Nyumbani

NEMC YASHIRIKI HAFLA YA KUKABIDHI MALI ZA MRADI WA KUHIMILI MABADILIKO YA TABIANCHI - KONGWA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki katika hafla ya kufunga na kukabidhi mali za Mradi wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (Enhancing Climate Change Adaptation for Agro-Pastoral Communities in Kongwa District).

Mradi huo unaofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi (Adaptation Fund) umekuwa ukitekelezwa katika Kata za Ugogoni na Mtanana, ukinufaisha jumla ya vijiji 12 chini ya usimamizi wa NEMC na utekelezaji wa Foundation for Energy, Climate and Environment (FECE) pamoja na Halmashauri ya wilaya ya Kongwa.

Mradi umewezesha afua mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama kwa matumizi ya binadamu, mifugo na kilimo, ujenzi wa miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji wa matone, josho, manywesheo ya mifugo pamoja na upandaji miti.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi amelipongeza shirika la FECE pamoja na uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa kwa ushirikiano mkubwa waliouonyesha katika kusimamia mradi huo. Amesema mradi huo unachangia katika kutekeleza Dira ya Taifa ya 2025-2050, agenda ya kukijanisha Tanzania pamoja na Sera na Sheria za usimamizi wa mazingira.

Akizindua kisima cha maji kilichojengwa na mradi huo katika kiiji cha Mautya A, Dkt. Semesi amewapongeza wananchi kuwa sehemu ya wanufaika wa mradi huo na kutoa wito kwao kulinda miundombinu ya kisima hicho na kukichukulia kama mali yao.

Aidha, kwa nyakati tofauti tofauti, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kongwa, Diwani wa Kata ya Ugogoni pamoja na viongozi wengine wameishukuru NEMC kwa usimamzi wa mradi huu pamoja na kuahidi kuulinda ili uweze kutoa huduma endelevu.

NEMC YATUNUKU TUZO WASHINDI WA MAZINGIRA CHALLENGE, YAINGIA MAKUBALIANO NA MABALOZI WA MAZINGIRA SABASABA


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), tarehe 11 Julai, 2026, limeadhimisha Siku ya Mazingira katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yaliyofanyika katika Viwanja vya Sabasaba, jijini Dar es Salaam, ambapo liliwatunuku vyeti na tuzo washindi wa Mazingira Challenge, kusaini Hati za Makubaliano (MoU) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) pamoja na Mabalozi wa Mazingira. Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa mazingira, washirika wa maendeleo, sekta binafsi, wasanii na wananchi.

Shindano la Mazingira Challenge ni sehemu ya mkakati wa NEMC wa kuibua na kuhamasisha ubunifu unaochochea utunzaji wa mazingira, hususan miongoni mwa vijana na makundi mbalimbali ya jamii. Vilevile, kusainiwa kwa Hati za Makubaliano (MoU) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) pamoja na Mabalozi wa Mazingira kunalenga kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa elimu ya mazingira, kuendesha kampeni za uhamasishaji na kuongeza ushiriki wa wananchi katika juhudi za uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira nchini.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kulinda mazingira na kuhimiza wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa sera, mipango na programu za uhifadhi wa mazingira ili kuhakikisha rasilimali za asili zinalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, alisema maadhimisho hayo yamekuwa fursa muhimu ya kutoa elimu kwa umma, kutambua mchango wa wadau mbalimbali na kuhamasisha ubunifu katika usimamizi wa mazingira. Alibainisha kuwa NEMC itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha utoaji wa elimu ya mazingira, kuhamasisha matumizi endelevu ya rasilimali za mazingira na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Maadhimisho hayo yalipambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali waliotumia sanaa kuhamasisha utunzaji wa mazingira, huku wananchi waliotembelea Kijiji cha Mazingira wakiendelea kupata elimu kuhusu masuala mbalimbali ya mazingira na huduma zinazotolewa na NEMC pamoja na wadau wake. Hafla hiyo imeonesha dhamira ya Serikali na NEMC ya kuendelea kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali katika kujenga jamii inayowajibika kwa mazingira na kuendeleza ajenda ya maendeleo endelevu nchini.




DKT. MUYUNGI AIPONGEZA NEMC KUHUSISHA VIJANA WENYE UBUNIFU - KIJIJI CHA MAZINGIRA


Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi amevutiwa na Kijiji cha Mazingira katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Dkt. Muyungi amesema kilichomvutia zaidi ni kuona namna ambavyo vijana wabunifu wamepewa nafasi ya kuonesha ujuzi wao katika kutumia fursa zinazopatikana kwenye Mazingira kupitia kampeni ya Taka ni Fursa.

Dkt. Muyungi amesema kuna haja ya kuwawezesha vijana wenye mitaji midogo ili waweze kufanya mambo makubwa kupitia ubunifu wao kwenye kutumia fursa mbalimbali za urejelezaji na uchakataji taka ili kujipatia kipato na kusafisha Mazingira.

Dkt. Muyungi aliambatana na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi alipotembelea Kijiji cha Mazingira mara baada ya kushiriki hafla ya ufunguzi waaonesho hayo Julai 3,2026.

