Nyumbani

NEMC YAKABIDHIWA RASMI MAABARA INAYOTEMBEA KUIMARISHA KAGUZI ZA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekabidhiwa rasmi Maabara inayotembea na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) mahususi kwa ajili ya Kaguzi za Mazingira hususan kupima sampuli za kimazingira zikijumuisha za Ubora wa maji, Kelele, udongo, kemikali, madini tembo, hewa na sampuli nyinginezo za kimazingira.

Maabara hiyo ni manufaa ya Mradi wa kujenga uwezo kwa Taasisi za Serikali na binafsi (EMA Project) unaotekelezwa na NEMC kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la watu wa Sweden (SIDA).

Akizungumza wakati wa mapokezi ya Maabara hiyo yaliyofanyika katika Ofisi za NEMC Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi amesema Maabara hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda uliokuwa ukitumika kusafirisha sampuli kwenda maabara nyingine zilizoidhinishwa, ambapo gharama ya kipimo kimoja ilikuwa inaweza kufikia kati ya Shilingi za kitanzania milioni 5 hadi 10 kulingana na aina ya sampuli.

Ameongeza kuwa "kwa sasa NEMC itaweza kufanya uchunguzi ndani ya muda mfupi na kuchukua hatua stahiki mara moja, hali itakayoongeza ufanisi katika kulinda mazingira".

Akikabidhi Maabara hiyo kwa niaba ya Shirika la SIDA, Meneja Miradi ya Nishati na Mazingira, Stephen Mwalufamba kutoka Ubalozi wa Sweden nchini Tanzania ameeleza kuwa lengo kubwa la Miradi huo ni kuchangia juhudi za Serikali katika maswala ya Maendeleo na kuchangia Mazingira endelevu Kwa ajili ya ustawi wa wananchi huku akiipongeza NEMC kwa jitihada wanazofanya katika kutekeleza jukumu la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa EMA (NEMC) Bw. Paul Kalokola amesema "Maabara hiyo inavifaa vya kisasa vinavyoweza kutoa matokeo ya kisayansi kwa usahihi. Pia Maabara hiyo ina Kamera ya juu (Drone) inayoweza kusafiri umbali mrefu na kuchukua sampuli kwa ajili ya uchunguzi".

Mradi wa huo ulianza mnamo Juni 2020 na unatarajiwa kuisha mwezi Juni 2026 ambapo ulilenga kujenga uwezo kwa Taasisi za Serikali na binafsi kutekeleza Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 sura namba 191 ipasavyo.







NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA MASHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA MAZINGIRA-ZANZIBAR

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki Kikao cha kwanza cha kujenga Mashirikiano baina ya Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kilichofanyika Februari 17, 2026, Zanzibar.

Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange (katikati mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Baadhi ya watendaji kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Tanzania Bara mara baada ya Kikao cha mashirikiano kati ya pande hizo mbili. Wa pili kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Immaculate Sware Semesi na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) Bw. Sheha Mjaja Juma 

Kikao hicho kilichohudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi, kimelenga kujenga dhamira ya kuimarisha uratibu na ushirikiano wa kimkakati katika masuala ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa lengo la kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa Sheria na Mipango ya Mazingira kwa maendeleo endelevu ya Taifa unazingatiwa.

Aidha, Kikao hicho ambacho ni mwendelezo wa Kikao kilichoanza Februari 16, 2026 kwa ngazi ya wataalamu na Februari 17 kwa ngazi ya Viongozi, kutoka Tanzania Bara kimehudhuriwa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange (Mb), Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Kemilembe Mutasa pamoja na baadhi ya watendaji kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.



NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA UHIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA BAINA YA TANZANIA NA ZANZIBAR

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limeshiriki mkutano wa siku mbili ulioandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais wenye lengo la kuleta ushirikiano kuhusu masuala ya uhifadhi na usimamizi wa Mazingira baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.


Mkutano huo umeanza Februari 16 , 2026 kwa ngazi ya wataalamu na 17 Februari, 2026 kwa ngazi ya viongozi Kisiwani Zanzibar.

Itakumbukwa kuwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimeweka utaratibu wa wizara, Idara na Taasisi zisizo za Muungano za SJMT na SMZ zinazoshabihiana kimajukumu kufanya vikao vya kuimarisha ushirikiano ili kubadilishana uzoefu, kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji na kujadili na kushughulikia changamoto mbalimbali za kiutendaji zilizopo baina ya pande hizo mbili







NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI WILAYA YA KINONDONI KATIKA VIWANJA VYA NYAKASANGWE

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikamilifu katika mkutano wa kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi wa Wilaya ya Kinondoni, uliofanyika katika viwanja vya Nyakasangwe.

Mkutano huo umeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa Albert Chalamila, pamoja na Mkuu wa wilaya  na viongozi wa Tasisi za Umma na wananchi wa Manispaa ya kinondoni






NEMC YASHIRIKI SEMINA KUHUSU MIPANGO NA MIKAKATI YA SERIKALI JUU YA HIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki semina kuhusu Mipango na Mikakati ya Serikali juu ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanyika jijini Dodoma Februari 13, 2026.

Kwa upande wa NEMC, Semina hiyo imehudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi ikiwa ni hatua mojawapo ya kuimarisha utekelezaji wa Mipango na Mikakati ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.






