Nyumbani

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la WaterAid-Tanzania, limefanya ziara ya mafunzo nchini Rwanda. Mafunzo haya yameandaliwa na kutekelezwa na WaterAid-Rwanda, na yamefanyika katika Ofisi za shirika hilo.


Lengo kuu la mafunzo haya ni kujifunza namna WaterAid-Rwanda inavyotekeleza miradi ya maji, hususan katika eneo la Bugesera, ikiwa ni pamoja na mbinu za kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na usimamizi wa huduma za usafi wa mazingira.

Ziara hii ya mafunzo imehudhuriwa na viongozi na wataalamu mbalimbali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mkurugenzi Msaidizi wa Usambazaji wa Maji na Usafi wa Mazingira, Afisa Tawala wa Mkoa wa Manyara, pamoja na maafisa wengine kutoka serikalini na WaterAid

NEMC, CSE WAANDAA WARSHA YA KIKANDA KUCHOCHEA FURSA MPYA KATIKA USIMAMIZI WA TAKA ZA MATAIRI CHAKAVU

 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Kituo cha Sayansi na Mazingira - India (CSE) wameandaa warsha ya kikanda inayolenga kujadili changamoto na fursa zitokanazo na ongezeko la taka za matairi chakavu.

 Warsha hiyo imewakutanisha washiriki kutoka mamlaka za usimamizi wa mazingira na wadau mbalimbali kutoka nchi za Kenya, Uganda, Afrika Kusini, Ghana na Nigeria. Mkutano huu umefanyika katika Hoteli ya Four Points by Sheraton na New Africa Hotel jijini Dar es Salaam tarehe 23 na 24 Machi 2026.

Katika warsha hiyo, mada mbalimbali zimejadiliwa ikiwemo miundo ya kisheria na kikanuni, teknolojia za kuongeza thamani ya taka za matairi, pamoja na matumizi ya masoko katika kukuza dhana ya uchumi rejeleshi. Lengo kuu ni kubadilishana uzoefu na kubuni mbinu mbadala zitakazosaidia kupunguza athari za kimazingira huku zikichangia maendeleo endelevu ya kiuchumi katika ukanda wa Afrika.





NEMC KUAINISHA FURSA ZILIZOPO KATIKA TAKA, MACHI 30

Ni katika Viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam, Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya kuondoa Taka 

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limejipanga kutoa elimu kuhusu fursa zilizopo kwenye taka katika Maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Kuondoa Taka yanayotarajiwa kuadhimishwa Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yatatanguliwa na maonesho yatakayoanza tarehe 28 hadi siku ya kilele, Machi 30, 2026 yatakayobainisha namna ambavyo taka ni fursa kupitia ubunifu wa bidhaa zitokanazo na taka

Akizungumza na vyombo vya Habari, Meneja Uzingatiaji wa Sheria (NEMC) Bw. Hamadi Taimuru amesema siku hii inalenga kuhamasisha umma  kupunguza uzalishaji wa taka na kutoa elimu kwa wadau na wananchi wote kutambua fursa za uwekezaji katika taka kupitia ukusanyaji, uchakataji na Urejelezaji wa taka.

"Tunawaomba wananchi na wadau wote tufike katika viwanja vya Mnazi mmoja kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi na moja jioni kujifunza na kujionea fursa za uwekezaji katika eneo la taka". Amesema Bw. Taimuru

Aidha ameongeza kuwa Maadhimisho hayo yamelenga kuhimiza na kuhakikisha kuwa dhana ya 𝗣𝘂𝗻𝗴𝘂𝘇𝗮, 𝗧𝘂𝗺𝗶𝗮 𝘁𝗲𝗻𝗮 𝗻𝗮 𝗥𝗲𝗷𝗲𝗹𝗲𝘇𝗮 inatekelezwa kwa vitendo na kwa matakwa ya Sheria ili kuwa na Mazingira safi, afya bora ya jamii na matumizi ya rasilimali endelevu Kwa ajili ya Maendeleo ya Taifa.

Kauli mbiu ya kimataifa ya Maadhimisho haya ni "𝒌𝒖𝒘𝒆𝒛𝒆𝒔𝒉𝒂 𝒕𝒂𝒌𝒂 𝒔𝒊𝒇𝒖𝒓𝒊 𝒌𝒘𝒆𝒏𝒚𝒆 𝑺𝒆𝒌𝒕𝒂 𝒚𝒂 𝒄𝒉𝒂𝒌𝒖𝒍𝒂" ambayo inaangazia tatizo la upotevu wa chakula Duniani na Athari zake kwa Mazingira na Jamii ambapo inakadiriwa kuwa upotevu wa chakula huchangia takribani asilimia kumi (10%) ya hewa chafuzi (greenhouse gases)

Ameongeza kuwa, kitaifa inaendelea Kaulimbiu ya '𝑻𝒂𝒌𝒂 𝒏𝒊 𝑭𝒖𝒓𝒔𝒂' ambayo inaweka msisitizo kuwa taka si taka tu bali ni malighafi za kutengeneza bidhaa nyingine.

