Ni katika Viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam, Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya kuondoa Taka
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limejipanga kutoa elimu kuhusu fursa zilizopo kwenye taka katika Maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Kuondoa Taka yanayotarajiwa kuadhimishwa Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.
Maadhimisho hayo yatatanguliwa na maonesho yatakayoanza tarehe 28 hadi siku ya kilele, Machi 30, 2026 yatakayobainisha namna ambavyo taka ni fursa kupitia ubunifu wa bidhaa zitokanazo na taka
Akizungumza na vyombo vya Habari, Meneja Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Bw. Hamadi Taimuru amesema siku hii inalenga kuhamasisha umma kupunguza uzalishaji wa taka na kutoa elimu kwa wadau na wananchi wote kutambua fursa za uwekezaji katika taka kupitia ukusanyaji, uchakataji na Urejelezaji wa taka.
"Tunawaomba wananchi na wadau wote tufike katika viwanja vya Mnazi mmoja kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi na moja jioni kujifunza na kujionea fursa za uwekezaji katika eneo la taka". Amesema Bw. Taimuru
Aidha ameongeza kuwa Maadhimisho hayo yamelenga kuhimiza na kuhakikisha kuwa dhana ya 𝗣𝘂𝗻𝗴𝘂𝘇𝗮, 𝗧𝘂𝗺𝗶𝗮 𝘁𝗲𝗻𝗮 𝗻𝗮 𝗥𝗲𝗷𝗲𝗹𝗲𝘇𝗮 inatekelezwa kwa vitendo na kwa matakwa ya Sheria ili kuwa na Mazingira safi, afya bora ya jamii na matumizi ya rasilimali endelevu Kwa ajili ya Maendeleo ya Taifa.
Kauli mbiu ya kimataifa ya Maadhimisho haya ni "𝒌𝒖𝒘𝒆𝒛𝒆𝒔𝒉𝒂 𝒕𝒂𝒌𝒂 𝒔𝒊𝒇𝒖𝒓𝒊 𝒌𝒘𝒆𝒏𝒚𝒆 𝑺𝒆𝒌𝒕𝒂 𝒚𝒂 𝒄𝒉𝒂𝒌𝒖𝒍𝒂" ambayo inaangazia tatizo la upotevu wa chakula Duniani na Athari zake kwa Mazingira na Jamii ambapo inakadiriwa kuwa upotevu wa chakula huchangia takribani asilimia kumi (10%) ya hewa chafuzi (greenhouse gases)
Ameongeza kuwa, kitaifa inaendelea Kaulimbiu ya '𝑻𝒂𝒌𝒂 𝒏𝒊 𝑭𝒖𝒓𝒔𝒂' ambayo inaweka msisitizo kuwa taka si taka tu bali ni malighafi za kutengeneza bidhaa nyingine.