Nyumbani

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗢𝗡𝗚𝗢𝗭𝗔 𝗠𝗔𝗝𝗔𝗗𝗜𝗟𝗜𝗔𝗡𝗢- 𝗪𝗔𝗥𝗦𝗛𝗔 𝗬𝗔 𝗞𝗜𝗞𝗔𝗡𝗗𝗔 𝗞𝗔𝗧𝗜 𝗬𝗔𝗞𝗘 𝗡𝗔 𝗖𝗦𝗘 𝗡𝗔 𝗜𝗡𝗗𝗜𝗔



 𝗡𝗶 𝗞𝗮𝘁𝗶𝗸𝗮 𝗙𝘂𝗿𝘀𝗮 𝘇𝗶𝗹𝗶𝘇𝗼𝗽𝗼 𝗸𝘄𝗲𝗻𝘆𝗲 𝗨𝘀𝗶𝗺𝗮𝗺𝗶𝘇𝗶 𝘄𝗮 𝘁𝗮𝗸𝗮 𝘇𝗮 𝗠𝗮𝘁𝗮𝗶𝗿𝗶 𝗖𝗵𝗮𝗸𝗮𝘃𝘂

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Machi 25, 2026, limeendelea kuongoza majadiliano katika siku ya pili ya warsha ya Kikanda kuchochea fursa mpya katika Usimamizi wa taka za matairi chakavu ambapo mawasilisho ya kanuni za Usimamizi wa matairi chakavu (End-of-Life Tyres – ELTs) katika nchi zinazotekeleza mfumo wa Extended Producer Responsibility (EPR) yalifanyika.

Aidha, wasilisho la kitaalamu kutoka kituo cha Afrika Kusini cha kukuza uzalishaji wa kijani kuhusu umuhimu wa usimamizi wa matairi chakavu katika kulinda mazingira, kuchochea uchumi wa kijani na kuunda ajira, huku washiriki kutoka Ghana wakishirikisha uzoefu wa matumizi mbadala ya matairi chakavu na mbinu za kuwaunganisha wakusanyaji wadogo katika mfumo rasmi.

Kadhalika, mwakilishi kutoka Much Asphalt - Afrika Kusini aliwasilisha kuhusu matumizi ya teknolojia za kisasa zinazotumia matairi chakavu katika ujenzi wa barabara kama njia ya kuongeza thamani ya taka na kuboresha uimara wa barabara.

Kupitia warsha hiyo, NEMC imeongeza uelewa wa kuhusu mbinu bora za kuthibiti taka zitokanazo na matairi chakavu na kukuza uchumi rejeleshi.

MAAFISA HABARI NA WADAU WA ELIMU KWA UMMA WASISITIZWA KUWAUNGANISHA WANANCHI



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb) amewataka Maafisa Habari, Uhusiano na Mawasiliano wa Serikali pamoja na wadau wengine wa Elimu kwa Umma kutumia nafasi zao kuwaunganisha Watanzania kwa kutoa taarifa zenye kuleta tija kwa jamii kwa kuzingatia weledi, ujuzi na ubunifu.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ametoa wito huo alipokuwa akifungua Mkutano wa 110 wa Wadau wa Elimu kwa Umma unaofanyika jijini Arusha kuanzia Machi 23 hadi 27, 2025 katika Ukumbi wa PAPU akiwa ndiye Mgeni Rasmi ambapo amewataka wadau hao wa elimu kwa Umma ambao asilimia kubwa ni Maafisa Habari, Uhusiano na Mawasiliano wa Serikali kuhakikisha wanaongeza ubunifu katika kufikisha taarifa zenye kuwaunganisha Watanzania.

"Tumieni nafasi zenu kuunganisha Watanzania na kupitia mada zinazofundishwa ni imani yangu kwamba zitaongeza weledi na ujuzi, hivyo tumieni vizuri kuongeza ubunifu katika kuwaeleza wananchi kuhusu mambo mazuri yanayotekelezwa na Serikali" Amesema Dkt. Mwigulu.

