Nyumbani

MRADI WA KIHANSI MKOMBOZI WA MAZINGIRA KWA WANANCHI WA MLIMBA

 Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuanzia Machi 9 hadi 16 linafanya ufuatiliaji katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), Taasisi ya Utafiti wa Kahawa Tanzania (TaCRI), Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na Halmashauri za Wilaya ya Mlimba, Kilolo na Mafinga kwa lengo la kutathmini mafanikio ya Mradi wa Kihansi ambao umechangia kwa kiasi kikubwa katika uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii.

Mradi huo ulitekelezwa kuanzia mwaka 2001 hadi 2019 kupitia awamu tatu ambazo ni Lower Kihansi Environmental Management Project (LKEMP I na II) pamoja na Kihansi Catchment Conservation Management Project (KCCMP). Miradi hiyo ililenga kuimarisha uhifadhi wa baioanuai katika bonde la Kihansi pamoja na kulinda vyanzo vya maji.

Kupitia miradi hiyo, wananchi walipewa elimu ya uhifadhi wa mazingira na kuwezeshwa kufanya shughuli za kilimo nje ya vyanzo vya maji ili kupunguza uharibifu wa mazingira. Miradi hiyo ilitekelezwa chini ya uratibu na usimamizi wa NEMC kwa kushirikiana na taasisi za utafiti na wadau wengine.

Aidha, wananchi wa Halmashauri hizo waliwezeshwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi kupitia vikundi, ikiwemo kilimo cha mpunga, kilimo cha miti, ufugaji wa nyuki na ufugaji wa samaki. Hatua hiyo imechangia kuongeza kipato na kuboresha ustawi wa kaya nyingi katika maeneo hayo.

Kutokana na uwezeshaji huo, baadhi ya wanufaika wamefanikiwa kujenga nyumba bora, kusomesha watoto, kuongeza ukubwa wa mashamba ya kilimo pamoja na kumiliki mifugo, jambo ambalo limeimarisha ustawi wa familia zao na jamii kwa ujumla.

Mmoja wa wanufaika wa mradi huo, Bw. Philiscacius Shaban Masongela, ameishukuru NEMC kwa mchango wake katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia miradi ya uhifadhi na uwezeshaji wa kiuchumi. “Kupitia mradi huu nimeweza kuongeza kipato, kujenga nyumba nzuri, kukuza shamba la mpunga na kumiliki mifugo. Hakika mradi huu umeleta mabadiliko chanya katika maisha yetu,” amesema Bw. Masongela.

Naye Bi. Pudensiana Valentine Chagawe kutoka Kikundi cha Nguvu Kazi katika Kijiji cha Chita, Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, amesema elimu ya shamba darasa aliyopatiwa kupitia mradi huo imemwezesha kutumia mbinu za kilimo cha kisasa na kuongeza uzalishaji wa mazao. “Awali nilikuwa napata takribani debe 30 (magunia matatu) za mpunga katika nusu heka, lakini baada ya kupata mafunzo ya shamba darasa na kutumia mbinu bora za kilimo, uzalishaji umeongezeka hadi kufikia debe 180 (magunia 18). Hii imenisaidia kuongeza kipato na kuboresha maisha ya familia yangu,” amesema Bi. Chagawe.

Timu ya NEMC imewapongeza wananchi wa maeneo hayo kwa kuendelea kutumia maarifa na ujuzi walioupata kupitia Mradi wa Kihansi katika kuboresha shughuli zao za kiuchumi, kuinua vipato vya familia zao hiki wakitunza mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗙𝗨𝗡𝗚𝗜𝗔 𝗨𝗝𝗘𝗡𝗭𝗜 𝗪𝗔 𝗠𝗔𝗝𝗘𝗡𝗚𝗢 𝗠𝗔𝗪𝗜𝗟𝗜 𝗠𝗜𝗞𝗢𝗖𝗛𝗘𝗡𝗜

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limefungia ujenzi wa majengo mawili yaliyokuwa yanaendelea kujengwa katika eneo la Mikocheni, mtaa wa Regent, mkoani Dar es Salaam, kufuatia ukiukwaji wa taratibu za usimamizi wa mazingira. Majengo yaliyosimamishwa ni pamoja na VIENNATANZANIA CO LTD na TAFBROS LIMITED

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya kubainika kuwa miradi hiyo ilikuwa inaendelea kuwa na vibali vya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA). NEMC imeagiza kusimamishwa mara moja kwa shughuli zote za ujenzi hadi taratibu zote za kisheria zitakapokamilika.

