Nyumbani

NEMC YAONGEZA VYOMBO VYA USAFIRI KUIMARISHA MIUNDOMBINU WEZESHI YA UTEKELEZAJI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeongeza vyombo vya usafiri kwa kutumia mapato yake ya ndani, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha miundombinu wezeshi ya utekelezaji wa majukumu ya kimazingira, ikiwemo ufuatiliaji, ukaguzi na uzingatiaji wa Sheria ya mazingira nchini.

Akizungumza leo Agosti 11, 2026 wakati wa makabidhiano ya magari mawili kwa baadhi ya viongozi wa Baraza, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema Baraza limeanza na magari mawili kati ya matano kwa ajili ya viongozi na linatarajia kununua magari mengine 20 ndani ya mwaka huu kwa ajili ya kuimarisha utendaji kazi katika Kanda zote 13 nchini.


 
“Magari haya tumeyanunua sisi wenyewe kwa kutumia mapato yetu ya ndani na tunaanza na magari 5 kwa ajili ya viongozi, lakini kwa malengo tuliyojiwekea kwa mwaka huu tutanunua magari mengine 20 " amesema Dkt. Semesi.

Ameongeza “Hii ni katika kuhakikisha tunaboresha utendaji kazi katika jukumu tulilokasimiwa la usimamizi wa mazingira nchini, sawa na malengo na matakwa ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 pamoja na malengo ya Rais wetu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan,”

Naye Mkurugenzi wa Utawala na Fedha Bw. Dickson Mjinja alipozungumza aliahidi utunzwaji wa magari hayo na kutumika kwa malengo kusidiwa huku akisistiza uwajibikaji kufikia





NEMC YAWEKA MSINGI WA UTEKELEZAJI WA ESG NA URIPOTI WA UENDELEVU


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeendelea kuimarisha uwezo wake katika masuala ya Mazingira, Jamii na Utawala Bora (Environmental, Social and Governance – ESG) pamoja na uripoti wa uendelevu, kupitia mafunzo ya siku tano yaliyotolewa na KPMG kuanzia tarehe 3 hadi 7 Agosti 2026 katika Ofisi ya Kanda ya Temeke ya NEMC, Dar es Salaam.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango endelevu wa Baraza wa kuimarisha mifumo na kanuni za ESG na kuweka uripoti wa uendelevu kuwa sehemu ya utendaji wa kitaasisi. Mpango huo unahusisha maandalizi ya Sera ya ESG, Mfumo wa ESG, pamoja na Ripoti ya Uendelevu ya Baraza kwa mwaka wa fedha 2025/2026, kwa kuzingatia vipaumbele vya kitaifa na mifumo ya kimataifa inayotambulika katika uripoti wa uendelevu.


Katika mafunzo hayo, maafisa walioteuliwa kuwa Mabingwa wa ESG na Uripoti wa Uendelevu (ESG & Sustainability Reporting Champions) walipata uelewa na ujuzi wa vitendo kuhusu misingi ya ESG, mifumo ya uripoti wa uendelevu, tathmini ya masuala muhimu ya kimazingira, kijamii na kiutawala, ushirikishwaji wa wadau, usimamizi wa takwimu za ESG, pamoja na namna ya kuandaa na kuratibu uripoti wa uendelevu ndani ya taasisi.


Aidha, mafunzo hayo yameweka msingi wa kuanza kwa vikao na shughuli za vitendo vitakavyowezesha maandalizi ya Sera ya ESG, Mfumo wa ESG na Ripoti ya kwanza ya Uendelevu ya NEMC. Hatua hii inalenga kuhakikisha kuwa masuala ya ESG yanaendelea kujumuishwa katika mipango, shughuli na mifumo ya utendaji wa Baraza.


Kupitia hatua hiyo, NEMC inaendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira, ufanisi wa kitaasisi, uwajibikaji na uwazi, sambamba na kuchangia katika utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu na vipaumbele vya taifa.




