Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yusuf Masauni amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa ujenzi wa Jengo la kituo cha kutoa elimu kuhusu athari za afya na mazingira zitokanazo na matumizi yasiyo salama ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji wa madini wa dhahabu kwa wachimbaji wadogo na masuala ya Mazingira kwa ujumla mkoani Geita.
Mhe. Masauni ametoa pongezi hizo Machi 14, 2026 alipozuru eneo la ujenzi wa Jengo hilo ambalo limefikia asilimia 80 ya ujenzi linalojengwa mkabala na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani humo.
Akizungumza mara baada ya Ukaguzi wa Jengo hilo, Waziri Masauni ameeleza namna alivyofurahishwa na Uzingatiaji wa maswala ya kimazingira katika ujenzi wa Jengo hilo na kwamba litatumika kama Kituo cha kutoa taaluma mbalimbali kwa wananchi kuhusiana na maswala ya Mazingira
"Jengo hili litasaidia masuala mbalimbali ya Mazingira, litakuwa kituo cha kutoa taaluma mbalimbali kwa wananchi kuhusiana na maswala ya Mazingira hususan changamoto kubwa ya matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa madini ambapo imekuwa ikiathiri mazingira na afya ya wananchi.
Akizungumza mara baada ya Ukaguzi wa Jengo hilo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi amesema Jengo hilo ni mfano wa ramani itakayotumika kujenga majengo mengine kumi na mbili (12) ya Kanda za NEMC. Aidha amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Martn Shegella kwa kuipatia NEMC eneo kwa ajili ya ujenzi wa Jengo hilo.
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP) Dkt. Befrina Igulu ameeleza Miundombinu rafiki kwa Mazingira iliyowekwa katika Jengo hilo ikiwa ni pamoja na Maabara na Maktaba za kisasa za elimu ya Zebaki mfumo wa nishati ya mwanga asili wa jua, mfumo wa uvunaji wa maji, Ukumbi wa Bodi na Ukumbi mkubwa wa Mikutano.
NEMC imejenga Jengo hilo ikiwa ni manufaa ya Mradi uliolenga kupunguza au kuondosha kabisa matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa Madini unafadhiliwa na Global Environment Facility (GEF) na kusimamiwa na Benki ya Dunia ambapo kwa Tanzania unatekelezwa katika Mikoa ya Geita, Mwanza, Mara, Shinyanga, Singida, Mbeya na Songwe.