Nyumbani

NEMC YAKUTANA NA MAKAMU WA RAIS MHE. BALOZI DKT. EMMANUEL JOHN NCHIMBI DODOMA

Ni katika kikao kazi cha kupitishana kwenye majukumu ya Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekutana na  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi kwenye kikaokazi cha kwanza na watendaji wake tangu kuteuliwa kwake chenye lengo la kupitishana kwenye majukumu ya utekelezaji wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi yake.

Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi akizungumza na watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na watumishi waliochini ya Ofisi hiyo wakiwemo NEMC katika kikaokazi cha kwanza tangu kuteuliwa kwake

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma kilihusisha Menejimenti na  watumishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Menejimenti ya Baraza pamoja na watendaji kutoka kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa masuala ya Carbon.

Akizungumza katika kikao hicho Balozi Dkt Emmanuel Nchimbi amesema ni kikao cha kukumbushana wajibu tulionao kwa watanzania wa kudumisha Muungano pamoja na kusimamia masuala mazima ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini hasa ikizingatiwa dira ya maendeleo ya 2050 kipengele cha tatu kimezingatia masuala ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira pamoja na Ustahimilivu wa masuala mazima ya mabadiliko ya Tabianchi.

 " Dhamana tuliyopewa ni kubwa, masuala ya Muungano, kutunza mazingira na uchumi wa buluu si vitu vya mchezo, ni lazima tumsaidie Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya siku miamoja (100) kutekeleza maagizo yahusuyo Muungano na Mazingira, tunao wajibu wa kuhakikisha Mazingira yanasimamiwa na kuhifadhiwa" Amesema Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi.

Ametoa maagizo yafuatayo: kila mtumishi aisome ilani ya chama kilichopo madarakani pamoja na dira ya maendeleo ya 2050 kwani ndio msingi wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali, masuala ya Muungano na Mazingira, Uchumi wa buluu, Carbon trade na nishati safi yasimamiwe na kutekelezwa kwa weledi,  malengo yote ya utekelezaji wa shughuli za Muungano na Mazingira yawe na namna sahihi ya ufuatiliaji na utekelezaji wake ili kufikia azma iliyokubaliwa.

Maagizo mengine ni kuandaa  mkakati wa mawasiliano utakaotoa muongozo wa namna ya kutangaza shughuli za mazingira, kuzingatia haki na stahiki za watumishi, kuhakikisha vijana wanaelewa maana halisi ya Muungano na kuuenzi pamoja na wakuu wa Taasisi kusimamia Sheria na  miongozo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Awali akimkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema NEMC inahitaji kupewa meno kwani kero za Mazingira zimekuwa nyingi hasa uchafuzi wa vyanzo vya maji na kelele chafuzi za Mazingira.

"Hakuna kitu kinanikera kama pale ocean road kila nikipita napakuta pachafu, panatoa harufu, matakataka yamezagaa, nikiwauliza NEMC.wanasema hawana meno" Mhe. Mhandisi Hamad Masauni.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Cyprian Luhemeja alipozungumza aliahidi kuyasimama na kuyatekeleza maagizo na maelekezo yote yaliyotolewa  kwa kushirikiana na watendaji wa Taasisi zote zilizo chini ya ofisi ya Makamu wa Rais.

Kikao kazi hicho kimehudhuriwa pia na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange, Naibu Katibu Mkuu Mazingira Profesa Peter Msoffe na Naibu Katibu Mkuu Muungano Bw. Abdallah H. Mitawi.




𝐍𝐄𝐌𝐂 𝐘𝐀𝐄𝐍𝐙𝐈 𝐌𝐀𝐀𝐃𝐇𝐈𝐌𝐈𝐒𝐇𝐎 𝐘𝐀 𝐒𝐈𝐊𝐔 𝐘𝐀 𝐖𝐀𝐋𝐄𝐌𝐀𝐕𝐔 𝐃𝐔𝐍𝐈𝐀𝐍𝐈

𝐘𝐚𝐬𝐡𝐢𝐤𝐚  𝐦𝐤𝐨𝐧𝐨 𝐊𝐢𝐭𝐮𝐨 𝐜𝐡𝐚 𝐄𝐫𝐢𝐜 𝐌𝐞𝐦𝐨𝐫𝐢𝐚𝐥 𝐌𝐨𝐫𝐨𝐠𝐨𝐫𝐨

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kupitia timu yake ya wanamichezo wanaoshiriki mashindano ya SHIMMUTA 2025 wametembelea Kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu cha Erick Memorial mkoani Morogoro Disemba 4, 2025.

