NEMC Kanda ya Morogoro/Rufiji imeshirika zoezi la kupanda miti 5,000 aina ya Mkongo ( Afzelia quanzensis) katika eneo la bwawa la Mindu, Kata ya Kauzeni Manispaa ya Morogoro. Zoezi lililoandaliwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) kama sehemu ya maadhimisho ya wiki ya Maji.
NEMC TANZANIA
Mazingira yetu, Uhai Wetu
NEMC YASHIRIKI ZIARA YA KATIBU MKUU DKT. RICHARD MUYUNGI-KAGERA
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) – Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi, limeshiriki ziara ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, iliyofanyika mkoani Kagera tarehe 16.03.2026, kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu matumizi ya nishati safi na uhifadhi wa mazingira.
Katika ziara hiyo, Dkt. Muyungi alitembelea Shule ya Sekondari Rugambwa iliyopo Manispaa ya Bukoba pamoja na Shule ya Msingi Hosiana iliyopo Wilaya ya Karagwe. Lengo la ziara hizo lilikuwa kujionea namna taasisi za elimu zinavyotekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhusu kuhamia matumizi ya nishati safi ili kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa unaochangia mabadiliko ya tabianchi.
Aidha, Katibu Mkuu alitembelea mradi wa Kaderes Enterprise uliopo Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera, ambapo alipata fursa ya kujionea juhudi za wadau katika utekelezaji wa miradi ya kaboni (carbon credit) inayolenga kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi na kuchangia katika uhifadhi wa mazingira.
Katika ziara hiyo, Dkt. Muyungi alisisitiza masuala mbalimbali kama vipaumbele vya kitaifa:
- Matumizi ya Nishati Safi: Kuimarisha matumizi ya nishati mbadala kama vile majiko banifu, gesi asilia, nishati ya jua na umeme safi ili kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, kulinda misitu, na kuboresha afya ya jamii.
- Udhibiti wa Hewa Ukaa: Kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi (GHGs) kupitia teknolojia rafiki kwa mazingira, ufanisi wa matumizi ya nishati, na utekelezaji wa miradi ya upandaji miti na uhifadhi wa misitu.
- Biashara ya Kaboni: Kukuza uelewa na ushiriki wa wadau katika miradi ya Kaboni kama fursa ya kiuchumi, ambapo jamii na taasisi zinaweza kunufaika kifedha kupitia uhifadhi wa mazingira na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.
- Ushirikishwaji wa Taasisi zenye zaidi ya watu 100: Kuhamasisha taasisi za serikali na zisizokuwa za serikali zenye watu zaidi ya 100 kuwa vinara wa matumizi ya nishati safi na elimu ya mazingira kwa vitendo.
-Pamoja na Uzingatiaji wa Sera na Sheria: Kusisitiza uzingatiaji wa miongozo na Sheria za Mazingira.
NEMC NA WATER AIDS WAADHIMISHA SIKU YA MAJI
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na shirika lisilo la kiserikali la WaterAid, katika kuadhimisha mwezi wa maji mwezi Machi na Siku ya urejelezaji Duniani (Global Recycling Day, tarehe 18 Machi), kuelekea kilele cha Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri (International Day of Zero Waste), limefanya tathmini ya hali ya udhibiti wa taka ngumu kwa lengo la kulinda chanzo cha maji cha Ziwa Bassotu kilichopo Kijiji cha Bassotu, Wilaya ya Hanang, Mkoa wa Manyara.
Tathmini hiyo imelenga kubaini changamoto zilizopo na kuweka mikakati bora ya udhibiti wa taka ndani ya kijiji hicho na maeneo jirani, ili kunusuru ziwa hilo ambalo kwa sasa linakabiliwa na hatari ya kugeuzwa dampo lisilo rasmi. Hali hii inachangiwa na utupaji holela wa taka ngumu, ikiwemo chupa za viuatilifu vinavyotokana na shughuli za kilimo, jambo linalohatarisha ubora wa maji, uhai wa viumbe hai ziwani na afya ya binaadamu na mazingira kwa ujumla.
Malengo hayo yanaweza kufikiwa endapo tutaimarisha utekelezaji wa dhana ya uchumi mzunguko (circular economy) kuelekea taka sifuri kupitia urejelezaji. Hatua hii itasaidia kulinda chanzo hicho cha maji na kuboresha hali ya mazingira ya Kijiji cha Bassotu kwa ujumla.