DKT. FESTO DUGANGE AITIKISA KAGERA, AITAKA NEMC KUKAZA UZI USIMAMIZI WA SHERIA ZA MAZINGIRA KWENYE MIRADI

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Dkt. Festo Dugange, amelitaka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuhakikisha linasimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira katika miradi yote ya maendeleo inayotekelezwa mkoani Kagera, ili kulinda rasilimali za mazingira na afya za wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya mazingira katika Halmashauri za Wilaya ya Karagwe na Misenyi, Dkt. Dugange alisisitiza kuwa NEMC inapaswa kuimarisha ukaguzi na ufuatiliaji wa miradi, kuhakikisha tathmini za athari kwa mazingira (EIA) zinafanyika kwa mujibu wa sheria na kwamba masharti yote ya kimazingira yanazingatiwa kabla na wakati wa utekelezaji.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri alikagua mradi wa vijana wa kuchakata taka za plastiki unaosaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira na kutoa ajira kwa vijana. Pia alitembelea mradi wa biashara ya kaboni kupitia kilimo mseto (Kinoni Agroforestry Farm) unaotekelezwa na kampuni ya KADERES, unaolenga kuwawezesha wakulima kunufaika na biashara ya hewa ukaa sambamba na kuhifadhi mazingira.

Aidha, alikagua Kiwanda cha Vifungashio (Magunia) cha KADERES, Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia unaohamasisha matumizi ya nishati mbadala ili kupunguza ukataji miti, pamoja na mradi wa ujenzi wa dampo la kuhifadhia maji taka wilayani Karagwe unaolenga kuboresha usafi wa mazingira na kulinda afya ya jamii.

Akizungumza na wananchi wa Karagwe na Misenyi, Dkt. Dugange alihamasisha jamii kuona mazingira kama fursa ya kiuchumi. Alieleza kuwa taka zinaweza kuwa rasilimali yenye thamani endapo zitasimamiwa na kuchakatwa kwa usahihi.

“Taka si taka tu bali ni rasilimali muhimu inayoweza kuleta manufaa ya kiuchumi. Taka zinazooza zinaweza kutumika kutengeneza gesi na mbolea ya asili kwa ajili ya bustani za kioganiki na kulinda rutuba ya udongo,” amesema.

Kwa upande wake, Meneja NEMC Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi Bw. Boniphace Guni, amesema NEMC itaendelea kuimarisha usimamizi wa miradi yote inayotekelezwa katika kanda hiyo na kuhakikisha sheria za mazingira zinatekelezwa kikamilifu nchini kote.

Ziara hiyo pia ilihusisha ushiriki wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe na Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha maendeleo endelevu yanakwenda sambamba na uhifadhi wa mazingira.

NEMC KANDA YA MOROGORO/RUFIJI NA MORUWASA WAPANDA MITI 5,000

NEMC Kanda ya Morogoro/Rufiji imeshirika zoezi la kupanda miti 5,000 aina ya Mkongo ( Afzelia quanzensis) katika eneo la bwawa la Mindu, Kata ya Kauzeni Manispaa ya Morogoro. Zoezi lililoandaliwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) kama sehemu ya maadhimisho ya wiki ya Maji.



NEMC YASHIRIKI ZIARA YA KATIBU MKUU DKT. RICHARD MUYUNGI-KAGERA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) – Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi, limeshiriki ziara ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, iliyofanyika mkoani Kagera tarehe 16.03.2026, kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu matumizi ya nishati safi na uhifadhi wa mazingira.

Katika ziara hiyo, Dkt. Muyungi alitembelea Shule ya Sekondari Rugambwa iliyopo Manispaa ya Bukoba pamoja na Shule ya Msingi Hosiana iliyopo Wilaya ya Karagwe. Lengo la ziara hizo lilikuwa kujionea namna taasisi za elimu zinavyotekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhusu kuhamia matumizi ya nishati safi ili kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa unaochangia mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, Katibu Mkuu alitembelea mradi wa Kaderes Enterprise uliopo Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera, ambapo alipata fursa ya kujionea juhudi za wadau katika utekelezaji wa miradi ya kaboni (carbon credit) inayolenga kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi na kuchangia katika uhifadhi wa mazingira.

Katika ziara hiyo, Dkt. Muyungi alisisitiza masuala mbalimbali kama vipaumbele vya kitaifa:

- Matumizi ya Nishati Safi: Kuimarisha matumizi ya nishati mbadala kama vile majiko banifu, gesi asilia, nishati ya jua na umeme safi ili kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, kulinda misitu, na kuboresha afya ya jamii.

- Udhibiti wa Hewa Ukaa: Kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi (GHGs) kupitia teknolojia rafiki kwa mazingira, ufanisi wa matumizi ya nishati, na utekelezaji wa miradi ya upandaji miti na uhifadhi wa misitu.

- Biashara ya Kaboni: Kukuza uelewa na ushiriki wa wadau katika miradi ya Kaboni kama fursa ya kiuchumi, ambapo jamii na taasisi zinaweza kunufaika kifedha kupitia uhifadhi wa mazingira na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.

- Ushirikishwaji wa Taasisi zenye zaidi ya watu 100: Kuhamasisha taasisi za serikali na zisizokuwa za serikali zenye watu zaidi ya 100 kuwa vinara wa matumizi ya nishati safi na elimu ya mazingira kwa vitendo.

-Pamoja na  Uzingatiaji wa Sera na Sheria: Kusisitiza uzingatiaji wa miongozo na Sheria za Mazingira.

NEMC NA WATER AIDS WAADHIMISHA SIKU YA MAJI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na shirika lisilo la kiserikali la WaterAid, katika kuadhimisha mwezi wa maji mwezi Machi na Siku ya urejelezaji Duniani (Global Recycling Day, tarehe 18 Machi), kuelekea kilele cha Siku ya Kimataifa ya Taka Sifuri (International Day of Zero Waste), limefanya tathmini ya hali ya udhibiti wa taka ngumu kwa lengo la kulinda chanzo cha maji cha Ziwa Bassotu kilichopo Kijiji cha Bassotu, Wilaya ya Hanang, Mkoa wa Manyara.

Tathmini hiyo imelenga kubaini changamoto zilizopo na kuweka mikakati bora ya udhibiti wa taka ndani ya kijiji hicho na maeneo jirani, ili kunusuru ziwa hilo ambalo kwa sasa linakabiliwa na hatari ya kugeuzwa dampo lisilo rasmi. Hali hii inachangiwa na utupaji holela wa taka ngumu, ikiwemo chupa za viuatilifu vinavyotokana na shughuli za kilimo, jambo linalohatarisha ubora wa maji, uhai wa viumbe hai ziwani na afya ya binaadamu na mazingira kwa ujumla.

Malengo hayo yanaweza kufikiwa endapo tutaimarisha utekelezaji wa dhana ya uchumi mzunguko (circular economy) kuelekea taka sifuri kupitia urejelezaji. Hatua hii itasaidia kulinda chanzo hicho cha maji na kuboresha hali ya mazingira ya Kijiji cha Bassotu kwa ujumla.

MATUKIO KATIKA PICHA, UKAGUZI WA MGODI WA DHAHABU WA GEITA GOLD MINES (GGM) KATIKA ZIARA YA MHESHIMIWA WAZIRI, MHANDISI HAMAD YUSUF MASAUNI MKOANI GEITA

Pichani ni ziara ya Mheshimiwa Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Yusuf Masauni (wa kwanza kushoto) akikagua hali ya Mazingira katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mines Mkoani Geita ambapo aliambatana na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi na baadhi ya watumishi wa NEMC, pamoja na Viongozi wengine kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Machi 14, 2026










MATUKIO KATIKA PICHA, WAZIRI MASAUNI (OFISI YA MAKAMU WA RAIS-MUUNGANO NA MAZINGIRA APANDA MTI KATIKA KITUO CHA ELIMU YA ZEBAKI CHA NEMC-GEITA

Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni akipanda mti katika eneo litakapokuwa lango kuu la Jengo la Kituo cha kutoa elimu kuhusu Athari za matumizi ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji Madini ya Dhahabu katika afya na Mazingira linalosimamiwa na NEMC chini ya ufadhili wa Global Environmental Facility (GEF) lililojengwa mkabala na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita ikiwa ni jitaha za kuunga mkono  azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania za kukijanisha Tanzanaia.

Mhe. Waziri amepanda mti huo wakati wa ziara yake alipotembelea Jengo hilo.

