Nyumbani

NEMC YATEMBELEA KIWANDA NCHINI NORWAY KUJIFUNZA UZALISHAJI SARUJI ISIYOZALISHA HEWA UKAA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) pamoja na wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Nishati, PURA na TANESCO, wametembelea Kiwanda cha Saruji cha Brevik kilichopo nchini Norway, kinachoendeshwa na kampuni ya Norcem chini ya Heidelberg Materials, ambacho ni kiwanda cha kwanza duniani cha saruji kuendesha kituo kamili cha kunasa na kuhifadhi hewa ya ukaa (CCS). Sekta ya saruji ni ngumu kupunguza hewa ya ukaa kwa sababu malighafi yake kuu (chokaa), huzalisha kaboni dioksaidi wakati wa mchakato.

Baadhi ya Wataalamu wa Mazingira wa NEMC na Wataalamu wa Kiwanda cha Saruji cha Brevik kilichopo nchini Norway wakiwa katika picha ya pamoja 

Kiwanda hiki kinatumia teknolojia ya kunasa dioksidi kaboni kwa njia ya amini (amine absorption) ambapo gesi ya ukaa hutenganishwa kutoka kwenye moshi wa mitambo, kisha hubanwa (compressed) na kubadilishwa kuwa kimiminika ili kusafirishwa. Ukaa ulionaswa unasafirishwa kupitia mtandao wa hifadhi wa Northern Lights. Baada ya kubadilishwa kuwa kimiminika, husafirishwa kwa meli hadi kituo cha nchi kavu kisha huingizwa kwenye tabaka za miamba ya ardhini chini ya Bahari ya Kaskazini. Mradi huu ni sehemu ya mpango wa Longship wa Norway unaolenga kusaidia viwanda kupunguza hewa chafu ili kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi.

Mradi huu wenye thamani ya takriban Euro milioni 400 unategemea ushirikiano wa karibu na msaada mkubwa wa kifedha wa serikali (takriban 75%) kutokana na gharama zake kubwa za kiufundi. Pia mradi huu umewezesha kutengenezwa kwa bidhaa mpya za saruji zenye alama ya “evoZero”, zinazouzwa kama saruji yenye uzalishaji usio na hewa ya ukaa kwa sababu ukaa wake unanaswa na kuhifadhiwa. Mafunzo na uzoefu unaopatikana hapa yanatarajiwa kusaidia katika utekelezaji wa miradi mingine ya CCS Duniani kote.

Kwa ujumla, kituo cha CCS cha Brevik kinaonyesha kuwa inawezekana kupunguza kwa kiwango kikubwa uzalishaji wa hewa ya ukaa katika sekta ya saruji. Ingawa bado kuna changamoto za gharama na matumizi makubwa ya nishati, mradi huu ni hatua kubwa ya kihistoria katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na ni mfano bora kwa viwanda vingine vizito vinavyolenga kufikia uzalishaji sifuri wa hewa ya ukaa.

WAHANDISI WA NEMC WASHIRIKI MAADHIMISHO YA 22 YA SIKU YA WAHANDISI NCHINI (22ND AED 2025)

Wahandisi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) wanashiriki Maadhimisho ya 22 ya Siku ya Wahandisi nchini (AED 2025) yanayofanyika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam kuanzia tarehe 24 - 26 Septemba, 2025 chini ya kauli mbiu isemayo "Kufanikisha Dira ya 2025 na Kusonga Mbele kuelekea Dira ya 2050: Nafasi ya Wahandisi."

Tukio hili limewaleta pamoja wahandisi zaidi ya 4,000, watunga sera, na wadau mbalimbali kujadili masuala muhimu ikiwemo maadili katika uhandisi, mabadiliko ya kidijitali, miundombinu ya kijani, nishati, maji, kilimo, ushindani wa viwanda, na maendeleo endelevu.

Kupitia ushiriki huu, wahandisi wa NEMC wanaendelea kuimarisha nafasi yao katika kuunganisha ubunifu wa uhandisi na uwajibikaji katika kusimamia uhifadhi wa mazingira ili kuhakikisha kwamba safari ya Tanzania kuelekea Dira ya 2050 inabaki endelevu, jumuishi, na yenye ustahimilivu.


Wahandisi wa Mazingira (NEMC) wakiwa katika picha ya pamoja nje ya Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es salaam  wakati wa Maadhimisho ya 22 ya Siku ya Wahandisi nchini 

NEMC YASHIRIKI KONGAMANO LA UNESCO LA PROGRAMU YA BINADAMU NA HIFADHI HAI CHINA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki Kongamano la Dunia la Programu ya UNESCO ya Binadamu na Hifadhi Hai lililofanyika Jijini Hangzhou nchini China kuanzia tarehe 22-25 Septemba 2025.

