Nyumbani

NEMC YAINGIA MTAANI KIDIGITALI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Halmashauri za Mkoa wa Dar es salaam  linaendesha zoezi maalumu la Ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi yote ya maendeleo kwa kutumia mfumo maalumu wa kidigitali uitwao 'Mazingira App'.

Akitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti amesema zoezi hilo litadumu kwa wiki nne na litahusisha kaguzi za Mazingira kwenye miradi ya maendeleo hususani kuangalia uzingatiaji wa matakwa ya Usimamizi wa Mazingira kama vile usimamizi wa taka, matumizi sahihi ya ardhi pamoja na  uhifadhi wa vyanzo vya maji.

Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti (wa kwanza kushoto) akitoa taarifa kwa Vyombo vya Habari kuhusu zoezi maalumu la Ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi yote ya maendeleo kwa kutumia mfumo maalumu wa kidigitali uitwao 'Mazingira App'.

Ameongeza kwa kutumia mfumo wa Mazingira App pia utawawezesha kuchunguza uzingatiaji wa Sheria zinazohusu afya ya jamii, usalama wa kazi na mipango miji  ambazo kwa kutokutekelezwa kwake huchangia kwa kiasi kikubwa uchafuzi au uharibifu wa mazingira.

Aidha Bw. Jamal Baruti amesema ushirikiano na uongozi wa Jiji la Dar es salaam umelenga kuongeza uelewa na ufanisi kwa maafisa mazingira kuhusu Usimamizi hafifu wa taka ngumu, changamoto ya taka za plastiki, uharibifu wa Mazingira kutokana na uchimbaji holela wa kwenye mito na mabonde na matumizi holela ya ardhi kinyume na taratibu za mipangomiji.

Kwa upande wake Meneja Kanda ya Kaskazini Mashariki (NEMC) Bi. Glory Kombe alipozungumza amewataka Viongozi wa Halmashauri na Serikali za mitaa kutoa ushirikiano wakati wote wa zoezi hili ili kufikia tija tarajiwa kwa maendeleo endelevu ya Mazingira nchini.

Kadhalika Meneja Glory Kombe amefafanua  kuwa jukumu la Halmashauri na Mamlaka za Serikali za mitaa ni kuhakikisha Miradi ya maendeleo inazingatia taratibu za Mazingira ikiwemo ufanyikaji wa Tathmini ya Mazingira na Jamii kama ilivyobainishwa kwenye Sheria ya Mazingira na Kanuni zake na kusimamia usafi wa Mazingira kwa ujumla pamoja na kuwataka maofisa Mazingira na Kamati za Mazingira kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Sheria.

Meneja Kanda ya Kaskazini Mashariki Bi. Glory Kombe (wa kulia) akichangia mada katika Mkutano huo
Meneja Uzingatiaji wa Sheria (NEMC)Bw. Hamadi Taimuru (wa kulia) akichangia mada katika Mkutano huo

 NEMC imeanzisha mfumo huo wa Mazingira app' ambao ni wa kidigitali ili kurahisisha na kuongeza  ufanisi katika ukusanyaji na uhifadhi wa Taarifa za Miradi pamoja na usajili wa Miradi mipya ambapo zitachangia Baraza na Serikali kupanga na kusimamia Miradi ya maendeleo kwa ufanisi zaidi.



NEMC YAKAGUA MGODI WA 'URANIUM' MKOANI RUVUMA UNAOTARAJIWA KUANZA 2026

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lilifika na kukagua Mgodi wa madini aina ya Uranium uliopo katika Wilaya ya Namtumbo Mkoani Ruvuma ambao ulikuwa katika Uchimbaji mdogo wa majaribio huku Uchimbaji mkubwa ukitarajiwa kuanza mwaka 2026.

NEMC ilifika na kufanya Ukaguzi katika Mgodi huo na kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha shughuli za Uchimbaji katika Mgodi huo haziathiri Mazingira, Viumbe hai na wakazi wa jirani na Mgodi huo ikiwa ni agizo la Serikali.

Awali NEMC ilianza kwa kutoa elimu ya Mazingira na Afya kwa wakazi wa vijiji vilivyo karibu na Mgodi huo ili kuwajengea uelewa kuhusiana na madini ya 'Uranium' jinsi yanavyoweza kuhatarisha afya na Mazingira ikiwa hayata chakatwa na kudhibitiwa kwa umakini.

Akizungumza katika Ukaguzi huo Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria Bw. Jamal Baruti alisema NEMC ilifika katika Mgodi huo kufanya Ukaguzi ili kutathmini ikiwa wawekezaji katika Mgodi huo wamekidhi na kuzingatia miondombinu ya Mazingira ambayo haita haribu Mazingira, kuhatarisha usalama wa wakazi na wafanyakazi katika Mgodi huo kabla Uchimbaji mkubwa haujaanza.

Timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC na Kampuni ya Uchimbaji ya MANTRA wakikagua moja ya mlima wenye madini ya  'Urunium' wakati wa ukaguzi wa Mgodi huo. Wa pili kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti.

Aidha Bw. Baruti alieleza kuwa Mradi wa Mgodi huo utakuwa na uwezo wa kuzalisha tani elfu 27 kwa siku na utakuwa ni Mradi mkubwa wa Uchimbaji madini nchini ukilinganisha na Miradi mingine nchini Tanzania.

Aliongeza kuwa Tanzania  itakuwa nchi ya nne ya uzalishaji wa madini ya 'Uranium' Duniani huku akiwasisitiza wawekezaji na wananchi kuzingatia uhifadhi Mazingira na si tu kuangalia manufaa ya Mgodi huo.

Meneja wa Kampuni ya MANTRA Bw. Beria Vorster akitoa maelezo kwa wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC wakati wa ukaguzi wa mtambo wa kuchenjua madini ya 'Urunium' ikiwa ni sehemu ya Ukaguzi wa Mgodi huo.

Kwa upande wake Meneja Kanda ya Kusini (NEMC) Bw. Boniface Guni alisema ziara hiyo iliwasaidia NEMC kupata picha ya Mradi huo ambayo itawasaidia kusimamia Mpango wa Usimamizi wa Mazingira na jamii ipasavyo.

Naye Mwenyekiti wa Kitongoji cha Buchushu Kijiji cha Iguseka Bw. Omary Rashid aliishukuru NEMC kwa kuwapatia elimu hiyo adhimu ya Mazingira wakazi wa vijiji hivyo ambayo ni muhimu katika utunzaji wa Mazingira na Afya ya binadamu.

Timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC na Kampuni ya Uchimbaji ya MANTRA wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya ukaguzi wa Mgodi wa madini ya 'Urunium' katika eneo la Mto Mkuju Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma. Wa katikati ni Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti na kushoto kwake ni Meneja wa Mradi Bw. Beria Vorster

RUVUMA YAFIKIWA ELIMU YA MAZINGIRA- MADINI YA URANIUM

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lilitoa elimu ya kimazingira na afya kwa vijiji viwili vya Mtonya na Mandela-Likuyu katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo Mkoani Ruvuma kufuatia Mradi wa Uchimbaji wa Madini aina ya 'Uranium'  ulitarajiwa kuanza katika mgodi ulio karibu na vijiji hivyo.

Elimu hiyo ilitolewa kwa wananchi kuanzia 8-9 Septemba, 2025 kwa vijiji hivyo huku ikifuatiwa na ukaguzi uliofanyika katika mgodi huo ambapo ilikuwa hatua ya awali ya kuelimisha jamii na wawekezaji kabla ya Mradi huo kuanza ambapo  ni maagizo yaliyotolewa na Serikali ili kuhakikisha jamii inatambua uwepo wa Mradi huo na kuhakikisha  jamii haiathiriki na Mradi huo.

Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti akizungumza wakati wa utoaji wa elimu ya ya Mazingira na Afya kwa wanakijiji wa Mtonya Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma kufuatia Uchimbaji mkubwa wa madini ya 'Urunium' utakaoanza mwakani 2026

Meneja Kanda ya Kusini NEMC Bw. Boniface Guni akiwasilisha mada kwa wanakijiji wa Mandela-Likuyu Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma wakati wa utoaji wa elimu ya Mazingira na Afya kufuatia Uchimbaji mkubwa wa madini ya 'Urunium' utakaoanza mwakani 2026

Meneja Kanda ya Kusini NEMC Bw. Boniface Guni akiwasilisha mada kwa wanakijiji wa Mtonya Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma wakati wa utoaji wa elimu ya Mazingira na Afya kufuatia Uchimbaji mkubwa wa madini ya 'Urunium' utakaoanza mwakani 2026

Akizungumza katika utoaji wa elimu hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti aliutaka Uongozi wa vijiji hivyo kutumia Kamati za Mazingira na kushirikiana na Serikali kuendelea kuelimisha jamii juu ya maswala ya Mazingira na Afya ya jamii yanayoweza kusababishwa na Mradi huo.

Kwa upande wake, Meneja Kanda ya Kusini (NEMC) Bw. Boniface Guni aliwataka wakazi wa vijiji hivyo kuchangamkia fursa za ajira katika Mradi huo huku wakizingatia ulinzi wa Afya zao na Mazingira.

