Tarehe 29 Julai 2026, ulihitimishwa rasmi Mkutano wa 48 wa Kamati ya Urithi wa Dunia wa UNESCO (48th Session of the World Heritage Committee) uliofanyika jijini Busan, Jamhuri ya Korea, ukihusisha wajumbe kutoka Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972 pamoja na wadau mbalimbali wa kimataifa.
Mkutano huo ulitoa fursa ya kujadili na kufanya maamuzi muhimu kuhusu uhifadhi, usimamizi na maendeleo endelevu ya maeneo ya Urithi wa Dunia. Aidha, ulijadili hali ya uhifadhi wa maeneo yaliyopo kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia, mapendekezo ya maeneo mapya ya kuorodheshwa, pamoja na changamoto zinazoathiri urithi wa asili na wa kiutamaduni duniani, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi na ongezeko la shughuli za kibinadamu.
Tanzania ilishiriki kikamilifu katika mkutano huo, ikichangia mijadala kuhusu uhifadhi wa maeneo ya Urithi wa Dunia, usimamizi wa mifumo ya ikolojia, uhifadhi wa bioanuwai na matumizi ya mbinu za kisayansi katika kuimarisha usimamizi endelevu wa mazingira. Ushiriki huo umeendelea kuonesha dhamira ya nchi katika kutekeleza Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972 na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika uhifadhi wa urithi wa asili na wa kiutamaduni.
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuhakikisha maeneo ya Urithi wa Dunia nchini yanalindwa na kusimamiwa kwa kuzingatia misingi ya uhifadhi wa mazingira, matumizi endelevu ya rasilimali na utekelezaji wa mikataba ya kimataifa ya mazingira.
Kupitia ushiriki katika majukwaa ya kimataifa kama haya, Tanzania inaendelea kujifunza na kubadilishana uzoefu na mataifa mengine, huku ikiimarisha nafasi yake katika juhudi za pamoja za kulinda urithi wa dunia na mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)












