Nyumbani

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA UHIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA BAINA YA TANZANIA NA ZANZIBAR

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limeshiriki mkutano wa siku mbili ulioandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais wenye lengo la kuleta ushirikiano kuhusu masuala ya uhifadhi na usimamizi wa Mazingira baina ya Tanzania Bara na Zanzibar.


Mkutano huo umeanza Februari 16 , 2026 kwa ngazi ya wataalamu na 17 Februari, 2026 kwa ngazi ya viongozi Kisiwani Zanzibar.

Itakumbukwa kuwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimeweka utaratibu wa wizara, Idara na Taasisi zisizo za Muungano za SJMT na SMZ zinazoshabihiana kimajukumu kufanya vikao vya kuimarisha ushirikiano ili kubadilishana uzoefu, kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji na kujadili na kushughulikia changamoto mbalimbali za kiutendaji zilizopo baina ya pande hizo mbili







NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI WILAYA YA KINONDONI KATIKA VIWANJA VYA NYAKASANGWE

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikamilifu katika mkutano wa kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi wa Wilaya ya Kinondoni, uliofanyika katika viwanja vya Nyakasangwe.

Mkutano huo umeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wakiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa Albert Chalamila, pamoja na Mkuu wa wilaya  na viongozi wa Tasisi za Umma na wananchi wa Manispaa ya kinondoni






NEMC YASHIRIKI SEMINA KUHUSU MIPANGO NA MIKAKATI YA SERIKALI JUU YA HIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki semina kuhusu Mipango na Mikakati ya Serikali juu ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanyika jijini Dodoma Februari 13, 2026.

Kwa upande wa NEMC, Semina hiyo imehudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi ikiwa ni hatua mojawapo ya kuimarisha utekelezaji wa Mipango na Mikakati ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.






RUNGU LA NEMC LASHUKIA KIWANDA CHA JUYE NA YK TOSH KWA KUKIUKA SHERIA ZA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) leo Februari 12, 2026 limevifungia viwanda vya Juye Concrete Company Limited na YK Tosh Company Limited vilivyopo Mikocheni jijini Dar es Saalam vinavyojihusisha na uzalishaji wa zege, kufuatia ukiukwaji wa masharti ya kisheria ya mazingira.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya timu ya wataalamu wa mazingira kutoka NEMC kufanya ukaguzi katika viwanda hivyo na kubaini mapungufu mbalimbali ya kimazingira.

Akizungumza mara baada ya ukaguzi huo, Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria (NEMC), Bw. Hamadi Taimuru, amesema kuwa changamoto zilizobainika ni pamoja na kuanzisha shughuli za uzalishaji bila kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM), kukosekana kwa miundombinu ya kudhibiti vumbi, pamoja na ukosefu wa mfumo wa kutibu maji taka yanayozalishwa kiwandani, hali iliyosababisha maji hayo kutiririka katika maeneo ya makazi ya wananchi bila kutibiwa.

Bw. Taimuru alieleza kuwa NEMC ilishawahi kufanya ukaguzi katika viwanda hivyo zaidi ya mara nne na kutoa maelekezo ya maandishi na mdomo ili kufanya marekebisho ya miundombinu  hiyo. Hata hivyo, maelekezo hayo hayakutekelezwa  jambo linalosababisha malalamiko kutoka kwa majirani kuendelea na hivyo kusababisha Baraza kuchukua hatua ya kuvifungia viwanda hivyo ili vipate muda wa kuweza kutekeleza kikamilifu masharti yote yaliyotolewa kwa mujibu wa sheria.

Naye Meneja wa Kanda ya Mashariki Kaskazini (NEMC), Bi. Glory Kombe, amewataka wawekezaji wote kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira kabla ya kuanza kwa miradi yao ili kupata ushauri wa kitaalamu mapema, kuzingatia sheria na kuepusha madhara kwa mazingira na afya ya jamii.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Juye Concrete Company Limited, Bw. Cao Zhojun, ameihakikishia NEMC kuwa kampuni yake itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa ili kuhakikisha shughuli za uzalishaji zinaendeshwa kwa kuzingatia matakwa ya kisheria na viwango vya kimazingira.

NEMC itaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira kwa lengo la kulinda mazingira na afya ya wananchi, huku ikihakikisha kuwa shughuli za maendeleo na uwekezaji zinafanyika kwa kuzingatia misingi ya uendelevu na uwajibikaji wa kimazingira.



MWENYEKITI WA BODI YA NEMC AZINDUA MWALO WA MFANO KWA WACHIMBAJI WADOGO WA DHAHABU – GEITA

 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Mhandisi Mwanasha Tumbo, amezindua mwalo wa mfano wa uchenjuaji wa dhahabu kwa wachimbaji wadogo wa Mgusu mkoani Geita ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha mazingira ya uchimbaji na uchakataji madini pamoja na kudhibiti matumizi ya kemikali ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu.

