanza cha kujenga Mashirikiano baina ya Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kilichofanyika Februari 17, 2026, Zanzibar.

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange (katikati mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Baadhi ya watendaji kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Tanzania Bara mara baada ya Kikao cha mashirikiano kati ya pande hizo mbili. Wa pili kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Immaculate Sware Semesi na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) Bw. Sheha Mjaja Juma 

Kikao hicho kilichohudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi, kimelenga kujenga dhamira ya kuimarisha uratibu na ushirikiano wa kimkakati katika masuala ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa lengo la kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa Sheria na Mipango ya Mazingira kwa maendeleo endelevu ya Taifa unazingatiwa.

Aidha, Kikao hicho ambacho ni mwendelezo wa Kikao kilichoanza Februari 16, 2026 kwa ngazi ya wataalamu na Februari 17 kwa ngazi ya Viongozi, kutoka Tanzania Bara kimehudhuriwa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange (Mb), Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Kemilembe Mutasa pamoja na baadhi ya watendaji kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.



NEMC YAFUTURISHA SERENA

Mwanasheria Mkuu wa Serikali -Mgeni rasmi  Aahidi Ushirikiano wa Kisheria katika Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira Nchini Baraza la Taifa l...