Wanawake wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kutoka Kanda 13 nchini wameungana na wanawake wote duniani kuadhimisha Kilele cha Siku ya Wanawake Duniani, kilichoadhimishwa kitaifa katika Mkoa wa Geita, ambapo kwa Mkoa wa Dar es Salaam wanawake wameadhimisha katika Uwanja wa Barafu, Kata ya Mburahati, Wilaya ya Ubungo, ambapo mgeni rasmi katika hafla hiyo ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert John Chalamila.
Maadhimisho hayo yaliyosindikizwa na kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwaWanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira ya Maendeleo 2050,” ikisisitiza umuhimu wa usawa wa kijinsia na kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Albert John Chalamila alisisitiza kuwa maadhimisho haya ni fursa muhimu ya kuimarisha ushiriki wa wanawake katika vyombo vya maamuzi, kubadilisha mitazamo ya kijamii, na kuchangia moja kwa moja katika malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050. Aliongeza kuwa kuwepo kwa mazingira rafiki kwa wanawake ni muhimu katika kufanikisha maendeleo jumuishi ya taifa.
Maadhimisho haya yameonyesha wazi kuwa uwezeshaji wa wanawake ni chachu muhimu ya maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa, huku akisisitiza kwamba wanawake wanapaswa kuendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ili kuchangia ustawi wa Taifa.