Nyumbani

NEMC YAWATAKA WAMILIKI WA MABASI KUIMARISHA USAFI WA MAZINGIRA BARABARANI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limewataka wamiliki wa vyombo vya usafiri pamoja na abiria kuboresha usafi katika mabasi na maeneo ya usafiri barabarani, kwa kuzuia tabia ya kutupa taka nje ya magari na kukojoa mabarabarani.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi alipokuwa akiongea na vyombo vya habari kuhusu umuhimu wa kuhifadhi na kusimamia Mazingira nchini. 

Amesema kumekuwepo na mitazamo iliyojengeka kwa abiria wa mabasi makubwa yanayoenda safari ndefu na fupi ya kutokuthamini mazingira na kuwa na tabia ya kutupa taka ovyo na kukojoa barabarani hali inayochafua mazingira, kuharibu hali ya hewa na kuhatarisha afya za jamii. 

Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi akizungumza na vyombo vya Habari wakati akitoa wito wa kuwataka wamiliki wa vyombo vya usafiri kuepuka uchafuzi wa mazingira.

“Mazingira safi ni haki ya kila Mtanzania, na ni jukumu letu sote kuhakikisha tunayahifadhi. Kutupa taka nje ya gari na kukojoa barabarani si tu ni tabia mbaya, bali pia ni ukiukwaji wa Sheria za mazingira. Tunawaomba wasafiri na wamiliki wa mabasi kushirikiana nasi kwa kuweka na kutumia vyombo vya kutupa taka ili tukome uchafuzi huu,” alisema Mkurugenzi Mkuu Dkt. Immaculate Sware Semesi

Aidha, NEMC imetahadharisha kuwa watakaobainika kutupa taka au kukojoa mabarabarani watachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo faini na adhabu nyingine zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria za mazingira.

“Ninawahimiza watanzania wote kuwa mabalozi wa usafi katika maeneo wanayopitia. Tukichukua hatua sasa, tunaweza kulinda afya zetu na mazingira kwa vizazi vya sasa na baadae”.

NEMC imeendelea kutoa simu ya bure 0800 110 115 kwa ajili ya kuripoti uchafuzi wa Mazingira unaosababishwa na abiria, shughuli za binadamu, viwanda bubu au raia ili kuimarisha usimamizi na kuleta mabadiliko chanya katika jamii

NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA KAMATI YA KIMATAIFA GENEVA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC limeshiriki Mkutano wa kamati ya kimataifa ya majadiliano ya kuanzisha mkataba wa kimataifa wa kukabiliana na uchafuzi unaotokana na Plastiki nchini nchini Uswisi mjini Geneva

Mkutano huo umehusisha jopo la wadau wa Mazingira kutoka nchini Tanzania likiongozwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) profesa Peter Msofe, Balozi wa Tanzania nchini Kenya, maafisa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, NEMC, TBS, na GCLA ambao walishiriki kikamilifu kwa siku zote kumi za majadiliano ya kuanzishwa Mkataba huo.

Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Bw. Hamadi Taimuru akiwasilisha mada katika Mkutano huo

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Profesa Peter Msoffe (wa kwanza kulia) na Bw. Hamadi Taimuru (wa pili kushoto) wakifuatilia Mkutano huo


Hata hivyo kutokana na mitazamo na misimamo ya nchi mbalimbali kulingana na maslahi ya nchi zao, majadiliano hayo hayakuweza kufikia muafaka na hivyo mwenyekiti wa Mkutano ndugu Luisaliaghirisha majadiliano mpaka pale atakapotangaza tarehe mpya ya kuendeleza majadiliano hayo na hatimaye kupata mkataba husika.

Majadiliano ya washiriki wa Mkutano huo ikiwa ni sehemu ya Mkutano huo

NEMC YAUNGANA NA TAASISI NYINGINE KUADHIMISHA SIKU MAALUMU YA MAZINGIRA MAONESHO YA SABASABA 2025

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC  Julai 6, 2025  limeungana na Taasisi mbalimbali kuadhimisha Siku ya maalumu ya Mazingira iliyotengwa kwa mara ya kwanza kwenye Maonesho ya Biashara ya Kimataifa (sabasaba) 2025.

Mgeni rasmi katika Maadhimisho hayo alikuwa ni Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Cyprian Luhemeja huku tukio hilo likibebwa na Kauli mbiu isemayo "Matumizi ya Nishati safi na utunzaji wa Mazingira Kwa ustawi wa Tanzania bora".


Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja akizungumza wakati wa hafla ya Siku maalumu ya Mazingira iliyotengwa katika maonesho ya Sabasaba 2025 iliyofanyika tarehe 6/7/2025

Akizungumza katika hotuba yake Mhe. Cyprian Luhemeja ameitaka siku hiyo ya tarehe 6 /7 itengwe rasmi kuwa siku maalumu ya Mazingira kila mwaka katika maonesho hayo kuanzia maonesho ya 50 ya biashara ya kimataifa (sabasaba).

Hafla ya Siku maalum ya Mazingira tarehe 6/7/2025 iliyotengwa katika msimu wa maonesho ya Sabasaba 2025

Sambamba na hilo amesisitiza watanzania wote kutunza Mazingira kwa kuwa Mazingira yaliumbwa kwanza Kisha mwanadamu akaumbwa baadae ili ayatunze, ayahifadhi na kuyalinda.

"Hii duniani ilianza kwa kutengenezewa Mazingira, mwanadamu ameumbwa wa mwisho baada ya Mazingira kutengenezewa na mwanadamu alipoumbwa alipewa kazi ya kuyatunza na kuyahifadhi Mazingira lakini mwanadamu anayaharibu kwa uchafuzi na ukataji wa miti.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi Cyprian Luhemeja (wa nne kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC Bi. Mwanasha Tumbo (wa pili kulia) Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mkuu wa  Tantrade, Dkt. Latifa M. Khamis (wa tatu kulia), timu ya wanawake na Samia na baadhi ya washiriki wa Siku maalumu ya Mazingira iliyotengwa katika msimu wa maonesho ya Sabasaba 2025

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Baraza Dkt. Immaculate Sware Semesi amewapongeza washindi wa Mazingira Challenge iliyofanyika siku kadhaa zilizopita ambayo ililenga kumpata balozi kinara wa  Utunzaji wa Mazingira na anayehamasisha utunzaji wa Mazingira kwa kupiga picha ya Mazingira safi yanayomzunguka na kuwasilisha NEMC Kwa ajili ya mashindano hayo.

Maadhimisho hayo yalipambwa na mabalozi wa Mazingira pamoja na watumbuizaji nguli akiwemo Mrisho Mpoto pamoja na Mr. Tree na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Menejimenti ya NEMC, TANTRADE, STAMICO, Wanawake na Samia, Shirika la PUMA pamoja na wananchi waliotembelea maonesho ya sabasaba.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja akimkabidhi zawadi na cheti cha heshima Mshindi wa kwanza wa mashindano ya ‘Mazingira Challenge’ Bw. Paulo Dotto Masele yaliyofanyika katika msimu wa sabasaba

Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja akimkabidhi zawadi na cheti cha heshima Mshindi wa pili wa mashindano ya ‘Mazingira Challenge’ Bi. Magdalena Chuma yaliyofanyika katika msimu wa sabasaba


Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja akimkabidhi zawadi na cheti cha heshima Mshindi wa tatu wa mashindano ya ‘Mazingira Challenge’ Bw. Stanley Urassa  yaliyofanyika katika msimu wa sabasaba

"Hii duniani ilianza kwa kutengenezewa Mazingira, mwanadamu ameumbwa wa mwisho baada ya Mazingira kutengenezewa na mwanadamu alipoumbwa alipewa kazi ya kuyatunza na kuyahifadhi Mazingira lakini mwanadamu anayaharibu kwa uchafuzi na ukataji wa miti.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Baraza Dkt. Immaculate Sware Semesi amewapongeza washindi wa Mazingira Challenge iliyofanyika siku kadhaa zilizopita ambayo ililenga kumpata balozi kinara wa  Utunzaji wa Mazingira na anayehamasisha utunzaji wa Mazingira kwa kupiga picha ya Mazingira safi yanayomzunguka na kuwasilisha NEMC Kwa ajili ya mashindano hayo.

Maadhimisho hayo yalipambwa na mabalozi wa Mazingira pamoja na watumbuizaji nguli akiwemo Mrisho Mpoto pamoja na Mr. Tree na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Menejimenti ya NEMC, TANTRADE, STAMICO, Wanawake na Samia, Shirika la PUMA pamoja na wananchi waliotembelea maonesho ya sabasaba.



Ugawaji wa Zawadi kwa Wadau wengine 


NEMC YAPIGA KAMBI SABASABA – YAWAKARIBISHA WANANCHI KUPATA ELIMU YA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) lilipiga kambi viwanja vya sabasaba maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ili kutoa elimu ya uhifadhi na usimamizi wa mazingira kwa wananchi waliotembelea banda hilo katika Jengo la Karume.

Akizungumza katika maonesho hayo, Mhandisi Mwandamizi wa NEMC, Bw. Haji Kiselu, alisema Baraza limejipanga kikamilifu kuhakikisha elimu ya mazingira iliyo jumuishi inamfikia kila mwananchi, ili kwa pamoja tuweze kuyasimamia kwa maendeleo endelevu nchini.

Kwa upande wake, Mhandisi wa NEMC, Bw. Peres Ntinginya, alipozungumza, alisisitiza kuwa utunzaji wa mazingira ni jukumu la kila mmoja hivyo yapasa kuwajibika na kutoa  wito kwa wananchi kutumia nishati safi ya kupikia kwa kuwa matumizi yake husaidia kulinda afya ya binadamu na viumbe hai, kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa, pamoja na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.

Naye Mkazi wa Rufiji, Bw. Ayubu Njanja, alisema elimu aliyoipata kutoka kwa Maafisa wa Baraza imempa mwongozo sahihi wa kuzingatia katika kuhakikisha 

Bw. Ayubu Njanja akipatiwa elimu ya mazingira kutoka kwa wataalam wakati wa msimu wa maonesho ya 49 ya Sabasaba. 




Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika  maonesho ya 49 ya Sabasaba 2025 




Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika  maonesho ya 49 ya Sabasaba 2025 


NEMC YATEKELEZA AGIZO LA RAIS, YAONGEZA HUDUMA VIWANJA VYA NZUGUNI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limetekeleza agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan la kuongeza muda wa kutoa huduma zake katika viwanja vya maonesho ya Nane Nane vilivyopo Nzuguni, Jijini Dodoma. 

Hatua hiyo inalenga kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi, hususan wakulima na wafugaji wanaoshiriki maonesho hayo, ili kuwajengea uelewa na kuwasaidia kutekeleza shughuli zao kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira.

Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika maoneshoya wakulima, Nanenane 2025 katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma katika siku za nyongeza ikiwa ni agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuongeza muda wa maonesho hayo

NEMC inaendelea kutoa elimu inayohusu masuala ya matumizi endelevu ya ardhi, uhifadhi wa vyanzo vya maji, na namna ya kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi katika sekta ya kilimo na ufugaji.

Vilevile, wananchi wameelimishwa kuhusu taratibu za kupata vibali vya mazingira na umuhimu wa kufanya Tathmini ya athari kwa mazingira kabla ya kuanzisha miradi.

Baraza hilo linaendelea kuwakaribisha wananchi wote kutembelea banda lake ili kushirikiana kwa pamoja katika kusimamia na kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu ya Taifa. 

“Mazingira ni msingi wa maisha yetu. Tukiyaacha, na sisi tutapotea. Tushirikiane kuyatunza kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo,”



Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika maonesho ya wakulima, Nanenane 2025 katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma katika siku za nyongeza ikiwa ni agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuongeza muda wa maonesho hayo


NEMC YASHIRIKI HAFLA YA UFUNGAJI WA MAONESHO YA NANENANE, RAIS AONGEZA SIKU MBILI ZA KUTOA HUDUMA UWANJANI HAPO

Baraza la Taifa la Hifadhi na  Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikamilifu kwenye hafla ya ufungaji wa maonesho ya 32 ya wakulima (Nanenane) Kitaifa yaliyofanyika katika viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma leo

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan ambapo katika hotuba yake  amesisitiza umuhimu wa kilimo bora na endelevu kama mhimili wa maendeleo ya Taifa. 

Amesema sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi  ndio uti wa mgongo wa uchumi wa nchi, hivyo zinahitaji uwekezaji wa kutosha, ubunifu na usimamizi madhubuti ili kuijenga kesho bora kwa Watanzania wote.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati akiwasili katika Viwanja vya Nzuguni Jijini Dodoma kufunga Maonesho ya Wakulima (Nanenane 2025) katika viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Ameelekeza Wizara ya Kilimo kuimarisha upatikanaji wa pembejeo bora kwa wakulima, pamoja na kuunganisha nguvu katika kukuza sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan  ametangaza kuongeza siku mbili zaidi za maonesho hadi tarehe 10 Agosti ili kutoa nafasi kwa wananchi na wadau kuendelea kupata huduma na elimu mbalimbali.

" Maonesho haya ni siku nane, lakini kiuhalisia siku nane hazitimii kwani maandalizi yanachelewa, hivyo kuanzia mwaka ujao maandalizi ya maonesho yaanze tarehe 25/07." Ameelekeza Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan

Hafla hiyo ya ufungaji imehudhuriwa pia na viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Makatibu Wakuu, Manaibu Katibu, Wakuu wa Mikoa ya Dodoma na Singida, Wakuu wa Taasisi za Serikali na Binafsi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa hafla ya ufungaji wa Maonesho ya Wakulima (Nanenane 2025) katika viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Kwa upande wake, NEMC ilitumia maonesho haya kutoa elimu juu ya uhifadhi wa mazingira katika shughuli za kilimo na ufugaji, ikiwa ni pamoja na matumizi salama ya  mbolea, upandaji miti, na ulinzi wa vyanzo vya maji. 

Maonesho ya Nanenane mwaka huu yameendelea kuwa jukwaa muhimu kwa serikali, Taasisi na wananchi kushirikiana katika kuendeleza kilimo chenye tija na rafiki kwa mazingira.


Baadhi ya watumishi wa NEMC na Ofisi ya Makamu wa Rais wakiwakatika hafla ya ufungaji wa maonesho ya wakulima (Nanenane 2025) katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma


NEMC YAWAFIKIA WADAU TAKRIBANI 1,450 ELIMU YA MAZINGIRA MAONESHO YA NANENANE

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limewafikia wadau takriban 1,450  kwa utoaji wa  elimu ya uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira katika Maonesho ya Kilimo ya Nane Nane jijini Dodoma na Viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya mwaka huu.

Elimu hiyo imetolewa kwa wadau kutoka sekta mbalimbali ikiwa ni sehemu ya juhudi za Baraza hilo kuhamasisha uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Katika banda lake la maonesho, NEMC ilielimisha kuhusu mbinu bora za kilimo hifadhi kinachozingatia mazingira, ufugaji endelevu, uvuvi salama pamoja na kulinda vyanzo vya maji. 

Aidha, wananchi na wadau waliotembelea hapo walielimishwa kuhusu umuhimu wa kufanya tathmini ya athari kwa mazingira kabla ya kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo hususani ya kilimo  ili kupunguza athari hasi kwa mazingira.

Miongoni mwa masuala yaliyopatiwa kipaumbele ni pamoja na kuwahimiza wawekezaji kusajili miradi NEMC ili kupata vyeti vya mazingira kama kigezo muhimu cha kuendesha shughuli zao kisheria na kwa kuzingatia mazingira.


Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika maonesho ya wakulima, Nanenane 2025 katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.

Katika maonesho hayo, wataalamu wa NEMC pia walieleza athari za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja za shughuli za binadamu kama uchomaji moto hovyo, ukataji miti na utupaji taka kwenye mifumo ya ikolojia, hali inayochangia mabadiliko ya tabianchi, mmomonyoko wa ardhi na upungufu wa rasilimali maji.

“Tunawahimiza wawekezaji kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira. Elimu tunayoitoa ni msingi wa kufanya maamuzi sahihi ya kisera, kiuchumi na kijamii yanayozingatia mustakabali wa mazingira yetu,” alisema Bi. Dalia Kilamlya, Afisa Mazingira NEMC

Kwa ujumla, mwitikio wa wadau mbalimbali katika kupata elimu ya mazingira kutoka NEMC umetajwa kuwa mkubwa na wenye kuleta matumaini ya mabadiliko chanya katika namna jamii inavyoshiriki kwenye kulinda na kuhifadhi mazingira.


Elimu ya Mazingira ikitolewa kwa wageni waliotembelea banda la NEMC katika Maonesho ya Wakulima, Nanenane 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya John Mwakangale Jijini Mbeya.


NEMC YASHIRIKI MKUTANO WA SABA WA UMOJA WA MATAIFA KUHUSU MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashiriki Mkutano wa Saba (07) wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (07th Unit...