RUNGU LA NEMC LASHUKIA KIWANDA CHA JUYE NA YK TOSH KWA KUKIUKA SHERIA ZA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) leo Februari 12, 2026 limevifungia viwanda vya Juye Concrete Company Limited na YK Tosh Company Limited vilivyopo Mikocheni jijini Dar es Saalam vinavyojihusisha na uzalishaji wa zege, kufuatia ukiukwaji wa masharti ya kisheria ya mazingira.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya timu ya wataalamu wa mazingira kutoka NEMC kufanya ukaguzi katika viwanda hivyo na kubaini mapungufu mbalimbali ya kimazingira.

Akizungumza mara baada ya ukaguzi huo, Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria (NEMC), Bw. Hamadi Taimuru, amesema kuwa changamoto zilizobainika ni pamoja na kuanzisha shughuli za uzalishaji bila kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM), kukosekana kwa miundombinu ya kudhibiti vumbi, pamoja na ukosefu wa mfumo wa kutibu maji taka yanayozalishwa kiwandani, hali iliyosababisha maji hayo kutiririka katika maeneo ya makazi ya wananchi bila kutibiwa.

Bw. Taimuru alieleza kuwa NEMC ilishawahi kufanya ukaguzi katika viwanda hivyo zaidi ya mara nne na kutoa maelekezo ya maandishi na mdomo ili kufanya marekebisho ya miundombinu  hiyo. Hata hivyo, maelekezo hayo hayakutekelezwa  jambo linalosababisha malalamiko kutoka kwa majirani kuendelea na hivyo kusababisha Baraza kuchukua hatua ya kuvifungia viwanda hivyo ili vipate muda wa kuweza kutekeleza kikamilifu masharti yote yaliyotolewa kwa mujibu wa sheria.

Naye Meneja wa Kanda ya Mashariki Kaskazini (NEMC), Bi. Glory Kombe, amewataka wawekezaji wote kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira kabla ya kuanza kwa miradi yao ili kupata ushauri wa kitaalamu mapema, kuzingatia sheria na kuepusha madhara kwa mazingira na afya ya jamii.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Juye Concrete Company Limited, Bw. Cao Zhojun, ameihakikishia NEMC kuwa kampuni yake itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa ili kuhakikisha shughuli za uzalishaji zinaendeshwa kwa kuzingatia matakwa ya kisheria na viwango vya kimazingira.

NEMC itaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira kwa lengo la kulinda mazingira na afya ya wananchi, huku ikihakikisha kuwa shughuli za maendeleo na uwekezaji zinafanyika kwa kuzingatia misingi ya uendelevu na uwajibikaji wa kimazingira.



MWENYEKITI WA BODI YA NEMC AZINDUA MWALO WA MFANO KWA WACHIMBAJI WADOGO WA DHAHABU – GEITA

 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Mhandisi Mwanasha Tumbo, amezindua mwalo wa mfano wa uchenjuaji wa dhahabu kwa wachimbaji wadogo wa Mgusu mkoani Geita ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha mazingira ya uchimbaji na uchakataji madini pamoja na kudhibiti matumizi ya kemikali ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu.

Uzinduzi huo umefanyika wakati wa ziara ya kikazi ya Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya Baraza mkoani Geita, kujiridhisha na masuala ya Mazingira kwa elimu ya matumizi ya teknolojia salama na rafiki kwa mazingira katika shughuli za uchimbaji mdogo wa dhahabu.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Mhandisi Mwanasha Tumbo alisisitiza umuhimu wa wachimbaji kuzingatia mbinu bora na salama katika shughuli zao ili kulinda afya zao, jamii inayowazunguka pamoja na mazingira kwa ujumla. Alieleza kuwa mwalo huo wa mfano utakuwa chachu ya mabadiliko kwa wachenjuaji na wachimbaji wengine kuiga mifumo bora ya uchakataji madini.

Katika ziara hiyo, Bodi pia ilitembelea eneo linalojengwa jengo la ofisi litakalotumika kama Kituo cha Uhamasishaji (Awareness Centre) chini ya Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP). Kituo hicho kinatarajiwa kutoa elimu kwa wachimbaji na jamii kuhusu athari za zebaki na umuhimu wa kutumia teknolojia mbadala zisizo na madhara kwa afya na mazingira.

Aidha, wajumbe wa Bodi walipata fursa ya kuonana na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Reuben Shigella, ambaye alieleza kufurahishwa na ujio huo na kupongeza ushirikiano mzuri uliopo kati ya Baraza na uongozi wa mkoa. Alisisitiza kuendelezwa kwa mahusiano hayo kwa lengo la kuleta maendeleo endelevu na kulinda rasilimali za Taifa.

Kama sehemu ya kuunga mkono jitihada za uhifadhi wa mazingira, Bodi ya NEMC, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita na Menejimenti walishiriki zoezi la upandaji miti katika eneo la jengo la kituo hicho, wakionesha dhamira ya dhati ya kuimarisha utunzaji wa mazingira.

Ziara hiyo pia ilihusisha kutembelea mgodi wa Geita Gold Mining (GGM), ambapo wajumbe walijionea hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kulinda mazingira na kuendesha shughuli za uchimbaji kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa.

Kwa ujumla, ziara hiyo imeimarisha ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi, kuimarisha ushirikiano na wadau pamoja na kuhamasisha matumizi ya teknolojia salama katika sekta ya uchimbaji mdogo wa dhahabu.











NEMC YAKABIDHIWA RASMI MAABARA INAYOTEMBEA KUIMARISHA KAGUZI ZA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekabidhiwa rasmi Maabara inayotembea na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA)...