Shindano la Mazingira Challenge ni sehemu ya mkakati wa NEMC wa kuibua na kuhamasisha ubunifu unaochochea utunzaji wa mazingira, hususan miongoni mwa vijana na makundi mbalimbali ya jamii. Vilevile, kusainiwa kwa Hati za Makubaliano (MoU) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) pamoja na Mabalozi wa Mazingira kunalenga kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa elimu ya mazingira, kuendesha kampeni za uhamasishaji na kuongeza ushiriki wa wananchi katika juhudi za uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira nchini.
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kulinda mazingira na kuhimiza wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa sera, mipango na programu za uhifadhi wa mazingira ili kuhakikisha rasilimali za asili zinalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, alisema maadhimisho hayo yamekuwa fursa muhimu ya kutoa elimu kwa umma, kutambua mchango wa wadau mbalimbali na kuhamasisha ubunifu katika usimamizi wa mazingira. Alibainisha kuwa NEMC itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha utoaji wa elimu ya mazingira, kuhamasisha matumizi endelevu ya rasilimali za mazingira na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Maadhimisho hayo yalipambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali waliotumia sanaa kuhamasisha utunzaji wa mazingira, huku wananchi waliotembelea Kijiji cha Mazingira wakiendelea kupata elimu kuhusu masuala mbalimbali ya mazingira na huduma zinazotolewa na NEMC pamoja na wadau wake. Hafla hiyo imeonesha dhamira ya Serikali na NEMC ya kuendelea kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali katika kujenga jamii inayowajibika kwa mazingira na kuendeleza ajenda ya maendeleo endelevu nchini.






Hakuna maoni:
Chapisha Maoni