Kwa upande wa NEMC Kongamano hilo limehudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa Baraza Dkt. Immaculate Sware Semesi pamoja na Meneja wa Tafiti za Mazingira (NEMC) Dkt. Rose Sallema.

Wawakilishi wengine kutoka Tanzania katika kongamano hilo ni kutoka TANAPA

Kongamano hilo limelenga Kuimarisha ushirikiano wa Kimataifa, kupata maarifa na teknolojia mpya katika kusimamia na kuhifadhi Mazingira nchini, ni fursa katika uendelevu wa Hifadhi za Taifa, fursa za Kutangaza vivutio vya kitalii, kuimarisha Ushirikiano na Jamii, kuitangaza Tanzania kimataifa, kuvutia wawekezaji na kusaidia kufikia malengo ya Maendeleo nchini.


Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi (wa pili kushoto) katika Ukumbi wa Kongamano hilo, kushoto kwake ni Meneja Tafiti za Mazingira (NEMC) Dkt. Rose Sallema pamoja na washiriki wengine wa Kongamano hilo lililofanyika Nchini China

Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi (wa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Meneja Tafiti za Mazingira(NEMC) Dkt. Rose Sallema na mshiriki mwingine wa Kongamano hilo

Meneja Tafiti za Mazingira (NEMC) Dkt. Rose Sallema (wa katikati) na baadhi ya washiriki wa Kongamano hilo.


NEMC NA TANAPA WAADHIMISHA SIKU YA FARU DUNIANI KATIKA HIFADHI YA TAIFA YA MKOMAZI- KILIMANJARO

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na TANAPA wameadhimisha Siku ya Faru Duniani ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi, Same mkoani Kilimanjaro Septemba 22,2025.

Akizungumza kwa niaba ya Meneja wa NEMC Kanda ya Kaskazini, Afisa Mazingira Mwandamizi Bw. Francis Nyamhanga amezungumzia kuhusu umuhimu wa Faru kwenye mfumo wa Ikolojia.

"Kwenye mfumo wa Ikolojia Faru husaidia kufungua njia kwa kuvunja miti kwa ajili ya Wanyama wengine wadogo kuweza kupata malisho lakini pia hula mbegu za mimea mbalimbali hivyo kupitia kinyesi chao husaidia kusambaza mbegu katika mifumo Ikolojia na kinyesi hicho pia hurutubisha mifumo ikolojia bila kusahau wanachangia kukuza pato la Taifa kwani Faru ni kivutio cha utalii" amesema Bw. Francis.

 Afisa Uhifadhi wa TANAPA, Bw. Jackson Lyimo na Afisa Mazingira Mwandamizi wa NEMC Bw. Francis Nyamhanga wakiwa katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomanzi Mkoani Kilimanjaro katika Siku ya Maadhimisho ya Siku ya Faru Duniani

Afisa Uhifadhi wa TANAPA, Bw. Jackson Lyimo ameeleza namna wanavyowafikia Jamii kwa kutoa elimu ya Uhifadhi wa Faru.

"Hifadhi Ina programu maalumu inayofahamika kama Rafiki wa Faru ambayo inafikia Jamii kwa kuipa elimu ya jinsi ya Faru hawa walivyotoweka, walivyorejeshwa na jinsi wanavyolindwa na kuzalishwa katika Hifadhi hii. Hadi sasa tumefikia shule 120 na kuwafikia walimu na wanafunzi takribani 3,600 toka Julai 2022" amesema Mhifadhi Lyimo.

Katika kuadhimisha Siku hii pia wanafunzi kutoka shule mbalimbali wamefika katika Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi kujifunza namna Uhifadhi wa Faru unavyofanyika. Maadhimisho ya Siku ya Faru Duniani hufanyika mnamo Septemba 22 kila mwaka kwa lengo la kuelimisha Umma kuhusiana na Uhifadhi wa Faru na kuwalinda dhidi ya ujangili.






NEMC YAADHIMISHA SIKU YA USAFI DUNIANI KWA KUFANYA USAFI HOSPITAL YA MWANANYAMALA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), katika kuadhimisha Siku ya Usafi Duniani tarehe 20 Septemba ya kila mwaka kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa mazingira, akiwemo DEPO, limefanya usafi Hospitali ya Mwananyamala na maeneo mengine nchi nzima ambapo Kanda 13 zipo zikitoa huduma za Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira.

Zoezi hilo limehusisha watumishi wa NEMC, wawakilishi kutoka DEPO, pamoja na baadhi ya wananchi wa maeneo ya jirani, ambapo usafi mkubwa umefanyika katika mazingira ya hospitali hiyo, ikiwa ni pamoja na kuondoa taka, kufagia, na kusafisha mitaro ya maji taka.

Watumishi wa NEMC, DEPO na baadhi ya wakazi wa Mwananyamala wakifanya Usafi kwenye Mazingira ya Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala katika Maadhimisho ya Siku ya Usafi Duniani, tarehe 20 Septemba.