Pia Dkt. Mwigulu amesisitiza Wadau hao wa elimu kwa Umma kujenga utamaduni wa kufanya Tafiti kupata taarifa sahihi kabla ya kupeleka kwa wananchi huku akiwataka wadau hao kuhakikisha wanatoa taarifa wakiwa na uelewa juu ya taarifa hizo wanazozitoa.

"Ni lazima msome na kuelewa kile mnachokipeleka kwa wananchi, huku mkihakikisha kwamba mnalinda Taswira za Taasisi zenu" Amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ni moja kati ya Taasisi zinazoshiriki Mkutano huo kwa kuwakilishwa na Afisa Uhusiano na Mawasiliano wake, Bw. Tajiri Kihemba ikizingatiwa kwamba NEMC ni kati ya wadau Muhimu wa masuala ya utoaji wa elimu kwa Umma katika eneo la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

Mkutano huu umeandaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ikiwa na lengo la kuongeza uelewa kwa wadau wa elimu kwa Umma juu ya namna bora ya kutimiza jukumu hilo muhimu ili kufanikisha kufikisha taarifa kwa Watanzania na wadau wengine wa maendeleo nchini.

NEMC NA UDSM WAANDAA KONGAMANO LA UZINDUZI WA MTAMBO WA NISHATI SAFI YA HAIDROJENI

 Baraza la Taifa la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Asasi Binafsi ya Bora Women Go Green limeandaa Kongamano la uzinduzi wa mtambo wa Nishati safi ya kupikia aina ya haidrojeni likiwa na lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini lililofanyika leo Machi 25, 2026 katika Ukumbi wa Nkurumah Hall wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.


Akizungumza katika uzinduzi wa mtambo huo, Mgeni rasmi, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange amesema uzinduzi wa mtambo huo ni hatua muhimu katika kufikia malengo ya Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia.

Aidha Dkt. Dungage amesisitiza kuwa ili kukabiliana na changamoto na athari za mazingira na zile za mabadiliko ya tabianchi, ni lazima kuongeza jitihada za Utunzaji na Usimamizi wa mazingira, kuwekeza kwenye vyanzo vya nishati mbadala na kuwa na mifumo ya kusaidia kustahimili mabadiliko ya tabianchi.


Ameeleza kuwa Serikali inalenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2030, akitaja vyanzo kama umeme, bayogesi, haidrojeni, gesi asilia, nishati ya jua, majiko banifu na mkaa mbadala kuwa ni suluhisho la kudumu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema uzinduzi huo sio tu ishara ya maendeleo ya teknolojia, bali pia ni uwekezaji katika ubunifu na uwezo wa vijana wa Kitanzania.


Ameongeza kuwa matumizi ya mtambo huo yana uwezo wa kubadilisha maisha ya jamii kwa kupunguza gharama, kulinda afya dhidi ya moshi wa kupikia, na kuhifadhi mazingira, huku akizipongeza taasisi zote zilizohusika kufanikisha kongamano hilo.









Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la WaterAid-Tanzania, limefanya ziara ya mafunzo nchini Rwanda. Mafunzo haya yameandaliwa na kutekelezwa na WaterAid-Rwanda, na yamefanyika katika Ofisi za shirika hilo.

Lengo kuu la mafunzo haya ni kujifunza namna WaterAid-Rwanda inavyotekeleza miradi ya maji, hususan katika eneo la Bugesera, ikiwa ni pamoja na mbinu za kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na usimamizi wa huduma za usafi wa mazingira.

Ziara hii ya mafunzo imehudhuriwa na viongozi na wataalamu mbalimbali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mkurugenzi Msaidizi wa Usambazaji wa Maji na Usafi wa Mazingira, Afisa Tawala wa Mkoa wa Manyara, pamoja na maafisa wengine kutoka serikalini na WaterAid

NEMC, CSE WAANDAA WARSHA YA KIKANDA KUCHOCHEA FURSA MPYA KATIKA USIMAMIZI WA TAKA ZA MATAIRI CHAKAVU

 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Kituo cha Sayansi na Mazingira - India (CSE) wameandaa warsha ya kikanda inayolenga kujadili changamoto na fursa zitokanazo na ongezeko la taka za matairi chakavu.