Aidha Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti alisema NEMC itaendelea na ufuatiliaji wa maswala ya kimazingira kwa kushirikiana na Taasisi nyingine huku akiitaka Kampuni ya Mantra TZ LTD ya Uchimbaji katika mgodi huo kutambua haki za wakazi wa vijiji hivyo na kuchangia shughuli za maendeleo ya wakazi wa vijiji hivyo kama manufaa ya Mradi huo.

Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti (wa tatu kulia waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanakijiji na Viongozi wa Kijiji cha Mtonya Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma mara baada ya kuwapatia elimu ya Mazingira na Afya kufuatia Uchimbaji mkubwa wa madini ya 'Urunium' utakaoanza mwakani 2026

NEMC YASHIRIKI MAONESHO YA KIMATAIFA YA BIASHARA NA UWEKEZAJI KUSINI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara na Uwekezaji Kusini (Kusini International Trade Fair and Festival) yanayofanyika kuanzia tarehe 14-21, Septemba, 2025 katika eneo la fukwe ya Matema Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya.

Maonesho hayo yamelenga kutangaza fursa za kibiashara zilizopo katika mikoa ya Kusini ambapo NEMC inatumia fursa hiyo kutoa elimu ya Mazingira.


Maafisa Mazingira wa NEMC Kanda ya Kusini wakitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda lao katika maonesho hayo.

DKT. SERERA AVUTIWA NA USHIRIKI WA NEMC KWENYE MAONESHO YA BIASHARA YA KIMATAIFA BARANI AFRIKA (IATE)

Naibu Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara, Dkt. Suleiman Serera amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa namna ambavyo linatoa elimu kwa wadau mbalimbali wakiwemo wawekezaji kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika kwenye Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Barani Afrika yanayotambulika kama Intra African Trade Fair (IATF) yanayoendelea jijini Algiers nchini Algeria kuanzia Septemba 4-10, 2025.

Dkt. Serera ambaye ni Mkuu wa msafara wa Ujumbe wa Tanzania unaoshiriki Maonesho hayo, ametoa pongezi hizo alipofika Banda la Tanzania akiambatana na mwenyeji wake ambaye ni Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Iman S. Njalikai.

Naibu Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara, Dkt. Suleiman Serera akizungumza na Mhandisi Mwandamizi wa Mazingira (NEMC) Bw. Peres Ntiginya wakati alipotembelea Banda la Tanzania katika maonesho hayo

"Uchumi tunaoutaja ni Uchumi wa Viwanda, lakini Viwanda tunavyohitaji ni viwanda vinavyozingatia Uhifadhi wa Mazingira, hivyo basi NEMC kwa kuja hapa wanawaambia wawekezaji waje lakini yapo ya kuzingatia kuhusu Utunzaji na Uhifadhi wa Mazingira" amesema Dkt. Serera.

"NEMC inalo jukumu la kuendelea kutoa elimu na nilichopenda zaidi ni kwamba hakuna urasimu, nimeona hapa taarifa zote unaweza kuzisoma na kuzipata kupitia "QR Code" kabla hata ya kuja kuwekeza Tanzania, Na hapa niwapongeze sana NEMC kwa namna mnavyofanya kazi vizuri na muendelee hivyo kwani Mazingira ni uhai ni lazima tuyatunze ili yatutunze" Amesisitiza Dkt. Serera.

Naye Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Imani S. Njalikai amezitaka Taasisi zinazoshiriki Maonesho hayo kuitumia fursa hii vizuri hasa katika maeneo ambayo Algeria inafanya vizuri kwenye sekta ya nishati ambayo ni pamoja na gesi, mafuta, mbolea na sekta ya madawa (pharmaceutical) ambayo ni pamoja na mafunzo kwenye maeneo hayo.

Ujumbe wa Tanzania ukiwa katika picha ya pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Viwanda na Biashara, Dkt. Suleiman Serera katika Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Barani Afrika yanayotambulika kama Intra African Trade Fair (IATF) yaliyofanyika jijini Algiers nchini Algeria kuanzia Septemba 4-10, 2025.

NEMC ikiwa ni moja ya Taasisi inayoshiriki Maonesho hayo ikiwakilishwa na Mhandisi Mkuu, Peres Ntinginya na Afisa Uhusiano na Mawasiliano, Bw. Tajiri Kihemba. Taasisi nyingine zinazoshiriki ni pamoja na TANTRADE ambao ni waratibu kwa upande wa Tanzania, TMDA, FCC, TISEZA, PURA, TFS, ZIPA.