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗞𝗜𝗙𝗨𝗡𝗚𝗜𝗔 𝗞𝗜𝗪𝗔𝗡𝗗𝗔 𝗖𝗛𝗔 𝗦𝗔𝗡 𝗦𝗛𝗔𝗡 𝗡𝗔 𝗕𝗔𝗜-𝗟𝗬 𝗣𝗔𝗣𝗘𝗥 𝗖𝗢. 𝗟𝗧𝗗 𝗠𝗞𝗨𝗥𝗔𝗡𝗚𝗔 𝗞𝗪𝗔 𝗨𝗞𝗜𝗨𝗞𝗪𝗔𝗝𝗜 𝗪𝗔 𝗦𝗛𝗘𝗥𝗜𝗔 𝗬𝗔 𝗠𝗔𝗭𝗜𝗡𝗚𝗜𝗥𝗔

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekifungia kiwanda cha SAN SHAN na BAI-LY PAPER CO. LTD kwa kukiuka sheria na taratibu za mazingira, hatua iliyochukuliwa baada ya timu ya ukaguzi wa mazingira uliofanyika katika Wilaya ya Mkuranga ukiongozwa na Meneja wa Utekelezaji wa Sheria wa NEMC, Mhandisi Luhuvilo Mwamila.

Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mhandisi Luhuvilo alisema kiwanda cha SAN SHAN kinachojihusisha na uchakataji wa mafuta machafu (waste oil) kimekuwa kikizalisha moshi mzito na harufu kali kutokana na kukosa mfumo wa kudhibiti hewa chafuzi. Aidha, kiwanda hicho kimekuwa kikitiririsha maji taka yenye mafuta machafu kwenye mazingira na kusababisha uchafuzi mkubwa katika maeneo ya jirani.

NEMC imebainisha kuwa kiwanda hicho hakina Cheti cha Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (TAM) na kwamba mwekezaji wake amekuwa akiwazuia wakaguzi kutekeleza majukumu yao ya ukaguzi, hali iliyokwamisha juhudi za kitaalamu za kushauri maboresho ya uzalishaji unaozingatia uhifadhi wa mazingira. NEMC pia ilieleza kuwa viongozi wa Halmashauri walishindwa kukikagua kiwanda hicho kutokana na vikwazo vilivyowekwa na uongozi wa kiwanda.

Kwa upande wa kiwanda cha BAI-LY PAPER CO. LTD, kinachozalisha karatasi za chooni (Toilet paper), kimekutwa kikitiririsha maji taka kwenye mazingira na kusababisha uchafuzi unaohatarisha afya za wakazi wa maeneo ya jirani.

Kutokana na changamoto hizo, NEMC ilishirikiana na Jeshi la Polisi kufanikisha ukaguzi wa viwanda hivyo na hatimaye kuvifungia. Bi. Luhuvilo ametoa rai kwa viwanda vyote nchini kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira, kuweka mifumo madhubuti ya kudhibiti uchafuzi wa mazingira na kushirikiana na wakaguzi ili kulinda afya za wananchi na mazingira kwa ujumla.







NEMC YASHIRIKI KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI-DODOMA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki kikamilifu kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika tarehe 5 Juni 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete (JKCC) Jijini Dodoma.

Maadhimisho hayo, yanayofanyika kila mwaka tarehe 5 Juni, kwa mwaka huu yaliadhimishwa kitaifa kwa kauli mbiu isemayo “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania”.


Mgeni rasmi wa hafla hiyo alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel Nchimbi ambapo kabla ya kilele cha Maadhimisho hayo kikitanguliwa na maonesho ya wiki nzima yaliyolenga kutoa elimu kwa wadau mbalimbali kuhusu uhifadhi na usimamizi wa mazingira kupitia banda lake maalum.

Katika hafla hiyo pia ulizinduliwa Mkakati wa Kitaifa wa Kukijanisha Tanzania ikiwa ni hatua kufikia Taifa linalostawi kiuchumi bila kuharibu Mazingira.

















NEMC YAMTAMBUA JACKLINE ELIABI KWA WASILISHO BORA LA UCHUMI MZUNGUKO KATIKA KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limemtambua mwanafunzi wa Darasa la Sita, Jackline Eliabi wa Shule ya Msingi Manyinga, Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro, kwa uwasilishaji wake bora wa dhana ya Uchumi Mzunguko katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.

Jackline alipata pongezi na kutunukiwa zawadi baada ya kuwasilisha kwa umahiri dhana hiyo muhimu inayohamasisha matumizi endelevu ya rasilimali, upunguzaji wa taka na uhifadhi wa mazingira. Uwasilishaji wake ulionesha uelewa mkubwa wa masuala ya mazingira na mchango wa wanafunzi katika kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kutunza mazingira kwa maendeleo endelevu.

Zawadi hiyo ilitolewa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Immaculate Sware Semesi, ikiwa ni kutambua mchango wa wanafunzi katika kusukuma gurudumu la uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini. Dkt. Semesi alieleza kuwa wanafunzi ni wadau muhimu katika juhudi za kulinda mazingira na kwamba wao ndio mabalozi wa baadaye wa mazingira watakaosaidia kuendeleza agenda ya maendeleo endelevu kwa manufaa ya taifa na vizazi vijavyo.





DKT. NCHIMBI AZURU BANDA LA NEMC MAADHIMISHO YA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Emmanuel Nchimbi ametembelea Banda la NEMC Leo ikiwa ni  siku ya kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayoadhimishwa kila tarehe 5, Mei ya Kila mwaka ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) katika kuhifadhi na kusimamia mazingira nchini.


Maadhimisho ya mwaka huu yamefanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania,” ikihamasisha ushiriki wa wadau wote katika kutunza mazingira, kupambana na uharibifu wa mazingira na kuendeleza matumizi endelevu ya rasilimali asilia kwa maendeleo ya Taifa na ustawi wa vizazi vijavyo.





NEMC YAONGEZA VYOMBO VYA USAFIRI KUIMARISHA MIUNDOMBINU WEZESHI YA UTEKELEZAJI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeongeza vyombo vya usafiri kwa kutumia mapato yake ya ndani, ikiwa ni sehemu ...