Nyumbani

SERIKALI YASISITIZA UWAJIBIKAJI WA MAZINGIRA KWA VIWANDA NA WADAU WA TAKA HATARISHI

Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria za mazingira kwa sekta ya viwanda, kampuni za uteketezaji taka pamoja na wadau wanaohusika na uhifadhi wa bidhaa hatarishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kulinda afya za wananchi na kuhakikisha maendeleo endelevu ya taifa.


Hayo yamejadiliwa katika mkutano wa wadau wa mazingira ulioandaliwa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), uliowakutanisha wamiliki wa viwanda, wateketezaji wa taka na wenye maghala ya bidhaa hatarishi kwa lengo la kujadili namna bora ya kuimarisha usimamizi wa mazingira nchini.


Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mheshimiwa Reuben Nhamanilo Kwagilya, amesema ukuaji wa sekta ya viwanda unapaswa kwenda sambamba na utekelezaji wa sheria za mazingira ili kupunguza athari zinazoweza kuhatarisha afya za wananchi na mazingira.


Alieleza kuwa mazingira ni msingi muhimu wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, hivyo kila mdau wa uzalishaji na usimamizi wa taka ana wajibu wa kuhakikisha shughuli zake zinafanyika kwa kuzingatia viwango vya usalama wa mazingira na afya.


Katika kikao hicho, Serikali ilisisitiza umuhimu wa utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, ikiwemo udhibiti wa uchafuzi wa hewa, maji na ardhi unaotokana na shughuli za viwanda pamoja na usimamizi sahihi wa taka ngumu na taka hatarishi.


Aidha, wadau walikumbushwa umuhimu wa kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) kabla ya kuanza miradi ya maendeleo pamoja na kufanya ukaguzi wa mazingira mara kwa mara ili kuhakikisha shughuli za uzalishaji zinaendana na matakwa ya sheria.


Mkutano huo pia uliangazia changamoto zinazotokana na ongezeko la taka za viwandani na matumizi ya kemikali hatarishi, ambapo NEMC ilihimiza matumizi ya teknolojia safi na mifumo bora ya uteketezaji na urejelezaji taka ili kupunguza uchafuzi wa mazingira.


Katika kuimarisha usimamizi endelevu wa rasilimali, Serikali imeendelea kuhamasisha utekelezaji wa dhana ya Uchumi Mzunguko (Circular Economy) inayolenga kupunguza uzalishaji wa taka, kutumia tena bidhaa na kurejeleza malighafi kwa matumizi mengine ya kiuchumi.


Wadau wa mazingira walielezwa kuwa utekelezaji wa mfumo huo unaweza kusaidia viwanda kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ufanisi wa matumizi ya rasilimali pamoja na kuongeza ushindani wa bidhaa katika soko la ndani na kimataifa.


Kwa upande wake, NEMC ilisisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wataalam wa mazingira ni muhimu katika kuhakikisha Tanzania inakuwa na sekta ya viwanda inayozingatia sheria, inalinda mazingira na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.


Mkutano huo umetajwa kuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto zinazokabili wadau wa mazingira pamoja na kuibua mapendekezo yatakayosaidia kuboresha utekelezaji wa sheria za mazingira nchini.


Kupitia mikutano kama hiyo, Serikali inalenga kujenga uelewa mkubwa kwa wadau kuhusu umuhimu wa matumizi salama ya kemikali, uhifadhi sahihi wa bidhaa hatarishi, usimamizi wa taka na uwekezaji katika teknolojia rafiki kwa mazingira kwa ajili ya ustawi wa kizazi cha sasa na kijacho.



TAKA SI UCHAFU TENA: TANZANIA YAELEKEA UCHUMI WA KIJANI KUPITIA UREJELESHAJI

Katika hatua muhimu ya kuimarisha usimamizi wa mazingira na kukuza uchumi wa kijani nchini, Serikali kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), imekutana na wadau wa usimamizi wa taka na urejelezaji jijini Dar es Salaam kujadili mustakabali wa sekta hiyo na nafasi yake katika maendeleo endelevu ya Taifa.