Uzinduzi huo umefanyika wakati wa ziara ya kikazi ya Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya Baraza mkoani Geita, kujiridhisha na masuala ya Mazingira kwa elimu ya matumizi ya teknolojia salama na rafiki kwa mazingira katika shughuli za uchimbaji mdogo wa dhahabu.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Mhandisi Mwanasha Tumbo alisisitiza umuhimu wa wachimbaji kuzingatia mbinu bora na salama katika shughuli zao ili kulinda afya zao, jamii inayowazunguka pamoja na mazingira kwa ujumla. Alieleza kuwa mwalo huo wa mfano utakuwa chachu ya mabadiliko kwa wachenjuaji na wachimbaji wengine kuiga mifumo bora ya uchakataji madini.

Katika ziara hiyo, Bodi pia ilitembelea eneo linalojengwa jengo la ofisi litakalotumika kama Kituo cha Uhamasishaji (Awareness Centre) chini ya Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP). Kituo hicho kinatarajiwa kutoa elimu kwa wachimbaji na jamii kuhusu athari za zebaki na umuhimu wa kutumia teknolojia mbadala zisizo na madhara kwa afya na mazingira.

Aidha, wajumbe wa Bodi walipata fursa ya kuonana na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Reuben Shigella, ambaye alieleza kufurahishwa na ujio huo na kupongeza ushirikiano mzuri uliopo kati ya Baraza na uongozi wa mkoa. Alisisitiza kuendelezwa kwa mahusiano hayo kwa lengo la kuleta maendeleo endelevu na kulinda rasilimali za Taifa.

Kama sehemu ya kuunga mkono jitihada za uhifadhi wa mazingira, Bodi ya NEMC, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita na Menejimenti walishiriki zoezi la upandaji miti katika eneo la jengo la kituo hicho, wakionesha dhamira ya dhati ya kuimarisha utunzaji wa mazingira.

Ziara hiyo pia ilihusisha kutembelea mgodi wa Geita Gold Mining (GGM), ambapo wajumbe walijionea hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika kulinda mazingira na kuendesha shughuli za uchimbaji kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa.

Kwa ujumla, ziara hiyo imeimarisha ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi, kuimarisha ushirikiano na wadau pamoja na kuhamasisha matumizi ya teknolojia salama katika sekta ya uchimbaji mdogo wa dhahabu.











SIKU 100 ZA SAMIA NA MAZINGIRA: Mageuzi, Uwajibikaji na Mustakabali wa Kijani kwa Tanzania




MazingiraYetuUhaiWetu Tuyatunze, Yatutunze

Katika kipindi cha siku 100 tangu kuingia madarakani kwa Samia Suluhu Hassan, Tanzania imeshuhudia kasi mpya ya mageuzi katika sekta ya mazingira. Chini ya uongozi wake, dhamira ya kulinda rasilimali za asili imewekwa katika mstari wa mbele wa ajenda ya maendeleo ya Taifa.

Kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Serikali imeonesha kwa vitendo kuwa maendeleo ya kweli hayawezi kutenganishwa na uhifadhi wa mazingira. Kauli mbiu #MazingiraYetuUhaiWetu si maneno tu ni mwito wa kitaifa wa kuchukua hatua sasa kwa ajili ya kizazi cha leo na kesho.

NEMC: Safari ya Kuwa Mamlaka Kamili ya Mazingira kuelekea Dira ya 2050

Katika safari ya kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, NEMC inaendelea kuimarishwa ili kuwa mamlaka kamili ya usimamizi wa mazingira nchini. Hatua hii ni ya kimkakati ikiipa taasisi nguvu zaidi za kisheria, kiutendaji na kiusimamizi.

Kadri miradi ya kimkakati, viwanda, uchimbaji madini na ujenzi wa miundombinu inavyoongezeka, ndivyo changamoto za kimazingira zinavyoongezeka pia. Kuifanya NEMC kuwa mamlaka kamili kutarahisisha:

· Uamuzi wa haraka na sahihi

· Utekelezaji madhubuti wa Sheria ya Mazingira

· Ufuatiliaji na ukaguzi wa miradi kwa ufanisi

· Kupunguza mwingiliano wa majukumu kati ya taasisi

Hii ni hatua ya kuwekeza katika uchumi imara unaoheshimu rasilimali za asili.

Utekelezaji Imara wa Sheria ya Mazingira

Katika siku 100, NEMC imekagua jumla ya miradi 648 nchini kote. Lengo? Kuhakikisha kila mradi unatekelezwa kwa kuzingatia misingi ya uhifadhi wa mazingira na kulinda afya za wananchi.

Mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na:

· Tani 3,775.61 za taka hatarishi kuteketezwa kwa usalama

· Tani 74.40 za taka kurejelezwa

· Lita 722,500 za mafuta machafu kuchakatwa upya

Hatua hizi zimeimarisha uwajibikaji wa wawekezaji na kuonesha kuwa ukuaji wa uchumi unaweza kwenda sambamba na utunzaji wa mazingira.

Maboresho ya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM)

Huduma za Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (TAM/EIA) zimeboreshwa kwa kupunguza muda wa uchakataji wa maombi bila kupunguza viwango vya kitaaluma.