Akizungumza katika zoezi hilo, Meneja wa NEMC Kanda ya Mashariki Kaskazini, Bi. Glory Kombe amesema kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kuhamasisha jamii juu ya umuhimu wa kuwa na mazingira safi, salama na endelevu kwa afya na maendeleo ya Taifa.

"Siku hii si ya kusherehekea tu, bali ni ya kutafakari na kuchukua hatua. Mazingira safi ni msingi wa afya bora, ukiangalia taka zilizookotwa hapa nyingi ni za majumbani, kunamifuko ya plastiki, chupa, mabaki ya vyakula ambazo zingetakiwa kutenganishwa kutokea nyumbani. Tuna wajibu wa pamoja kuhakikisha tunatunza mazingira yetu kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho," alisema.

Meneja wa NEMC Kanda ya Mashariki Kaskazini, Bi. Glory Kombe akizungumza na vyombo vya Habari mara baada ya zoezi hilo

Kwa upande wake, mwakilishi wa DEPO, Bw. Humphrey Milinga alieleza kuwa ushirikiano kati ya mashirika ya mazingira na Taasisi za afya ni hatua muhimu katika kuhakikisha jamii inapata huduma katika mazingira rafiki na salama.

"Tumeona ni vyema kufanya usafi hospitalini kwani ni maeneo ya kuhudumia afya, na mazingira yake yanapokuwa safi, yanasaidia kuzuia maambukizi ya magonjwa," aliongeza.

Katika maadhimisho hayo, kanda mbalimbali za NEMC pia zilitekeleza shughuli za usafi katika maeneo yao husika, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya usafi inayolenga kuhamasisha ushiriki wa jamii nzima katika kulinda mazingira.

Watumishi wa NEMC, DEPO na baadhi ya wakazi wa Mwananyamala wakifanya Usafi kwenye Mazingira ya Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala katika Maadhimisho ya Siku ya Usafi Duniani, 20 Sepemba.

Siku ya Usafi Duniani huadhimishwa duniani kote kwa lengo la kuhamasisha watu kushiriki katika shughuli za usafi wa mazingira, kuondoa taka, na kuelimisha jamii juu ya athari za uchafuzi wa mazingira.

NEMC imesisitiza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi yenye mazingira safi na salama kwa wote.

Picha ya pamoja ya watumishi wa NEMC, DEPO, Hospitali ya Mwananyamala na wakazi wa Mwananyamala mara baada ya zoezi la Usafi wa Mazingira ya Hospitali hiyo ikiwa ni sehemu katika kuadhimisha siku ya Usafi Duniani.

NEMC YAINGIA MTAANI KIDIGITALI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa kushirikiana na Halmashauri za Mkoa wa Dar es salaam  linaendesha zoezi maalumu la Ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi yote ya maendeleo kwa kutumia mfumo maalumu wa kidigitali uitwao 'Mazingira App'.

Akitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti amesema zoezi hilo litadumu kwa wiki nne na litahusisha kaguzi za Mazingira kwenye miradi ya maendeleo hususani kuangalia uzingatiaji wa matakwa ya Usimamizi wa Mazingira kama vile usimamizi wa taka, matumizi sahihi ya ardhi pamoja na  uhifadhi wa vyanzo vya maji.

Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti (wa kwanza kushoto) akitoa taarifa kwa Vyombo vya Habari kuhusu zoezi maalumu la Ukaguzi wa Mazingira kwa Miradi yote ya maendeleo kwa kutumia mfumo maalumu wa kidigitali uitwao 'Mazingira App'.

Ameongeza kwa kutumia mfumo wa Mazingira App pia utawawezesha kuchunguza uzingatiaji wa Sheria zinazohusu afya ya jamii, usalama wa kazi na mipango miji  ambazo kwa kutokutekelezwa kwake huchangia kwa kiasi kikubwa uchafuzi au uharibifu wa mazingira.

Aidha Bw. Jamal Baruti amesema ushirikiano na uongozi wa Jiji la Dar es salaam umelenga kuongeza uelewa na ufanisi kwa maafisa mazingira kuhusu Usimamizi hafifu wa taka ngumu, changamoto ya taka za plastiki, uharibifu wa Mazingira kutokana na uchimbaji holela wa kwenye mito na mabonde na matumizi holela ya ardhi kinyume na taratibu za mipangomiji.

Kwa upande wake Meneja Kanda ya Kaskazini Mashariki (NEMC) Bi. Glory Kombe alipozungumza amewataka Viongozi wa Halmashauri na Serikali za mitaa kutoa ushirikiano wakati wote wa zoezi hili ili kufikia tija tarajiwa kwa maendeleo endelevu ya Mazingira nchini.

