Nyumbani

NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA 48 CHA KAMATI YA URITHI WA DUNIA YA UNESCO - BUSAN KOREA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kupitia Mkurugenzi Mkuu wake, Dkt. Immaculate Semesi, linashiriki katika Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia ya UNESCO (48th Session of the World Heritage Committee) kinachofanyika jijini Busan, Jamhuri ya Korea.

Kikao hicho kinawakutanisha wajumbe kutoka Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972, pamoja na wadau mbalimbali wa kimataifa, kwa lengo la kupitia, kujadili na kufanya maamuzi kuhusu masuala ya uhifadhi, usimamizi na maendeleo endelevu ya maeneo ya Urithi wa Dunia. Vilevile, kikao kinatoa fursa ya kutathmini hali ya uhifadhi wa maeneo yaliyopo kwenye Orodha ya Urithi wa Dunia, kuzingatia mapendekezo ya maeneo mapya yanayostahili kuorodheshwa, pamoja na kujadili changamoto zinazoathiri urithi wa asili na wa kiutamaduni duniani, ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la shughuli za kibinadamu na uendelezaji usiozingatia misingi ya uhifadhi.

Ushiriki wa NEMC katika mkutano huu unaakisi dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuendelea kutekeleza kikamilifu Mkataba wa Urithi wa Dunia wa mwaka 1972, kuimarisha usimamizi wa maeneo ya urithi wa dunia nchini, na kuendeleza ushirikiano wa kimataifa katika kuhifadhi urithi wa asili na wa kiutamaduni wenye thamani ya kipekee kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

Katika mkutano huo, Dkt. Semesi anawakilisha Tanzania katika mijadala mbalimbali inayohusu uhifadhi wa maeneo ya Urithi wa Dunia, usimamizi wa mifumo ya ikolojia, uhifadhi wa bioanuwai, pamoja na matumizi ya mbinu za kisayansi na mifumo bora ya usimamizi wa mazingira ili kuhakikisha maeneo hayo yanaendelea kuhifadhiwa kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

Aidha, ushiriki wa Tanzania ukiongozwa na Mheshimiwa Balozi Saidi Yakubu,Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu UNESCO na kuhudhuriwa pia na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera na Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji ( Mb),unatoa fursa ya kuimarisha ushirikiano wa kitaalamu na taasisi za kimataifa kama UNESCO na IUCN, kubadilishana uzoefu na nchi nyingine kuhusu mbinu bora za uhifadhi wa maeneo ya urithi, pamoja na kutafuta fursa za ushirikiano wa kiufundi na kifedha kwa ajili ya kuimarisha uhifadhi na usimamizi wa maeneo ya Urithi wa Dunia nchini Tanzania.

Tanzania ni miongoni mwa Mataifa Wanachama wa Mkataba wa Urithi wa Dunia na inajivunia kuwa na maeneo kadhaa yaliyotambuliwa na UNESCO kuwa ni Urithi wa Dunia kutokana na thamani yake ya kipekee ya kimataifa. Ushiriki wa NEMC katika kikao hiki unaimarisha nafasi ya Tanzania katika mijadala ya kimataifa kuhusu uhifadhi wa mazingira na urithi wa dunia, sambamba na kuendeleza diplomasia ya mazingira na kukuza mchango wa nchi katika utekelezaji wa ajenda za maendeleo endelevu duniani.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA 48 CHA KAMATI YA URITHI WA DUNIA YA UNESCO - BUSAN KOREA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kupitia Mkurugenzi Mkuu wake, Dkt. Immaculate Semesi, linashiriki katika Kikao ...