NEMC YASHIRIKIANA NA ASASI ZA KIRAIA KUSAFISHA FUKWE YA COCO, ΝΙΚΑΤΙΚΑ KUTΕΚELEΖΑ ΚΑΜΡENI YA ΝΕΜC USAFI KAMPENI'

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC, Asasi za kiraia na wakazi wa karibu na maeneo ya fukwe ya Coco leo 6 Septemba, 2025 wamefanya usafi wa fukwe ya Coco ikiwa ni sehemu ya Utekelezaji wa Kampeni ya 'NEMC Usafi Kampeni' iliyozinduliwa rasmi 4 Septemba, 2025.

Akizungumza mara baada ya zoezi hilo, Mhandisi wa Mazingira (NEMC) Bw. Joshua Muro amesema NEMC ipo tayari kushirikiana na jamii pamoja na Asasi za kiraia katika kutekeleza Kampeni hiyo ya 'NEMC Usafi Kampeni' yenye lengo la kuhamasisha jamii kusafisha na kuhifadhi Mazingira, Pia ameitaka jamii kubadili mtazamo juu ya jukumu la usafi wa Mazingira na kufafanua kuwa ni jukumu la kila mmoja kufanya usafi wa Mazingira yanayomzunguka.

Baadhi ya watumishi wa NEMC na DEPO wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya zoezi la usafi katika Fukwe ya Coco

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Asasi ya DEPO, Ndugu. Humphrey Milinga amesema lengo kubwa la zoezi hilo ni kuhamasisha jamii katika ngazi ya familia kusafisha Mazingira na kujumuika katika vikundi vya usafishaji Mazingira zikiwemo Fukwe.

Washiriki wengine walio jumuika katika zoezi hilo ni Africraft, MBC, WWF, TIA, TESCAR na Bethlehem Parish.

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira linaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa Mazingira na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Asasi za kiraia pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha nchi yetu inakuwa na safi na salama kwa ustawi wa Afya na Mazingira.

Baadhi ya wakazi wa maeneo ya jirani na Fukwe ya Coco na baadhi ya watumishi wa NEMC kisafisha Fukwe hiyo


NEMC YAJA NA USAFI KAMPENI 2025

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limezindua kampeni mpya ya usafi iitwayo "NEMC Usafi Kampeni' 2025" yenye lengo la kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika usafi wa mazingira na kuhakikisha nchi inakuwa safi, salama na yenye afya kwa wote.

Kampeni hiyo ambayo itatekelezwa kwa ushirikiano na Ofisi ya Rais - TAMISEMI, mamlaka za mikoa na Halmashauri, Taasisi binafsi, Asasi zisizo za kiserikali na wananchi, inalenga kuibua mabadiliko ya tabia na kukuza uwajibikaji wa pamoja katika kudhibiti ongezeko la uchafuzi wa mazingira, hasa taka ngumu na plastiki.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na utekelezajinwa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu alisema kwa sasa Tanzania inazalisha takriban tani milioni 14.4 hadi 20.7 za taka kwa mwaka, huku wastani wa uzalishaji taka kwa mtu mmoja ukiwa kati ya kilo 0.66 hadi 0.95 kwa siku. Hali hii inahitaji jitihada za dhati kutoka kwa kila mtanzania.

"Kampeni hii inalenga kuondoa dhana kuwa usafi ni jukumu la serikali pekee. Kila mtu anapaswa kushiriki, kwa kuwa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 inamtaka kila mtu kuwa mdau na mlinzi wa mazingira," alisema Baruti.

Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti akizungumza na Vyombo vya habari katika Uzinduzi wa Kampeni hiyo

Aliongeza kuwa kampeni hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, ambayo imeweka hifadhi ya mazingira kuwa moja ya mihimili ya maendeleo endelevu. Kupitia kampeni hii, taka zitatazamwa kama fursa ya ajira kupitia miradi ya kijani, vijana na wanawake watawezeshwa kupitia mafunzo ya ujasiriamali wa mazingira, huku upandaji miti ukihamasishwa kwa nguvu zote.

Miongoni mwa shughuli zitakazofanyika chini ya kampeni hiyo ni pamoja na operesheni za usafi, mafunzo ya elimu ya mazingira, mashindano ya usafi kwa shule na kata, uanzishaji wa bustani za kijani, maonesho ya bidhaa rafiki kwa mazingira, pamoja na uanzishwaji wa klabu za mazingira katika shule zote za msingi na sekondari ifikapo Juni 2026.

Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na utekelezajinwa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti akizungumza na Vyombo vya habari katika Uzinduzi wa Kampeni hiyo

Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Bw. Hamad Taimuru (kushoto) akielezea jambo wakati  wa uzinduzi wa "NEMC Usafi Kampeni"..

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...