Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki katika hafla ya kufunga na kukabidhi mali za Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (Enhancing Climate Change Adaptation for Agro-Pastoral Communities in Kongwa District).
Mradi huo unaofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (Adaptation Fund) umekuwa ukitekelezwa katika Kata za Ugogoni na Mtanana, ukinufaisha jumla ya vijiji 12 chini ya usimamizi wa NEMC na utekelezaji wa Foundation for Energy, Climate and Environment (FECE) pamoja na Halmashauri ya wilaya ya Kongwa.
Mradi umewezesha afua mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama kwa matumizi ya binadamu, mifugo na kilimo, ujenzi wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji wa matone, josho, manywesheo ya mifugo pamoja na upandaji miti.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi amelipongeza shirika la FECE pamoja na uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa kwa ushirikiano mkubwa waliouonyesha katika kusimamia mradi huo. Amesema mradi huo unachangia katika kutekeleza Dira ya Taifa ya 2025-2050, agenda ya kukijanisha Tanzania pamoja na Sera na Sheria za usimamizi wa mazingira.
Akizindua kisima cha maji kilichojengwa na mradi huo katika kiiji cha Mautya A, Dkt. Semesi amewapongeza wananchi kuwa sehemu ya wanufaika wa mradi huo na kutoa wito kwao kulinda miundombinu ya kisima hicho na kukichukulia kama mali yao.
Aidha, kwa nyakati tofauti tofauti, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kongwa, Diwani wa Kata ya Ugogoni pamoja na viongozi wengine wameishukuru NEMC kwa usimamzi wa mradi huu pamoja na kuahidi kuulinda ili uweze kutoa huduma endelevu.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni