Katika hatua muhimu ya kuimarisha usimamizi wa mazingira na kukuza uchumi wa kijani nchini, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), imekutana na wadau wa usimamizi wa taka na urejelezaji jijini Dar es Salaam kujadili mustakabali wa sekta hiyo na nafasi yake katika maendeleo endelevu ya Taifa.
Kikao hicho kilichofanyika tarehe 13 Mei 2026 katika ukumbi wa NEMC – Mikocheni, kiliwakutanisha viongozi wa Serikali, wadau wa mazingira, waokota taka rejeshi, waokota chuma chakavu, sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa taka unaolinda mazingira na kuongeza thamani ya kiuchumi kupitia urejelezaji.
Akifungua kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira), Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Haran Luvanda alisema kuwa Tanzania kwa sasa huzalisha zaidi ya tani milioni 14.4 za taka ngumu kila mwaka, huku karibu nusu ya taka hizo zikizalishwa katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Dodoma, Mbeya na Tanga. Alieleza kuwa iwapo taka hizo hazitasimamiwa vizuri zinaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo uchafuzi wa mazingira, magonjwa ya mlipuko, kuziba mifereji na mafuriko.
Hata hivyo, Serikali imebainisha kuwa taka si tatizo pekee bali pia ni rasilimali yenye uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa Taifa kupitia dhana ya uchumi mzunguko (Circular Economy). Kupitia mfumo wa “Punguza, Tumia Tena na Rejeleza” maarufu kama 3Rs, Serikali inalenga kubadili mtazamo wa jamii ili kuona taka kama chanzo cha ajira, malighafi na maendeleo.
Katika hotuba yake, Balozi Luvanda aliwatambua waokota taka rejeshi na waokota chuma chakavu kama mashujaa wa kimya wanaochangia kwa kiwango kikubwa kupunguza taka zinazopelekwa dampo, kuongeza viwango vya urejelezaji na kusaidia kupunguza uzalishaji wa gesijoto. Alisisitiza kuwa kazi yao imekuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa kijani nchini.
“Waokota taka na waokota chuma chakavu ni sehemu muhimu ya mfumo wa usimamizi wa taka nchini. Kupitia kazi yao, maelfu ya vijana na wanawake wamepata ajira na kipato huku mazingira yakihifadhiwa,” alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, Dkt. Immaculate Sware Semesi, alisema kuwa maadhimisho ya miaka 40 ya NEMC yenye kauli mbiu “NEMC@40: Tunza Mazingira, Linda Taifa” yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza uwekezaji na ubunifu katika sekta ya usimamizi wa taka.
Aliyataja makundi mbalimbali kama Tanzania Waste Pickers Association (TAWAPA), Tanzania Recyclers Association(TARA) pamoja na Mtandao wa Waokota Taka Rejeshi Dar es Salaam (MTAWADA) kuwa miongoni mwa wadau muhimu wanaosaidia kusukuma mbele agenda ya uchumi mzunguko nchini.
Dkt. Semesi alibainisha kuwa NEMC imeendelea kushuhudia ongezeko la wawekezaji na taasisi zinazojihusisha na shughuli za ukusanyaji, usafirishaji, uchakataji na urejelezaji wa taka, hali inayodhihirisha kuongezeka kwa mwamko wa uzingatiaji wa sheria za mazingira pamoja na kukua kwa sekta ya uchumi mzunguko nchini.
Aidha, alieleza kuwa matumizi ya teknolojia za kisasa katika usimamizi wa taka, ikiwemo mifumo ya kidijitali ya ufuatiliaji wa taka, mashine za uchakataji pamoja na teknolojia za kuzalisha nishati kutokana na taka, yanafungua ukurasa mpya wa uwekezaji na ubunifu nchini Tanzania.
#NEMC40 #Miaka40YaNEMC #NEMCat40 #SustainableTanzania #MazingiraYetuUhaiWetu #MsemajiMkuuWaSerikali #2026Trends #SamiaSuluhuHassan#𝑴𝒂𝒛𝒊𝒏𝒈𝒊𝒓𝒂𝒀𝒆𝒕𝒖𝑼𝒉𝒂𝒊𝑾𝒆𝒕𝒖
#TUNZAMAZINGIRALINDATAIFA