MKUTANO WA 48 WA KAMATI YA URITHI WA DUNIA WA UNESCO WAHITIMISHWA RASMI BUSAN, JAMHURI YA KOREA

Tarehe 29 Julai 2026, ulihitimishwa rasmi Mkutano wa 48 wa Kamati ya Urithi wa Dunia wa UNESCO (48th Session of the World Heritage Committee) uliofanyika jijini Busan, Jamhuri ya Korea, ukihusisha wajumbe kutoka Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972 pamoja na wadau mbalimbali wa kimataifa.

Mkutano huo ulitoa fursa ya kujadili na kufanya maamuzi muhimu kuhusu uhifadhi, usimamizi na maendeleo endelevu ya maeneo ya Urithi wa Dunia. Aidha, ulijadili hali ya uhifadhi wa maeneo yaliyopo kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia, mapendekezo ya maeneo mapya ya kuorodheshwa, pamoja na changamoto zinazoathiri urithi wa asili na wa kiutamaduni duniani, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi na ongezeko la shughuli za kibinadamu.

Tanzania ilishiriki kikamilifu katika mkutano huo, ikichangia mijadala kuhusu uhifadhi wa maeneo ya Urithi wa Dunia, usimamizi wa mifumo ya ikolojia, uhifadhi wa bioanuwai na matumizi ya mbinu za kisayansi katika kuimarisha usimamizi endelevu wa mazingira. Ushiriki huo umeendelea kuonesha dhamira ya nchi katika kutekeleza Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972 na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika uhifadhi wa urithi wa asili na wa kiutamaduni.

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhakikisha maeneo ya Urithi wa Dunia nchini yanalindwa na kusimamiwa kwa kuzingatia misingi ya uhifadhi wa mazingira, matumizi endelevu ya rasilimali na utekelezaji wa mikataba ya kimataifa ya mazingira.

Kupitia ushiriki katika majukwaa ya kimataifa kama haya, Tanzania inaendelea kujifunza na kubadilishana uzoefu na mataifa mengine, huku ikiimarisha nafasi yake katika juhudi za pamoja za kulinda urithi wa dunia na mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA 48 CHA KAMATI YA URITHI WA DUNIA YA UNESCO - BUSAN KOREA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kupitia Mkurugenzi Mkuu wake, Dkt. Immaculate Semesi, linashiriki katika Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia ya UNESCO (48th Session of the World Heritage Committee) kinachofanyika jijini Busan, Jamhuri ya Korea.

Kikao hicho kinawakutanisha wajumbe kutoka Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972, pamoja na wadau mbalimbali wa kimataifa, kwa lengo la kupitia, kujadili na kufanya maamuzi kuhusu masuala ya uhifadhi, usimamizi na maendeleo endelevu ya maeneo ya Urithi wa Dunia. Vilevile, kikao kinatoa fursa ya kutathmini hali ya uhifadhi wa maeneo yaliyopo kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia, kuzingatia mapendekezo ya maeneo mapya yanayostahili kuorodheshwa, pamoja na kujadili changamoto zinazoathiri urithi wa asili na wa kiutamaduni duniani, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la shughuli za kibinadamu na uendelezaji usiozingatia misingi ya uhifadhi.

Ushiriki wa NEMC katika mkutano huu unaakisi dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuendelea kutekeleza kikamilifu Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972, kuimarisha usimamizi wa maeneo ya urithi wa dunia nchini, na kuendeleza ushirikiano wa kimataifa katika kuhifadhi urithi wa asili na wa kiutamaduni wenye thamani ya kipekee kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

Katika mkutano huo, Dkt. Semesi anawakilisha Tanzania katika mijadala mbalimbali inayohusu uhifadhi wa maeneo ya Urithi wa Dunia, usimamizi wa mifumo ya ikolojia, uhifadhi wa bioanuwai, pamoja na matumizi ya mbinu za kisayansi na mifumo bora ya usimamizi wa mazingira ili kuhakikisha maeneo hayo yanaendelea kuhifadhiwa kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