Kadhalika katika kuunga mkono jitihada hizo Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi pia alipanda mti katika eneo hilo







WAZIRI MASAUNI AIPONGEZA NEMC UJENZI WA KITUO CHA KUTOA ELIMU YA ZEBAKI - GEITA

 Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Hamad Yusuf Masauni amelipongeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwa ujenzi wa Jengo la kituo cha kutoa elimu kuhusu athari za afya na mazingira zitokanazo na matumizi yasiyo salama ya Zebaki (Mercury) katika uchenjuaji  wa madini wa dhahabu  kwa wachimbaji wadogo na masuala ya Mazingira kwa ujumla mkoani Geita.

Mhe. Masauni ametoa pongezi hizo Machi 14, 2026 alipozuru eneo la ujenzi wa Jengo hilo ambalo limefikia asilimia 80 ya ujenzi linalojengwa mkabala na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Akizungumza mara baada ya Ukaguzi wa Jengo hilo, Waziri Masauni ameeleza namna alivyofurahishwa na Uzingatiaji wa maswala ya kimazingira katika ujenzi wa Jengo hilo na kwamba litatumika kama Kituo cha kutoa taaluma mbalimbali kwa wananchi kuhusiana na maswala ya Mazingira

"Jengo hili litasaidia masuala mbalimbali ya Mazingira, litakuwa kituo cha kutoa taaluma mbalimbali kwa wananchi kuhusiana na maswala ya Mazingira hususan changamoto kubwa ya matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa madini ambapo imekuwa ikiathiri mazingira na afya ya wananchi.

Akizungumza mara baada ya Ukaguzi wa Jengo hilo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Immaculate Sware Semesi amesema Jengo hilo ni mfano wa ramani itakayotumika kujenga majengo mengine kumi na mbili (12) ya Kanda za NEMC. Aidha amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Martn Shegella kwa kuipatia NEMC eneo kwa ajili ya ujenzi wa Jengo hilo.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kudhibiti Matumizi ya Zebaki kwa Wachimbaji Wadogo wa Dhahabu (EHPMP) Dkt. Befrina Igulu ameeleza  Miundombinu rafiki kwa Mazingira iliyowekwa katika Jengo hilo ikiwa ni pamoja na Maabara na Maktaba za kisasa za elimu ya Zebaki mfumo wa nishati ya mwanga asili wa jua, mfumo wa uvunaji wa maji, Ukumbi wa Bodi na Ukumbi mkubwa wa Mikutano.

NEMC imejenga Jengo hilo ikiwa ni manufaa ya Mradi uliolenga kupunguza au kuondosha kabisa matumizi ya Zebaki katika uchenjuaji wa Madini unafadhiliwa na Global Environment Facility (GEF) na kusimamiwa na Benki ya Dunia ambapo kwa Tanzania unatekelezwa katika Mikoa ya Geita, Mwanza, Mara, Shinyanga, Singida, Mbeya na Songwe.

NEMC KANDA YA ZIWA VICTORIA MASHARIKI YASHIRIKI ZIARA YA WAZIRI MASAUNI-MWANZA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeshiriki ziara ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) ya Ukaguzi wa Miradi ya uwekezaji Jijini Mwanza.

Ziara hiyo ililenga kukagua Miradi ya uwekezaji na namna inavyotekeleza Uhifadhi wa Mazingira Mkoani humo.

Akimpokea Mhe. Waziri katika Ofisi yake, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda amesema Ofisi yake inafanya juhudi kubwa kushirikiana na  NEMC kuhakikisha Mazingira yanalindwa na kutunzwa katika Mkoa huo licha ya changamoto zinazoikabili Ofisi yake hasa katika udhibiti wa Kelele chafuzi za Maeneo ya kumbi za starehe.

Akizungumza na vyombo vya habari mara baada ya Ukaguzi huo, Mhe. Waziri amewataka wawekezaji na watanzania wote kulinda Mazingira huku akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote wanaosababisha uharibifu wa Mazingira kwa namna yoyote.

"Tunawajibu wa kulinda Mazingira lli Mazingira yawe mazuri ni lazima sisi tuyalinde, na ili yawe mabaya ni lazima sisi tuyaharibu, Serikali inawajibu wa kuhakikisha watanzania wanaendelea kutunza Mazingira" amesema Mhe. Waziri Hamad Yusuf Masauni.



MRADI WA KIHANSI MKOMBOZI WA MAZINGIRA KWA WANANCHI WA MLIMBA

 Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuanzia Machi 9 hadi 16 linafanya ufuatiliaji katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), Taasisi ya Utafiti wa Kahawa Tanzania (TaCRI), Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na Halmashauri za Wilaya ya Mlimba, Kilolo na Mafinga kwa lengo la kutathmini mafanikio ya Mradi wa Kihansi ambao umechangia kwa kiasi kikubwa katika uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii.