Katika kipindi hiki:

· Miradi 381 yenye thamani ya trilioni 1.83 ilisajiliwa

· Miradi 362 iliidhinishwa baada ya kukidhi matakwa ya kisheria

Kwa kushirikiana na Institute of Resource Assessment ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, NEMC inaendelea kuboresha mifumo yake ili kuongeza uwazi, ufanisi na ubora wa huduma.

Ushirikiano wa Kitaifa na Kimataifa

Mageuzi haya yameenda sambamba na kuimarishwa kwa ushirikiano na taasisi mbalimbali, ikiwemo:

· WaterAid  Usimamizi wa miradi ya maji kwa kuzingatia mazingira

· UPS – Mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji wa uchafuzi

· Chuo Kikuu cha Mzumbe  Tafiti za mazingira

· Centre for Science and Environment (CSE)  Udhibiti wa taka mijini na Ziwa Victoria

· Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)   Tafiti za mabadiliko ya tabianchi

Ushirikiano huu unaimarisha uwezo wa kitaifa kwa kutumia teknolojia, tafiti na utaalamu wa hali ya juu.

Elimu na Uhamasishaji: Jamii Kwanza

Katika kukuza ushiriki wa wananchi, NEMC imeendesha kampeni kabambe za uhamasishaji:

· Infographics 105

· Machapisho 161 ya kidigitali

· Vipindi 14 vya redio

· Vipindi 6 vya televisheni

· Habari 88 magazetini

Kupitia mitandao ya kijamii na majukwaa ya kidigitali, maelfu ya Watanzania wamefikiwa na kuelimishwa kuhusu haki na wajibu wao katika kulinda mazingira.

Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi

Katika ajenda ya mabadiliko ya tabianchi, NEMC inatekeleza miradi katika maeneo mbalimbali ikiwemo Dodoma, Singida, Tabora, Mara na Zanzibar, kwa lengo la:

· Kuimarisha ustahimilivu wa jamii

· Kulinda mifumo ikolojia

· Kupunguza athari za kemikali hatarishi

Mradi wa kudhibiti matumizi ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu katika mikoa saba ni mfano wa juhudi za kulinda afya za wananchi na mazingira.

Utawala Bora na Uwajibikaji

Kwa kuendana na maelekezo ya Rais kuhusu nidhamu na uwajibikaji, NEMC ime:

· Kuboresha mifumo ya ndani ya usimamizi

· Kuimarisha Kamati ya Maadili

· Kutoa mafunzo ya maadili kwa watumishi

Hatua hizi zimeongeza uwazi, ufanisi na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi.

Mazingira ni Uhai, ni Uchumi, ni Mustakabali

Siku 100 za Rais Samia katika sekta ya mazingira zimeweka msingi imara wa mageuzi yanayolenga maendeleo endelevu. Kuimarishwa kwa NEMC, utekelezaji wa sheria, ushirikiano mpana na uhamasishaji wa umma ni dalili kuwa Tanzania inaelekea katika uchumi wa kijani na maendeleo jumuishi.

Ni wajibu wetu sote kutambua kuwa:

Mazingira si chaguo  ni msingi wa maisha yetu.

#MazingiraYetuUhaiWetu
Tuyatunze, Yatutunze.

 


 

BODI YA WAKURUGENZI NEMC YAFANYA MAPITIO YA MPANGO MKAKATI WA UTEKELEZAJI WA MIAKA MITANO

Bodi ya Wakurugenzi wa NEMC pamoja na Menejimenti wamefanya kikao katika Ukumbi wa Hoteli ya Adden Palace jijini Mwanza kufanya mapitio ya pamoja ya mpango mkakati wa utekelezaji wa Taasisi wa miaka mitano (NEMC Strategic Plan 2026-2030) kwa lengo la kutoa mwelekeo, vipaumbele na uhalisia wa utekelezaji wake katika kuleta matokeo chanya kwa Taifa. 

Kikao hicho kilichowakutanisha wataalamu kiliendeshwa na Mwenyekiti wa Bodi Mhandisi Mwanasha Tumbo, ambapo washiriki walipata fursa ya kujadili kwa kina vipaumbele vya kimkakati vinavyolenga kuimarisha Uhifadhi na Usimamizi endelevu wa mazingira, kuboresha mifumo ya kiutawala, kupongeza ufanisi wa matumizi ya rasilimali pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wadau.

Aidha maono na dhamira ya Taasisi yaliendelea kusisitizwa kupitia mikakati inayochochea matumizi ya Sayansi, teknolojia na ushirikiano wa wadau wa maendeleo.

Kwa ujumla mapitio ya Mpango mkakati yamehakikisha kuwa mwelekeo wa Baraza unaendana kikamilifu na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na ilani ya Chama hususan katika kulinda mazingira kwa maendeleo endelevu, kukuza uchumi wa kijani na kuboresha ustawi wa jamii. 

Kupitia kikao hiki, Baraza limeonesha dhamira thabiti ya kuhakikisha Mpango mkakati unakuwa chombo hai cha kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa kwa Sasa na vizazi vijavyo.







NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KUIMARISHA USHIRIKIANO WA UHIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA BAINA YA TANZANIA NA ZANZIBAR

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limeshiriki mkutano wa siku mbili ulioandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais wenye le...