Kikao hicho kilichofanyika tarehe 13 Mei 2026 katika ukumbi wa NEMC – Mikocheni, kiliwakutanisha viongozi wa Serikali, wadau wa mazingira, waokota taka rejeshi, waokota chuma chakavu, sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa taka unaolinda mazingira na kuongeza thamani ya kiuchumi kupitia urejelezaji.

Akifungua kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira), Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Haran Luvanda alisema kuwa Tanzania kwa sasa huzalisha zaidi ya tani milioni 14.4 za taka ngumu kila mwaka, huku karibu nusu ya taka hizo zikizalishwa katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Dodoma, Mbeya na Tanga. Alieleza kuwa iwapo taka hizo hazitasimamiwa vizuri zinaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo uchafuzi wa mazingira, magonjwa ya mlipuko, kuziba mifereji na mafuriko.

Hata hivyo, Serikali imebainisha kuwa taka si tatizo pekee bali pia ni rasilimali yenye uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa Taifa kupitia dhana ya uchumi mzunguko (Circular Economy). Kupitia mfumo wa “Punguza, Tumia Tena na Rejeleza” maarufu kama 3Rs, Serikali inalenga kubadili mtazamo wa jamii ili kuona taka kama chanzo cha ajira, malighafi na maendeleo.

Katika hotuba yake, Balozi Luvanda aliwatambua waokota taka rejeshi na waokota chuma chakavu kama mashujaa wa kimya wanaochangia kwa kiwango kikubwa kupunguza taka zinazopelekwa dampo, kuongeza viwango vya urejelezaji na kusaidia kupunguza uzalishaji wa gesijoto. Alisisitiza kuwa kazi yao imekuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa kijani nchini.

“Waokota taka na waokota chuma chakavu ni sehemu muhimu ya mfumo wa usimamizi wa taka nchini. Kupitia kazi yao, maelfu ya vijana na wanawake wamepata ajira na kipato huku mazingira yakihifadhiwa,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, Dkt. Immaculate Sware Semesi, alisema kuwa maadhimisho ya miaka 40 ya NEMC yenye kauli mbiu “NEMC@40: Tunza Mazingira, Linda Taifa” yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza uwekezaji na ubunifu katika sekta ya usimamizi wa taka.

Aliyataja makundi mbalimbali kama Tanzania Waste Pickers Association (TAWAPA), Tanzania Recyclers Association(TARA) pamoja na Mtandao wa Waokota Taka Rejeshi Dar es Salaam (MTAWADA) kuwa miongoni mwa wadau muhimu wanaosaidia kusukuma mbele agenda ya uchumi mzunguko nchini.


Dkt. Semesi alibainisha kuwa NEMC imeendelea kushuhudia ongezeko la wawekezaji na taasisi zinazojihusisha na shughuli za ukusanyaji, usafirishaji, uchakataji na urejelezaji wa taka, hali inayodhihirisha kuongezeka kwa mwamko wa uzingatiaji wa sheria za mazingira pamoja na kukua kwa sekta ya uchumi mzunguko nchini.

Aidha, alieleza kuwa matumizi ya teknolojia za kisasa katika usimamizi wa taka, ikiwemo mifumo ya kidijitali ya ufuatiliaji wa taka, mashine za uchakataji pamoja na teknolojia za kuzalisha nishati kutokana na taka, yanafungua ukurasa mpya wa uwekezaji na ubunifu nchini Tanzania.


#NEMC40 #Miaka40YaNEMC #NEMCat40 #SustainableTanzania #MazingiraYetuUhaiWetu #MsemajiMkuuWaSerikali #2026Trends #SamiaSuluhuHassan#𝑴𝒂𝒛𝒊𝒏𝒈𝒊𝒓𝒂𝒀𝒆𝒕𝒖𝑼𝒉𝒂𝒊𝑾𝒆𝒕𝒖 

#TUNZAMAZINGIRALINDATAIFA

TIMU YA UKAGUZI WA MAZINGIRA KUTOKA NEMC MAKAO MAKUU NA KANDA YA ZIWA VICTORIA MASHARIKI WAADHIMISHA MEIMOSI 2026 KWA KUPANDA MITI MAKUMBUSHO YA MWL. JULIUS K. NYERERE, BUTIAMA

Timu ya watumishi wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) wanaofanya ukaguzi wa mazingira katika mikoa ya Kanda ya Ziwa Victoria, wakiongozwa na Meneja wa Utekelezaji wa Sheria, Mha. Luhuvilo B. Mwamila, waliadhimisha Sikukuu ya Wafanyakazi- Meimosi 2026 kwa kupanda miti katika Makumbusho ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Butiama.

Hatua hiyo ni ishara ya kuenzi dira ya Baba wa Taifa katika kuhifadhi mazingira na kusimamia utekelezaji wa sheria za utunzaji wa rasilimali za Taifa.










NEMC YAUNGANA NA WATANZANIA WOTE KUSHEREHEKEA MEI MOSI

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeungana na Watanzania wote kwenye Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ngazi ya Mkoa yaliyofanyika Mei 1, 2026 katika viwanja vya Mnazi Mmoja, ambapo Kitaifa yamefanyikia Mkoani Njombe 

Akizungumza katika  maadhimisho hayo yenye kaulimbiu "𝙠𝙖𝙯𝙞 𝙯𝙚𝙣𝙮𝙚 𝙨𝙩𝙖𝙝𝙖 𝙣𝙞 𝙣𝙜𝙪𝙯𝙤 𝙞𝙢𝙖𝙧𝙖 𝙠𝙬𝙖 𝙢𝙖𝙚𝙣𝙙𝙚𝙡𝙚𝙤 𝙚𝙣𝙙𝙚𝙡𝙚𝙫𝙪 𝙠𝙖𝙩𝙞𝙠𝙖 𝙪𝙩𝙚𝙠𝙚𝙡𝙚𝙯𝙖𝙟𝙞 𝙬𝙖 𝘿𝙞𝙧𝙖 𝙮𝙖 2050" Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Albert Chalamila alisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, nidhamu kazini na uzalendo miongoni mwa wafanyakazi, akieleza kuwa mafanikio ya maendeleo ya mkoa na Taifa kwa ujumla yanategemea juhudi za kila mfanyakazi. 

Aidha, alihimiza waajiri kuhakikisha wanaboresha mazingira ya kazi na kuwapatia wafanyakazi nyenzo stahiki ili kuongeza ufanisi na tija.

Kupitia risala ya vyama vya wafanyakazi, ilielezwa kuwa kuna umuhimu wa kuendelea kupigania ajira zenye staha kwa wote ili kuwawezesha wananchi kuishi maisha bora ikiwemo  kulindwa kwa haki za wafanyakazi, kuboreshwa kwa maslahi yao pamoja na kuhakikisha mazingira salama ya kazi yanazingatiwa wakati wote.

Maadhimisho hayo yamekuwa fursa muhimu kwa wafanyakazi na waajiri kutafakari mchango wao katika maendeleo ya taasisi na Taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikisisitiza umuhimu wa kazi zenye staha, ulinzi wa haki za wafanyakazi na utekelezaji wa sheria za kazi kama msingi wa maendeleo endelevu.




