Nyumbani

NEMC NA IUCN WAKUSANYA MAONI YA WADAU KUHUSU RASIMU YA KANUNI ZA WAJIBU WA MZALISHAJI WA BIDHAA (EPR)

 


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na IUCN, limeanza mkutano wa siku mbili wa wadau kuhusu Rasimu ya Kanuni ya Wajibu wa Mzalishaji wa Bidhaa (Extended Producer Responsibility - EPR) katika Usimamizi wa Taka na Uhifadhi wa Mazingira. Mkutano huo umeanza rasmi tarehe 21 Julai 2026 mkoani Dodoma na unalenga kukusanya maoni ya wadau ili kuboresha rasimu ya kanuni hiyo kabla ya kukamilishwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Bw. Fredrick Mulinda, ambaye ni Afisa Mazingira Mkuu wa NEMC, amesema mkutano huo ni muhimu katika kujadili na kutoa maoni kuhusu Rasimu ya Kanuni za Wajibu wa Mzalishaji wa Bidhaa (EPR) katika Usimamizi wa Taka na Uhifadhi wa Mazingira. Amesema mkutano huo unaonesha dhamira ya pamoja ya Serikali na wadau mbalimbali katika kuimarisha usimamizi endelevu wa mazingira nchini kupitia mfumo utakaoweka wajibu kwa wazalishaji wa bidhaa katika usimamizi wa taka zinazotokana na bidhaa zao.

Aidha, Bw. Mulinda ameishukuru IUCN kwa ushirikiano wake wa karibu na NEMC katika kufanikisha maandalizi ya mkutano huo na kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhifadhi na kusimamia mazingira. Pia amewapongeza wataalamu wa NEMC na wadau wote walioshiriki maandalizi ya mkutano huo muhimu, akisisitiza kuwa ushirikiano wao utachangia kupatikana kwa kanuni imara zitakazoboreshwa kupitia maoni ya wadau.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

NEMC YASHIRIKI KIKAO CHA 48 CHA KAMATI YA URITHI WA DUNIA YA UNESCO - BUSAN KOREA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kupitia Mkurugenzi Mkuu wake, Dkt. Immaculate Semesi, linashiriki katika Kikao ...