Kadhalika Meneja Glory Kombe amefafanua  kuwa jukumu la Halmashauri na Mamlaka za Serikali za mitaa ni kuhakikisha Miradi ya maendeleo inazingatia taratibu za Mazingira ikiwemo ufanyikaji wa Tathmini ya Mazingira na Jamii kama ilivyobainishwa kwenye Sheria ya Mazingira na Kanuni zake na kusimamia usafi wa Mazingira kwa ujumla pamoja na kuwataka maofisa Mazingira na Kamati za Mazingira kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Sheria.

Meneja Kanda ya Kaskazini Mashariki Bi. Glory Kombe (wa kulia) akichangia mada katika Mkutano huo
Meneja Uzingatiaji wa Sheria (NEMC)Bw. Hamadi Taimuru (wa kulia) akichangia mada katika Mkutano huo

 NEMC imeanzisha mfumo huo wa Mazingira app' ambao ni wa kidigitali ili kurahisisha na kuongeza  ufanisi katika ukusanyaji na uhifadhi wa Taarifa za Miradi pamoja na usajili wa Miradi mipya ambapo zitachangia Baraza na Serikali kupanga na kusimamia Miradi ya maendeleo kwa ufanisi zaidi.



NEMC YAKAGUA MGODI WA 'URANIUM' MKOANI RUVUMA UNAOTARAJIWA KUANZA 2026

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lilifika na kukagua Mgodi wa madini aina ya Uranium uliopo katika Wilaya ya Namtumbo Mkoani Ruvuma ambao ulikuwa katika Uchimbaji mdogo wa majaribio huku Uchimbaji mkubwa ukitarajiwa kuanza mwaka 2026.

NEMC ilifika na kufanya Ukaguzi katika Mgodi huo na kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha shughuli za Uchimbaji katika Mgodi huo haziathiri Mazingira, Viumbe hai na wakazi wa jirani na Mgodi huo ikiwa ni agizo la Serikali.

Awali NEMC ilianza kwa kutoa elimu ya Mazingira na Afya kwa wakazi wa vijiji vilivyo karibu na Mgodi huo ili kuwajengea uelewa kuhusiana na madini ya 'Uranium' jinsi yanavyoweza kuhatarisha afya na Mazingira ikiwa hayata chakatwa na kudhibitiwa kwa umakini.

Akizungumza katika Ukaguzi huo Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria Bw. Jamal Baruti alisema NEMC ilifika katika Mgodi huo kufanya Ukaguzi ili kutathmini ikiwa wawekezaji katika Mgodi huo wamekidhi na kuzingatia miondombinu ya Mazingira ambayo haita haribu Mazingira, kuhatarisha usalama wa wakazi na wafanyakazi katika Mgodi huo kabla Uchimbaji mkubwa haujaanza.

Timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC na Kampuni ya Uchimbaji ya MANTRA wakikagua moja ya mlima wenye madini ya  'Urunium' wakati wa ukaguzi wa Mgodi huo. Wa pili kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bw. Jamal Baruti.

Aidha Bw. Baruti alieleza kuwa Mradi wa Mgodi huo utakuwa na uwezo wa kuzalisha tani elfu 27 kwa siku na utakuwa ni Mradi mkubwa wa Uchimbaji madini nchini ukilinganisha na Miradi mingine nchini Tanzania.

Aliongeza kuwa Tanzania  itakuwa nchi ya nne ya uzalishaji wa madini ya 'Uranium' Duniani huku akiwasisitiza wawekezaji na wananchi kuzingatia uhifadhi Mazingira na si tu kuangalia manufaa ya Mgodi huo.

Meneja wa Kampuni ya MANTRA Bw. Beria Vorster akitoa maelezo kwa wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC wakati wa ukaguzi wa mtambo wa kuchenjua madini ya 'Urunium' ikiwa ni sehemu ya Ukaguzi wa Mgodi huo.

Kwa upande wake Meneja Kanda ya Kusini (NEMC) Bw. Boniface Guni alisema ziara hiyo iliwasaidia NEMC kupata picha ya Mradi huo ambayo itawasaidia kusimamia Mpango wa Usimamizi wa Mazingira na jamii ipasavyo.

Naye Mwenyekiti wa Kitongoji cha Buchushu Kijiji cha Iguseka Bw. Omary Rashid aliishukuru NEMC kwa kuwapatia elimu hiyo adhimu ya Mazingira wakazi wa vijiji hivyo ambayo ni muhimu katika utunzaji wa Mazingira na Afya ya binadamu.

Timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC na Kampuni ya Uchimbaji ya MANTRA wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya ukaguzi wa Mgodi wa madini ya 'Urunium' katika eneo la Mto Mkuju Wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma. Wa katikati ni Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria NEMC Bw. Jamal Baruti na kushoto kwake ni Meneja wa Mradi Bw. Beria Vorster

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...