MATUKIO KATIKA PICHA, UKAGUZI WA MGODI WA DHAHABU WA GEITA GOLD MINES (GGM) KATIKA ZIARA YA MHESHIMIWA WAZIRI, MHANDISI HAMAD YUSUF MASAUNI MKOANI GEITA
Pichani ni ziara ya Mheshimiwa Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Yusuf Masauni (wa kwanza kushoto) akikagua hali ya Mazingira katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mines Mkoani Geita ambapo aliambatana na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi na baadhi ya watumishi wa NEMC, pamoja na Viongozi wengine kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Machi 14, 2026
MATUKIO KATIKA PICHA, WAZIRI MASAUNI (OFISI YA MAKAMU WA RAIS-MUUNGANO NA MAZINGIRA APANDA MTI KATIKA KITUO CHA ELIMU YA ZEBAKI CHA NEMC-GEITA
Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni akipanda mti katika eneo litakapokuwa lango kuu la Jengo la Kituo cha kutoa elimu kuhusu Athari za matumizi ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji Madini ya Dhahabu katika afya na Mazingira linalosimamiwa na NEMC chini ya ufadhili wa Global Environmental Facility (GEF) lililojengwa mkabala na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita ikiwa ni jitaha za kuunga mkono azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kukijanisha Tanzanaia.
Mhe. Waziri amepanda mti huo wakati wa ziara yake alipotembelea Jengo hilo.
Kadhalika katika kuunga mkono jitihada hizo Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi pia alipanda mti katika eneo hilo
WAZIRI MASAUNI AIPONGEZA NEMC UJENZI WA KITUO CHA KUTOA ELIMU YA ZEBAKI - GEITA
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yusuf Masauni amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa ujenzi wa Jengo la kituo cha kutoa elimu kuhusu athari za afya na mazingira zitokanazo na matumizi yasiyo salama ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji wa madini wa dhahabu kwa wachimbaji wadogo na masuala ya Mazingira kwa ujumla mkoani Geita.
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP) Dkt. Befrina Igulu ameeleza Miundombinu rafiki kwa Mazingira iliyowekwa katika Jengo hilo ikiwa ni pamoja na Maabara na Maktaba za kisasa za elimu ya Zebaki mfumo wa nishati ya mwanga asili wa jua, mfumo wa uvunaji wa maji, Ukumbi wa Bodi na Ukumbi mkubwa wa Mikutano.
NEMC imejenga Jengo hilo ikiwa ni manufaa ya Mradi uliolenga kupunguza au kuondosha kabisa matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa Madini unafadhiliwa na Global Environment Facility (GEF) na kusimamiwa na Benki ya Dunia ambapo kwa Tanzania unatekelezwa katika Mikoa ya Geita, Mwanza, Mara, Shinyanga, Singida, Mbeya na Songwe.
NEMC KANDA YA ZIWA VICTORIA MASHARIKI YASHIRIKI ZIARA YA WAZIRI MASAUNI-MWANZA
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki ziara ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) ya Ukaguzi wa Miradi ya uwekezaji Jijini Mwanza.
Ziara hiyo ililenga kukagua Miradi ya uwekezaji na namna inavyotekeleza Uhifadhi wa Mazingira Mkoani humo.
Akimpokea Mhe. Waziri katika Ofisi yake, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amesema Ofisi yake inafanya juhudi kubwa kushirikiana na NEMC kuhakikisha Mazingira yanalindwa na kutunzwa katika Mkoa huo licha ya changamoto zinazoikabili Ofisi yake hasa katika udhibiti wa Kelele chafuzi za Maeneo ya kumbi za starehe.
Akizungumza na vyombo vya habari mara baada ya Ukaguzi huo, Mhe. Waziri amewataka wawekezaji na watanzania wote kulinda Mazingira huku akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaosababisha uharibifu wa Mazingira kwa namna yoyote.
"Tunawajibu wa kulinda Mazingira lli Mazingira yawe mazuri ni lazima sisi tuyalinde, na ili yawe mabaya ni lazima sisi tuyaharibu, Serikali inawajibu wa kuhakikisha watanzania wanaendelea kutunza Mazingira" amesema Mhe. Waziri Hamad Yusuf Masauni.
NEMC KANDA YA MOROGORO/RUFIJI NA MORUWASA WAPANDA MITI 5,000
NEMC Kanda ya Morogoro/Rufiji imeshirika zoezi la kupanda miti 5,000 aina ya Mkongo ( Afzelia quanzensis) katika eneo la bwawa la Mindu, Kat...
-
Ni katika kufanya tathmini na kuimarisha umoja. Watumishi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Makao Makuu na k...
-
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...
-
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Kanda ya Kusini tarehe 15 Novemba 2025 lilishiriki kusimamia na kushuhudia Uteke...