Hata hivyo NEMC imetoa angalizo kwa niradi yote inayoendelezwa bila kufata taratibu za Mazingira kusitisha na kufika ofisi za NEMC kwaajili ya kuanza mchakato wa Uzingatiaji wa Sheria kabla ya kukaguliwa na kupewa adhabu.





NEMC NA THPS WAJADILI USHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA AFYA YA JAMII YA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Taasisi ya Tanzania Health Promotion Support (THPS) wamefanya kikao cha pamoja kuhusu ushirikiano katika masuala ya usimamizi wa mazingira na afya ya jamii tarehe 10 Machi 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Baraza jijini Dar es Salaam. 

Katika kikao hicho, pande zote mbili zimejadiliana na kukubaliana kushirikiana katika kujengea wadau uelewa kuhusu afya ya binadamu na mazingira, kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, kuimarisha tafiti kuhusu uhusiano kati ya mazingira na afya ya binadamu, pamoja na kuboresha usimamizi endelevu wa taka zitokanazo na huduma za afya.

Ushirikiano huu unalenga kuunga mkono juhudi za Taifa katika kulinda mazingira, kuboresha afya ya jamii na kuchochea maendeleo endelevu sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayosisitiza umuhimu wa mazingira salama na jamii yenye afya kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗦𝗛𝗜𝗥𝗜𝗞𝗜 𝗞𝗜𝗞𝗔𝗢 𝗞𝗜𝗟𝗜𝗖𝗛𝗢𝗔𝗡𝗗𝗔𝗟𝗜𝗪𝗔 𝗡𝗔 𝗕𝗘𝗡𝗞𝗜 𝗬𝗔 𝗗𝗨𝗡𝗜𝗔-𝗗𝗢𝗗𝗢𝗠𝗔

𝗟𝗲𝗻𝗴𝗼 𝗻𝗶 𝗸𝘂𝗷𝗮𝗱𝗶𝗹𝗶 𝗨𝘁𝗲𝗸𝗲𝗹𝗲𝘇𝗮𝗷𝗶 𝘄𝗮 𝗧𝗮𝘁𝗵𝗺𝗶𝗻𝗶 𝘆𝗮 𝗦𝗲𝗸𝘁𝗮 𝘆𝗮 𝗠𝗮𝗱𝗶𝗻𝗶 𝗻𝗰𝗵𝗶𝗻𝗶

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikao kilichoandaliwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Wizara ya Madini kilicholenga kujadili na kupata uelewa wa pamoja kuhusu utekelezaji wa Tathmini ya Sekta ya Madini nchini inayojulikana kama Mining Sector Diagnostic (MSD) 


Kikao hicho kilichofanyika tarehe 10 Machi 2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Best Western jijini Dodoma kiliwakutanisha wadau kutoka Wizara, Taasisi na Wakala za Serikali.

Tathmini ya MSD inalenga kuchambua namna shughuli za Sekta ya madini zinavyotekelezwa na kusimamiwa, hususan kwa kuzingatia masuala ya Sheria, Kanuni, mifumo ya kikodi pamoja na uwezo wa Taasisi mbalimbali za Serikali katika kusimamia Sekta hiyo.

Matokeo ya tathmini ya MSD yataisaidia Benki ya Dunia kutambua kwa kina mchango wa Sekta ya madini katika maendeleo ya Taifa, pamoja na kubaini maeneo yanayohitaji kuboreshwa.