Timu hiyo ya NEMC ilipata fursa ya kutembelea, kufariji na kuwapa misaada ya vyakula na vifaa vya usafi pamoja na kutoa elimu ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira ikiwa ni sehemu ya kuienzi siku maalumu ya walemavu ambapo duniani kote hufanyika tarehe 3 Disemba ya kila mwaka.

Akizungumza kwenye kituo hicho kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Afisa Utumishi Mkuu wa NEMC Bi. Shukrani Haule amesema Baraza linaendelea kushirikiana na watu wa makundi yote katika kuhakikisha Mazingira yanakuwa safi na  salama kwa watu wote, lakini pia kihakikisha makundi haya yanawezeshwa na kujumuishwa katika maamuzi yanayozingatia Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira nchini.

"Baraza katika kutekeleza majukumu yake linashirikiana na watu wote na kundi hili la watu wenye ulemavu limekuwa likilizingatiwa siku zote katika mipango yake yote" Amesema Bi. Shukrani.

Naye Mtendaji wa Taasisi hiyo ya Eric Memorial, Bw. Robert Mkalawa ametoa wito kwa Taasisi za Serikali kuona umuhimu wa siku hii kama ambayo NEMC imefanya.

"Tunashukuru kutembelewa Taasisi inayohusika na Mazingira ambao ni NEMC na hii inadhihirisha kuwa hakuna Mazingira bila watu na watu wenyewe ndio sisi bila kubagua, lakini nitoe rai kwa Taasisi nyingine za Serikali kuiga mfano wa NEMC katika kuadhikisha siku hii ya Walemavu Duniani". Amesema Bw. Robert.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa Michezo NEMC Bw. Fortinatus Patrick amesema kilichofanyika ni muendelezo wa kile alichokisisitiza Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi katika kuweka Mazingira wezeshi kwa makundi yote kujumuisha jamii za watu wenye ulemavu katika kuhifadhi Mazingira nchini.



NEMC NA TAASISI YA CSE WAENDESHA MAFUNZO YA NAMNA YA KUTENGENEZA ORODHA YA TAKA ZA VIWANDANI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira- NEMC, kwa kushirikiana na Taasisi ya Centre of Science and Environment ( CSE) ya India imefanya mafunzo juu ya mbinu za kutengeneza Orodha ya Taka za Viwandani. 

Lengo ni kutengeneza orodha ya viwanda vyote nchini pamoja na taka zinazozalishwa na viwanda hivyo ili kuboresha usimamizi wa taka. 

Aidha, jambo hili linaenda kuchangia kwenye sera ya Taka ni Uchumi ( Circular economy) kwa kubaini aina ya taka na viwanda vinavyoweza kuchakata au kutumia taka hizo.

NEMC YASAINI MAKUBALIANO YA AWALI NA UPS KUANZISHA MFUMO WA KIDIGITALI WA UFUATILIAJI WA UCHAFUZI WA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesaini makubaliano ya awali na Kampuni ya United Platform Solution (UPS) kwa ajili ya kuanzisha mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji wa uchafuzi wa mazingira katika miradi yote ya maendeleo nchini.

Hafla hiyo ya kusaini makubaliano hayo imefanyika Disemba 04,2025 katika ukumbi wa mikutano wa Baraza uliopo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Bw. Dickson Mjinja ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Fedha, amesema Baraza limefikia hatua hiyo ili kurahisisha masuala mazima ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira kwani mfumo huo ukikamilika utarahisisha kubaini viashiria vya uchafuzi wa mazingira na kupata taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu hali ya mazingira.

Naye Bw Mamadou Drame kutoka UPS alipozungumza amesema imekuwa azma yao kushirikiana na NEMC katika kuhakikisha uchafuzi wa Mazingira unadhibitiwa kidigitali ili kuyalinda kwa maendeleo endelevu.

Akifafanua namna mfumo huo utakavyotenda kazi, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria wa NEMC, Bw. Jamal Baruti amesema  kwa sasa utaanza mradi wa majaribio ambapo vifaa maalum vitawekwa katika miradi ya mazingira ikijumuisha miradi iliyopo katika Kanda 13 za NEMC nchi nzima hali itakayoimarisha zaidi usimamizi na Uhifadhi wa mazingira nchini.





NEMC YAUNGANA NA WATANZANIA WOTE KUADHIMISHA SIKU YA WALEMAVU DUNIANI

Yasisitiza mazingira jumuishi kwa ustawi wa walemavu 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) leo limeungana na jumuiya ya kimataifa kuadhimisha Siku ya Walemavu Duniani kwa kutoa wito wa kuimarishwa kwa mazingira jumuishi na rafiki kwa watu wote, hususani watu wenye ulemavu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema kuwa jitihada za kulinda mazingira haziwezi kuwa endelevu pasipo kuhakikisha ushiriki wa watu wenye ulemavu katika mipango na maamuzi yahusuyo mazingira.