Aidha, ushiriki wa Tanzania ukiongozwa na Mheshimiwa Balozi Saidi Yakubu,Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu UNESCO na kuhudhuriwa pia na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera na Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji ( Mb),unatoa fursa ya kuimarisha ushirikiano wa kitaalamu na taasisi za kimataifa kama UNESCO na IUCN, kubadilishana uzoefu na nchi nyingine kuhusu mbinu bora za uhifadhi wa maeneo ya urithi, pamoja na kutafuta fursa za ushirikiano wa kiufundi na kifedha kwa ajili ya kuimarisha uhifadhi na usimamizi wa maeneo ya Urithi wa Dunia nchini Tanzania.

Tanzania ni miongoni mwa Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia na inajivunia kuwa na maeneo kadhaa yaliyotambuliwa na UNESCO kuwa ni Urithi wa Dunia kutokana na thamani yake ya kipekee ya kimataifa. Ushiriki wa NEMC katika kikao hiki unaimarisha nafasi ya Tanzania katika mijadala ya kimataifa kuhusu uhifadhi wa mazingira na urithi wa dunia, sambamba na kuendeleza diplomasia ya mazingira na kukuza mchango wa nchi katika utekelezaji wa ajenda za maendeleo endelevu duniani.

WAZIRI MASAUNI ASITISHA SHUGHULI ZA KIWANDA CHA AFRICAN STEEL KWA UCHAFUZI WA MAZINGIRA


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amesitisha shughuli za Kiwanda cha African Steel Group Company Limited kilichopo Kijiji cha Mwavi, Kata ya Fukayosi, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani, kinachotumia chuma chakavu kuzalisha nondo kwa ukiukwaji wa Sheria na Kanuni za uhifadhi wa mazingira.

Hatua hiyo imefikiwa wakati wa ziara ya Waziri Masauni ya kukagua utekelezaji wa Sheria za mazingira katika viwanda vitatu vilivyopo Wilaya ya Bagamoyo, ambapo amekipongeza kiwanda cha KAMAL Refinery Limited kinachojishughulisha na uchakataji wa mafuta machafu na Roster Vehicle Equipment Limited kinachojihusisha na utengenezaji na uunganishaji wa magari (truck assembly) kwa Usimamizi mzuri wa Sheria ya Mazingira 

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Waziri Masauni amesema Kiwanda cha African Steel kimeendelea kuchafua mazingira licha ya kupewa maelekezo mara kadhaa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kufuatia ukaguzi uliofanyika lakini kimepuuza na kushindwa kuyatekeleza, hali iliyoilazimu Serikali kuchukua hatua ya kusitisha shughuli zake.

Ametaja ukiukwaji uliobainika kuwa ni uchafuzi mkubwa wa hewa unaotokana na moshi mzito unaohatarisha afya za wafanyakazi na wananchi, utiririshaji wa majitaka kwenye mazingira, utupaji holela wa taka pamoja na kukosekana kwa eneo maalumu la kuhifadhi chuma chakavu, hali inayosababisha uchafuzi wa ardhi. Kutokana na hali hiyo, ameamuru shughuli za kiwanda hicho kusitishwa hadi kitakapotekeleza kikamilifu maelekezo ya NEMC na Serikali.

Aidha, Waziri Masauni ameipongeza NEMC  kwa kazi kubwa ya ukaguzi na usimamizi wa mazingira nchini, huku Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Dkt. Immaculate Sware Semesi akiahidi kuendelea kusimamia kikamilifu Sheria ya Mazingira katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuhakikisha viwanda vinazingatia matakwa ya kisheria.