 Warsha hiyo imewakutanisha washiriki kutoka mamlaka za usimamizi wa mazingira na wadau mbalimbali kutoka nchi za Kenya, Uganda, Afrika Kusini, Ghana na Nigeria. Mkutano huu umefanyika katika Hoteli ya Four Points by Sheraton na New Africa Hotel jijini Dar es Salaam tarehe 23 na 24 Machi 2026.

Katika warsha hiyo, mada mbalimbali zimejadiliwa ikiwemo miundo ya kisheria na kikanuni, teknolojia za kuongeza thamani ya taka za matairi, pamoja na matumizi ya masoko katika kukuza dhana ya uchumi rejeleshi. Lengo kuu ni kubadilishana uzoefu na kubuni mbinu mbadala zitakazosaidia kupunguza athari za kimazingira huku zikichangia maendeleo endelevu ya kiuchumi katika ukanda wa Afrika.





NEMC KUAINISHA FURSA ZILIZOPO KATIKA TAKA, MACHI 30

Ni katika Viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam, Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya kuondoa Taka 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limejipanga kutoa elimu kuhusu fursa zilizopo kwenye taka katika Maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Kuondoa Taka yanayotarajiwa kuadhimishwa Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yatatanguliwa na maonesho yatakayoanza tarehe 28 hadi siku ya kilele, Machi 30, 2026 yatakayobainisha namna ambavyo taka ni fursa kupitia ubunifu wa bidhaa zitokanazo na taka

Akizungumza na vyombo vya Habari, Meneja Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Bw. Hamadi Taimuru amesema siku hii inalenga kuhamasisha umma  kupunguza uzalishaji wa taka na kutoa elimu kwa wadau na wananchi wote kutambua fursa za uwekezaji katika taka kupitia ukusanyaji, uchakataji na Urejelezaji wa taka.

"Tunawaomba wananchi na wadau wote tufike katika viwanja vya Mnazi mmoja kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi na moja jioni kujifunza na kujionea fursa za uwekezaji katika eneo la taka". Amesema Bw. Taimuru

Aidha ameongeza kuwa Maadhimisho hayo yamelenga kuhimiza na kuhakikisha kuwa dhana ya 𝗣𝘂𝗻𝗴𝘂𝘇𝗮, 𝗧𝘂𝗺𝗶𝗮 𝘁𝗲𝗻𝗮 𝗻𝗮 𝗥𝗲𝗷𝗲𝗹𝗲𝘇𝗮 inatekelezwa kwa vitendo na kwa matakwa ya Sheria ili kuwa na Mazingira safi, afya bora ya jamii na matumizi ya rasilimali endelevu Kwa ajili ya Maendeleo ya Taifa.

Kauli mbiu ya kimataifa ya Maadhimisho haya ni "𝒌𝒖𝒘𝒆𝒛𝒆𝒔𝒉𝒂 𝒕𝒂𝒌𝒂 𝒔𝒊𝒇𝒖𝒓𝒊 𝒌𝒘𝒆𝒏𝒚𝒆 𝑺𝒆𝒌𝒕𝒂 𝒚𝒂 𝒄𝒉𝒂𝒌𝒖𝒍𝒂" ambayo inaangazia tatizo la upotevu wa chakula Duniani na Athari zake kwa Mazingira na Jamii ambapo inakadiriwa kuwa upotevu wa chakula huchangia takribani asilimia kumi (10%) ya hewa chafuzi (greenhouse gases)

Ameongeza kuwa, kitaifa inaendelea Kaulimbiu ya '𝑻𝒂𝒌𝒂 𝒏𝒊 𝑭𝒖𝒓𝒔𝒂' ambayo inaweka msisitizo kuwa taka si taka tu bali ni malighafi za kutengeneza bidhaa nyingine.