“Haki ya kuishi katika mazingira safi, salama na yenye afya ni ya kila mtu. Tunajivunia kuwa sehemu ya juhudi za kuhakikisha miundombinu na huduma za kimazingira zinakuwa salama na zinazofikika kwa watu wenye ulemavu,” alisema Dkt. Semesi.

 Ujenzi wa Miundombinu Rafiki 

Baraza limeendelea kuhimiza Taasisi za umma na binafsi kutekeleza ujenzi shirikishi (inclusive design) ili kuhakikisha njia za kupita, majengo, vyoo na vifaa vya kimazingira vinapatikana na kutumika na watu wote bila vikwazo.

 Ushirikishwaji Katika Maamuzi 

Kwa kutambua umuhimu wa uwakilishi, NEMC imeweka mikakati inayolenga kuwahusisha watu wenye ulemavu katika kamati na majadiliano muhimu ya usimamizi wa mazingira katika ngazi mbalimbali za Taifa.

 Ulinzi Dhidi ya Hatari za Kimazingira 

Baraza pia linaimarisha mifumo ya tahadhari dhidi ya majanga kama mafuriko, uchafuzi na taka hatarishi, likibainisha kuwa watu wenye ulemavu mara nyingi hukumbwa kwa kiwango kikubwa zaidi na madhara ya majanga hayo. Mwongozo unaotolewa kwa mamlaka za mitaa unalenga kuhakikisha mipango ya dharura inawalinda na kuwatambua kikamilifu.

Elimu na Uhamasishaji

Kupitia ushirikiano na wadau mbalimbali, Baraza linaendeleza kampeni za elimu na uhamasishaji kuhusu umuhimu wa mazingira safi na salama kwa ajili ya ustawi wa watu wenye ulemavu, sambamba na kukuza mtazamo chanya katika jamii.

Dkt. Semesi alihitimisha kwa kusisitiza dhamira ya NEMC katika kuhakikisha sera na miradi ya mazingira nchini inatekelezwa kwa kuzingatia usawa na ujumuishaji.

“Hakuna mtu anayepaswa kuachwa nyuma katika kunufaika na rasilimali za mazingira. Ustawi wa watu wenye ulemavu ni sehemu ya ustawi wa Taifa,” alisema.

𝐍𝐄𝐌𝐂 𝐘𝐀𝐄𝐍𝐃𝐄𝐒𝐇𝐀 𝐌𝐀𝐅𝐔𝐍𝐙𝐎 𝐊𝐔𝐇𝐔𝐒𝐔 𝐍𝐘𝐄𝐍𝐙𝐎 𝐙𝐀 𝐔𝐒𝐈𝐌𝐀𝐌𝐈𝐙𝐈 𝐖𝐀 𝐌𝐀𝐙𝐈𝐍𝐆𝐈𝐑𝐀 𝐊𝐖𝐀 𝐖𝐈𝐙𝐀𝐑𝐀, 𝐓𝐀𝐀𝐒𝐈𝐒𝐈 𝐍𝐀 𝐇𝐀𝐋𝐌𝐀𝐒𝐇𝐀𝐔𝐑𝐈 𝐙𝐀 𝐌𝐀𝐍𝐈𝐒𝐏𝐀𝐀 𝐍𝐀 𝐖𝐈𝐋𝐀𝐘𝐀

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linaendeaha mafunzo kuhusu nyenzo za usimamizi wa mazingira kwa Wizara, Taasisi pamoja na Halmashauri za Manispaa na Wilaya nchini. Mafunzo haya yameandaliwa kupitia Mradi wa kujenga uwezo wa kitaifa katika kusimamia Sheria ya usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004. Mradi huu unafadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA). Mradi unalenga kuimarisha uelewa na uwezo wa watumishi katika kusimamia Sheria ya mazingira kwa ufanisi katika utekelezaji wa majukumu katika maeneo yao ya kazi.


Mafunzo hayo ya siku mbili yameanza tarehe 27 na kumalizika 28 Novemba 2025 jijini Dodoma. Kupitia mafunzo haya, washiriki wanapata maarifa ya kutathmini athari za kimazingira pamoja na kupanga mikakati endelevu ya utunzaji wa mazingira huku wakizingatia Nguzo ya tatu ya Dira ya maendeleo ya Taifa 2050 ambayo imeweka mkazo juu ya kuzingatia masuala ya utunzaji wa Mazingira nchini.