Mradi huo ulitekelezwa kuanzia mwaka 2001 hadi 2019 kupitia awamu tatu ambazo ni Lower Kihansi Environmental Management Project (LKEMP I na II) pamoja na Kihansi Catchment Conservation Management Project (KCCMP). Miradi hiyo ililenga kuimarisha uhifadhi wa baioanuai katika bonde la Kihansi pamoja na kulinda vyanzo vya maji.

Kupitia miradi hiyo, wananchi walipewa elimu ya uhifadhi wa mazingira na kuwezeshwa kufanya shughuli za kilimo nje ya vyanzo vya maji ili kupunguza uharibifu wa mazingira. Miradi hiyo ilitekelezwa chini ya uratibu na usimamizi wa NEMC kwa kushirikiana na taasisi za utafiti na wadau wengine.

Aidha, wananchi wa Halmashauri hizo waliwezeshwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi kupitia vikundi, ikiwemo kilimo cha mpunga, kilimo cha miti, ufugaji wa nyuki na ufugaji wa samaki. Hatua hiyo imechangia kuongeza kipato na kuboresha ustawi wa kaya nyingi katika maeneo hayo.

Kutokana na uwezeshaji huo, baadhi ya wanufaika wamefanikiwa kujenga nyumba bora, kusomesha watoto, kuongeza ukubwa wa mashamba ya kilimo pamoja na kumiliki mifugo, jambo ambalo limeimarisha ustawi wa familia zao na jamii kwa ujumla.

Mmoja wa wanufaika wa mradi huo, Bw. Philiscacius Shaban Masongela, ameishukuru NEMC kwa mchango wake katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia miradi ya uhifadhi na uwezeshaji wa kiuchumi. “Kupitia mradi huu nimeweza kuongeza kipato, kujenga nyumba nzuri, kukuza shamba la mpunga na kumiliki mifugo. Hakika mradi huu umeleta mabadiliko chanya katika maisha yetu,” amesema Bw. Masongela.

Naye Bi. Pudensiana Valentine Chagawe kutoka Kikundi cha Nguvu Kazi katika Kijiji cha Chita, Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, amesema elimu ya shamba darasa aliyopatiwa kupitia mradi huo imemwezesha kutumia mbinu za kilimo cha kisasa na kuongeza uzalishaji wa mazao. “Awali nilikuwa napata takribani debe 30 (magunia matatu) za mpunga katika nusu heka, lakini baada ya kupata mafunzo ya shamba darasa na kutumia mbinu bora za kilimo, uzalishaji umeongezeka hadi kufikia debe 180 (magunia 18). Hii imenisaidia kuongeza kipato na kuboresha maisha ya familia yangu,” amesema Bi. Chagawe.

Timu ya NEMC imewapongeza wananchi wa maeneo hayo kwa kuendelea kutumia maarifa na ujuzi walioupata kupitia Mradi wa Kihansi katika kuboresha shughuli zao za kiuchumi, kuinua vipato vya familia zao hiki wakitunza mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

𝗡𝗘𝗠𝗖 𝗬𝗔𝗙𝗨𝗡𝗚𝗜𝗔 𝗨𝗝𝗘𝗡𝗭𝗜 𝗪𝗔 𝗠𝗔𝗝𝗘𝗡𝗚𝗢 𝗠𝗔𝗪𝗜𝗟𝗜 𝗠𝗜𝗞𝗢𝗖𝗛𝗘𝗡𝗜

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limefungia ujenzi wa majengo mawili yaliyokuwa yanaendelea kujengwa katika eneo la Mikocheni, mtaa wa Regent, mkoani Dar es Salaam, kufuatia ukiukwaji wa taratibu za usimamizi wa mazingira. Majengo yaliyosimamishwa ni pamoja na VIENNATANZANIA CO LTD na TAFBROS LIMITED

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya kubainika kuwa miradi hiyo ilikuwa inaendelea kuwa na vibali vya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA). NEMC imeagiza kusimamishwa mara moja kwa shughuli zote za ujenzi hadi taratibu zote za kisheria zitakapokamilika.

Hata hivyo NEMC imetoa angalizo kwa niradi yote inayoendelezwa bila kufata taratibu za Mazingira kusitisha na kufika ofisi za NEMC kwaajili ya kuanza mchakato wa Uzingatiaji wa Sheria kabla ya kukaguliwa na kupewa adhabu.





Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la WaterAid-Tanza...