Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kupitia ofisi yake ya Kanda ya Bagamoyo, limetoa elimu ya mazingira kwa Shule ya Msingi Nia Njema, tarehe 9 Oktoba 2025.
Elimu hiyo iliyotolewa kwa walimu na wanafunzi imelenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Meneja wa Kanda ya Bagamoyo Bi. Ndimbumi Joram (wa pili kushoto) akitoa elimu ya Mazingira kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Nia njema, kulia kwake ni Mhandisi wa Mazingira (NEMC) Bw. Jerusalem Bagaza
Katika mafunzo hayo, Meneja wa Kanda ya Bagamoyo, Bi. Ndimbumi Joram, amewahimiza wanafunzi kuwa mabalozi wa mazingira bora kwa kuhakikisha usafi wa mazingira ya shule na majumbani mwao. Amesisitiza kuwa jukumu la kulinda mazingira sio la serikali pekee, bali ni wajibu wa kila mmoja, hasa watoto ambao ni viongozi wa kesho.
Aidha, Bi. Ndimbumi amezungumzia athari za utupaji hovyo wa taka ngumu na matumizi ya mifuko ya plastiki, akieleza kuwa plastiki ni moja ya changamoto kubwa inayoathiri mazingira duniani.
Amehimiza matumizi ya mifuko mbadala inayoweza kutumika mara nyingi kama njia mojawapo ya kupunguza taka za plastiki na kulinda afya ya mazingira.
Kwa kutambua juhudi za wanafunzi na walimu katika kushiriki kikamilifu mafunzo hayo, Meneja huyo ametoa zawadi za mifuko mbadala kama motisha na mfano wa vitendo vya ulinzi wa mazingira.
Shule ya Msingi Nia Njema imeahidi kuendeleza elimu hiyo kwa vitendo kwa kuanzisha klabu ya mazingira itakayosaidia kutunza mazingira ya shule na jamii kwa ujumla.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni