Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yusuf Masauni amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa ujenzi wa Jengo la kituo cha kutoa elimu kuhusu athari za afya na mazingira zitokanazo na matumizi yasiyo salama ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji wa madini wa dhahabu kwa wachimbaji wadogo na masuala ya Mazingira kwa ujumla mkoani Geita.
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP) Dkt. Befrina Igulu ameeleza Miundombinu rafiki kwa Mazingira iliyowekwa katika Jengo hilo ikiwa ni pamoja na Maabara na Maktaba za kisasa za elimu ya Zebaki mfumo wa nishati ya mwanga asili wa jua, mfumo wa uvunaji wa maji, Ukumbi wa Bodi na Ukumbi mkubwa wa Mikutano.
NEMC imejenga Jengo hilo ikiwa ni manufaa ya Mradi uliolenga kupunguza au kuondosha kabisa matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa Madini unafadhiliwa na Global Environment Facility (GEF) na kusimamiwa na Benki ya Dunia ambapo kwa Tanzania unatekelezwa katika Mikoa ya Geita, Mwanza, Mara, Shinyanga, Singida, Mbeya na Songwe.