NEMC NA IUCN WAKUSANYA MAONI YA WADAU KUHUSU RASIMU YA KANUNI ZA WAJIBU WA MZALISHAJI WA BIDHAA (EPR)

 


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na IUCN, limeanza mkutano wa siku mbili wa wadau kuhusu Rasimu ya Kanuni ya Wajibu wa Mzalishaji wa Bidhaa (Extended Producer Responsibility - EPR) katika Usimamizi wa Taka na Uhifadhi wa Mazingira. Mkutano huo umeanza rasmi tarehe 21 Julai 2026 mkoani Dodoma na unalenga kukusanya maoni ya wadau ili kuboresha rasimu ya kanuni hiyo kabla ya kukamilishwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Bw. Fredrick Mulinda, ambaye ni Afisa Mazingira Mkuu wa NEMC, amesema mkutano huo ni muhimu katika kujadili na kutoa maoni kuhusu Rasimu ya Kanuni za Wajibu wa Mzalishaji wa Bidhaa (EPR) katika Usimamizi wa Taka na Uhifadhi wa Mazingira. Amesema mkutano huo unaonesha dhamira ya pamoja ya Serikali na wadau mbalimbali katika kuimarisha usimamizi endelevu wa mazingira nchini kupitia mfumo utakaoweka wajibu kwa wazalishaji wa bidhaa katika usimamizi wa taka zinazotokana na bidhaa zao.

Aidha, Bw. Mulinda ameishukuru IUCN kwa ushirikiano wake wa karibu na NEMC katika kufanikisha maandalizi ya mkutano huo na kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhifadhi na kusimamia mazingira. Pia amewapongeza wataalamu wa NEMC na wadau wote walioshiriki maandalizi ya mkutano huo muhimu, akisisitiza kuwa ushirikiano wao utachangia kupatikana kwa kanuni imara zitakazoboreshwa kupitia maoni ya wadau.

KWAGILWA AFUNGIA KIWANDA CHA HANGJIN STEEL MKURANGA KWA UKIUKWAJI WA SHERIA ZA MAZINGIRA

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa, amesimamisha shughuli za Kiwanda cha Hangjin Steel kinachojihusisha na uzalishaji wa nondo kwa kutumia vyuma chakavu, kilichopo Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, baada ya kubainika kukiuka masharti ya Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira.

Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia ziara ya ukaguzi wa utekelezaji wa Sheria na Kanuni za Mazingira, ambapo ilibainika kuwa shughuli za kiwanda hicho zilikuwa zinasababisha athari kwa mazingira kutokana na kutokuzingatia masharti yaliyowekwa na mamlaka husika za usimamizi wa mazingira.

Miongoni mwa dosari zilizobainika ni kutokuwepo kwa mfumo wa udhibiti wa taka ndani ya kiwanda, kushindwa kudhibiti mafuta machafu yanayotumika kama chanzo cha nishati na hivyo kuchanganyika na maji na kutiririka kwenye makazi ya wananchi pamoja na mabonde ya maji. Aidha, kiwanda hicho kilibainika kutokuwa na mfumo madhubuti wa kudhibiti hewa chafu inayozalishwa na shughuli zake, pamoja na kukosa Cheti cha Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (TAM) kinachotakiwa kisheria.

Mhe. Kwagilwa ameuagiza uongozi wa kiwanda hicho kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na mamlaka za mazingira kabla ya kuruhusiwa kuendelea na shughuli zake. Maelekezo hayo yanajumuisha kurekebisha dosari zote zilizobainika, kuweka mifumo madhubuti ya kudhibiti uchafuzi wa mazingira na kutimiza matakwa yote ya kisheria yanayohusu usimamizi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema amepokea maelekezo yaliyotolewa na Mhe. Naibu Waziri na kuahidi kuwa Baraza hilo litayatekeleza kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ili kuhakikisha sheria inazingatiwa na mazingira yanaendelea kulindwa.

NEMC YAONGEZA VYOMBO VYA USAFIRI KUIMARISHA MIUNDOMBINU WEZESHI YA UTEKELEZAJI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeongeza vyombo vya usafiri kwa kutumia mapato yake ya ndani, ikiwa ni sehemu ...