Kupitia matokeo hayo, mapendekezo yatatolewa kuhusu namna bora ya kuimarisha ufanisi wa Sekta hiyo kwa kufanya maboresho ya sera, mifumo ya usimamizi na kuboresha mazingira ya uwekezaji.



NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA NANE WA AFRIMAB NCHINI ZAMBIA

NEMC yashiriki Makutano wa nane wa AfriMab (8th AfriMAB General Assembly) uliofanyika jijini Livingstone, Zambia kuanzia tarehe 9 hadi 13 Machi 2026. Madhumuni ya mkutano huo ni kuendeleza usimamizi endelevu wa hifadhi za bayosfia barani Afrika chini ya kaulimbiu “Kutumia rasilimali za asili za Afrika kupitia teknolojia rafiki kwa mifumo ya ikolojia.” NEMC imewakilishwa na Bi. Marlene Moshi, Afisa Mkuu Mazingira







NEMC KANDA YA KASKAZINI YAKAGUA KIWANDA CHA SARUJI CHA MOSHI CEMENT

NEMC Kanda ya Kaskazini yafanya ukaguzi kiwanda cha kutengeneza Saruji cha Moshi Cement kinachoendeshwa na Kampuni ya JUN YU INVESTMENT INTERNATIONAL CO. LTD kilichopo katika Mkoa wa Kilimanjaro karibu na mpaka wa Horiri. 

Timu ya ukaguzi ilibaini kuwa Kiwanda hicho kina cheti cha TAM, pia kina teknolojia madhubuti ya kudhibiti vumbi na kiwanda chote kimesakafiwa (paved). Hata hivyo kulikuwa na changamoto chache hasa namna ya  udhibiti wa chuma chakavu na usimamizi usiofaa wa madumu yaliyomaliza kemikali. 

Timu ya wataalam ilitoa maelekezo stahiki na muda wa utekelezaji ili kukabiliana na changamoto zilizoibuliwa wakati wa ukaguzi.



𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗞𝗜𝗙𝗨𝗡𝗚𝗜𝗔 𝗞𝗜𝗪𝗔𝗡𝗗𝗔 𝗖𝗛𝗔 𝗠𝗔𝗥𝗔 𝗡𝗜𝗟𝗘-𝗣𝗪𝗔𝗡𝗜

Baraza la Taifa la Hifadhi la na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekifunga Kiwanda cha Mara Nile Ltd kilichopo Misugusugu Kibaha Mkoani Pwani kinachojihusisha na uzalishaji wa kemikali ya Extra Neutral Alcohol (Ethanol) na Carbon dioxide kwa kosa la kutiririsha majitaka yasiyotibiwa  kwenye mazingira

Hatua hiyo imekuja mara baada ya NEMC kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu utiririshaji wa majitaka kwenye Mazingira hali iliyozua taharuki kwa afya za wananchi wanaozunguka eneo hilo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Bi. Luhuvilo Mwamila amesema awali NEMC ilifanya ukaguzi na kubaini mtambo wa kutibu majitaka usiotumika  badala yake, kiwanda kimekuwa kikitiririsha maji taka yasiyotibiwa moja kwa moja kwenye mazingira na kumwaga tope lenye kemikali hatarishi (sludge).  

Uchunguzi zaidi umeonyesha kuwa kiwanda kimekuwa kikinyonya majitaka na kuyamwaga kwenye machimbo ya mchanga nje ya eneo lao, huku tope sumu wakilichoma katika maeneo hayo hayo.  

Hali hii ni kinyume cha taratibu za mazingira na kuhatarisha afya ya jamii na usalama wa ikolojia. kutotii maelekezo ya mamlaka, hatua kali zimechukuliwa ili kulinda mazingira na afya ya wananchi.



DKT. FESTO DUGANGE AITIKISA KAGERA, AITAKA NEMC KUKAZA UZI USIMAMIZI WA SHERIA ZA MAZINGIRA KWENYE MIRADI

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Dkt. Festo Dugange, amelitaka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa M...