DKT. FESTO DUGANGE AITIKISA KAGERA, AITAKA NEMC KUKAZA UZI USIMAMIZI WA SHERIA ZA MAZINGIRA KWENYE MIRADI

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Dkt. Festo Dugange, amelitaka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuhakikisha linasimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira katika miradi yote ya maendeleo inayotekelezwa mkoani Kagera, ili kulinda rasilimali za mazingira na afya za wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya mazingira katika Halmashauri za Wilaya ya Karagwe na Misenyi, Dkt. Dugange alisisitiza kuwa NEMC inapaswa kuimarisha ukaguzi na ufuatiliaji wa miradi, kuhakikisha tathmini za athari kwa mazingira (EIA) zinafanyika kwa mujibu wa sheria na kwamba masharti yote ya kimazingira yanazingatiwa kabla na wakati wa utekelezaji.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri alikagua mradi wa vijana wa kuchakata taka za plastiki unaosaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira na kutoa ajira kwa vijana. Pia alitembelea mradi wa biashara ya kaboni kupitia kilimo mseto (Kinoni Agroforestry Farm) unaotekelezwa na kampuni ya KADERES, unaolenga kuwawezesha wakulima kunufaika na biashara ya hewa ukaa sambamba na kuhifadhi mazingira.

Aidha, alikagua Kiwanda cha Vifungashio (Magunia) cha KADERES, Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia unaohamasisha matumizi ya nishati mbadala ili kupunguza ukataji miti, pamoja na mradi wa ujenzi wa dampo la kuhifadhia maji taka wilayani Karagwe unaolenga kuboresha usafi wa mazingira na kulinda afya ya jamii.

Akizungumza na wananchi wa Karagwe na Misenyi, Dkt. Dugange alihamasisha jamii kuona mazingira kama fursa ya kiuchumi. Alieleza kuwa taka zinaweza kuwa rasilimali yenye thamani endapo zitasimamiwa na kuchakatwa kwa usahihi.

“Taka si taka tu bali ni rasilimali muhimu inayoweza kuleta manufaa ya kiuchumi. Taka zinazooza zinaweza kutumika kutengeneza gesi na mbolea ya asili kwa ajili ya bustani za kioganiki na kulinda rutuba ya udongo,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja NEMC Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi Bw. Boniphace Guni, amesema NEMC itaendelea kuimarisha usimamizi wa miradi yote inayotekelezwa katika kanda hiyo na kuhakikisha sheria za mazingira zinatekelezwa kikamilifu nchini kote.

Ziara hiyo pia ilihusisha ushiriki wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe na Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha maendeleo endelevu yanakwenda sambamba na uhifadhi wa mazingira.

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗢𝗡𝗚𝗢𝗭𝗔 𝗠𝗔𝗝𝗔𝗗𝗜𝗟𝗜𝗔𝗡𝗢- 𝗪𝗔𝗥𝗦𝗛𝗔 𝗬𝗔 𝗞𝗜𝗞𝗔𝗡𝗗𝗔 𝗞𝗔𝗧𝗜 𝗬𝗔𝗞𝗘 𝗡𝗔 𝗖𝗦𝗘 𝗡𝗔 𝗜𝗡𝗗𝗜𝗔

 𝗡𝗶 𝗞𝗮𝘁𝗶𝗸𝗮 𝗙𝘂𝗿𝘀𝗮 𝘇𝗶𝗹𝗶𝘇𝗼𝗽𝗼 𝗸𝘄𝗲𝗻𝘆𝗲 𝗨𝘀𝗶𝗺𝗮𝗺𝗶𝘇𝗶 𝘄𝗮 𝘁𝗮𝗸𝗮 𝘇𝗮 𝗠𝗮𝘁𝗮𝗶𝗿𝗶 𝗖𝗵𝗮𝗸𝗮𝘃𝘂 Baraza la Ta...