Akifungua mafunzo hayo, Meneja wa maeneo maalum na mabadiliko ya tabianchi kutoka NEMC, Dkt. Careen Kahangwa, aliwataka washiriki kutumia fursa hiyo kuboresha utendaji katika maeneo yao ya kazi. Mafunzo haya yanaendeshwa na timu ya wataalamu kutoka NEMC. Aidha wataalamu kutoka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ofisi ya Makamu wa Rais na taasisi binafsi ya Taka ni ajira nao walishiriki Katika kutoa mafunzo.

Washiriki wa mafunzo hayo wamepata nafasi ya kujadili kwa kina changamoto za kimazingira zinazojitokeza katika taasisi zao na kujifunza mbinu bora za kukabiliana nazo. Kupitia mafunzo haya, wanatarajiwa kuboresha mifumo ya ufuatiliaji, utoaji taarifa, na utekelezaji wa sheria na kanuni za mazingira nchini. Hatua hii muhimu itachangia kwa kiasi kikubwa kulinda na kuhifadhi mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.







𝐃𝐊𝐓. 𝐅𝐄𝐒𝐓𝐎 𝐃𝐔𝐆𝐀𝐍𝐆𝐄 𝐀𝐙𝐔𝐍𝐆𝐔𝐌𝐙𝐀 𝐍𝐀 𝐖𝐀𝐓𝐔𝐌𝐈𝐒𝐇𝐈 𝐖𝐀 𝐍𝐄𝐌𝐂

𝐀𝐬𝐢𝐬𝐢𝐭𝐢𝐳𝐚 𝐔𝐡𝐢𝐟𝐚𝐝𝐡𝐢 𝐧𝐚 𝐔𝐬𝐢𝐦𝐚𝐦𝐢𝐳𝐢 𝐰𝐚 𝐌𝐚𝐳𝐢𝐧𝐠𝐢𝐫𝐚 𝐡𝐚𝐬𝐚 𝐮𝐝𝐡𝐢𝐛𝐢𝐭𝐢 𝐰𝐚 𝐤𝐞𝐥𝐞𝐥𝐞 𝐜𝐡𝐚𝐟𝐮𝐳𝐢 𝐦𝐚𝐞𝐧𝐞𝐨 𝐲𝐚 𝐦𝐚𝐤𝐚𝐳𝐢


Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais  (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange, amefanya ziara yake ya kwanza katika Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na kuzungumza na watumishi wa Baraza hilo, akitoa maelekezo mahsusi juu ya kuimarisha usimamizi wa mazingira nchini.

Katika hotuba yake, Dkt. Dugange amesisitiza umuhimu wa kulinda afya ya jamii kupitia udhibiti wa kelele chafuzi, akibainisha kuwa kelele zimekuwa chanzo cha changamoto za kiafya, hususani magonjwa yasiyoambukiza katika maeneo ya makazi.

Amesema kelele chafuzi ni miongoni mwa mambo yanayoashiria uharibifu wa mazingira na yanapaswa kudhibitiwa kwa nguvu na umakini wa hali ya juu.

Akiweka msisitizo zaidi, Dkt. Dugange ameagiza NEMC kuandaa mpango mkakati wa mashirikiano  kati yake na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) hasa kwenye majiji  ili kuhakikisha udhibiti wa kelele chafuzi unatekelezwa katika ngazi zote kutoka Mtaa hadi Taifa. 

Amesisitiza  kuwa kila mtumishi wa NEMC ana jukumu la kuhakikisha jamii inajengewa uelewa na Sheria za Mazingira zinatekelezwa ipasavyo.

Katika mazungumzo hayo, Dkt. Dugange pia ameuzungumzia Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa 2050 unaohusisha nguzo tatu kuu, ikiwemo Uhifadhi wa Mazingira na Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi

Amefafanua uhusiano uliopo kati ya mazingira salama, afya bora, na kupungua kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Akigusia ajenda ya nishati safi, Dkt. Dugange alikumbusha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inataka ifikapo mwaka 2034, asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ambayo ina manufaa kwa jamii ikiwemo kupunguza uchafuzi wa hewa, kulinda mazingira na kupunguza gharama za maisha.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Mhandisi Mwanasha Tumbo, ameahidi kusimamia utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt.Immaculate Sware Semesi amepokea maelekezo na kuahidi kuyatekeleza kwa mujibu wa Sheria na kuhakikisha usimamizi thabiti wa mazingira nchini.



NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...