𝐌𝐈𝐀𝐊𝐀 𝟒𝟎 𝐘𝐀 𝐍𝐄𝐌𝐂: 𝐒𝐀𝐅𝐀𝐑𝐈 𝐘𝐀 𝐓𝐀𝐍𝐙𝐀𝐍𝐈𝐀 𝐊𝐔𝐄𝐋𝐄𝐊𝐄𝐀 𝐌𝐔𝐒𝐓𝐀𝐊𝐀𝐁𝐀𝐋𝐈 𝐖𝐀 𝐊𝐈𝐉𝐀𝐍𝐈 𝐍𝐀 𝐌𝐀𝐄𝐍𝐃𝐄𝐋𝐄𝐎 𝐄𝐍𝐃𝐄𝐋𝐄𝐕𝐔

Katika dunia inayokabiliwa na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira na kupungua kwa rasilimali asilia, Tanzania inaendelea kuwa mfano wa matumaini na uthabiti kupitia juhudi zake za kulinda mazingira. Maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) yanaonesha dhamira ya Taifa kulinda mazingira huku likiendeleza uchumi.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 1986, NEMC imekuwa mhimili wa usimamizi wa mazingira nchini. Zaidi ya miradi 35,000 imepitia Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA), hatua iliyosaidia kuoanisha maendeleo ya kiuchumi na ulinzi wa mazingira. Pia, utoaji wa vibali zaidi ya 28,000 umeimarisha uzingatiaji wa viwango vya mazingira na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa, huku juhudi za kudhibiti uchafuzi zikiepusha gharama kubwa za kurekebisha madhara.

Katika kujenga uwezo, wataalamu zaidi ya 12,000 wamepata mafunzo, na hivyo kuimarisha usimamizi wa mazingira katika sekta mbalimbali. Hii inaonesha kuwa mazingira si suala la pembeni bali ni msingi wa uchumi wa taifa, hasa katika sekta kama kilimo na utalii zinazotegemea rasilimali asilia.

Hata hivyo, changamoto bado zipo. Uharibifu wa misitu, kilimo kisicho endelevu na matumizi ya nishati zisizo rafiki vinaendelea kuathiri mazingira. Aidha, athari za mabadiliko ya tabianchi kama ukame na mafuriko zinaathiri maisha ya wananchi na uzalishaji. Hali hii inahitaji si sera pekee bali pia mabadiliko ya mtazamo, matumizi ya teknolojia na ushirikiano wa wadau wote.

Kupitia ushirikiano huo, wananchi zaidi ya milioni 4.2 wamefikiwa na elimu ya mazingira, huku sekta binafsi ikiongeza uwekezaji katika teknolojia safi na uzalishaji endelevu. Maboresho ya sera na sheria pia yameiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kimataifa katika masuala ya mazingira.

Kuelekea kilele cha maadhimisho tarehe 29 Mei 2026, shughuli kama upandaji wa miti 40,000 na utoaji wa elimu zinaonesha dhamira ya kuchukua hatua zaidi. Huu ni wakati wa kutafakari urithi tunaotaka kuacha kwa vizazi vijavyo.

Kwa ujumla, mafanikio ya miaka 40 ya NEMC yanaonesha kuwa Tanzania ina uwezo wa kufikia maendeleo endelevu. Hata hivyo, mafanikio ya baadaye yatategemea maamuzi ya sasa, ambapo kila Mtanzania ana wajibu wa kulinda mazingira kwa vitendo.

“𝑴𝒂𝒛𝒊𝒏𝒈𝒊𝒓𝒂 𝒔𝒊 𝒖𝒓𝒊𝒕𝒉𝒊 𝒕𝒖𝒍𝒊𝒐𝒖𝒑𝒐𝒌𝒆𝒂 𝒃𝒂𝒍𝒊 𝒏𝒊 𝒅𝒉𝒂𝒎𝒂𝒏𝒂 𝒕𝒖𝒍𝒊𝒚𝒐𝒂𝒛𝒊𝒎𝒂 𝒌𝒖𝒕𝒐𝒌𝒂 𝒌𝒘𝒂 𝒗𝒊𝒛𝒂𝒛𝒊 𝒗𝒊𝒋𝒂𝒗𝒚𝒐.”

NEMC NA ZEMA KUIMARISHA MASHIRIKIANO KATIKA USIMAMIZI WA MAZINGIRA

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC)  na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) wamekutana Zanzibar Aprili 27,2026 katika ziara ya mafunzo, kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika utekelezaji wa majukumu ya kimazingira, hasa mchakato wa ufanyaji wa Tathmini ya Athari kwa Mazingira na jamii katika miradi mikubwa na mchakato wa kupata vyeti vya kimazingira ili kuhakikisha maendeleo yanaendana na uhifadhi wa mazingira.

Akizungumza kwenye ziara hiyo, iliyohusisha wajumbe wa Bodi pamoja na Menejimenti ya pande zote mbili, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Mhandisi Mwanasha Tumbo, alisema Bara na Visiwani ni wamoja na hasa ikizingatiwa suala la mazingira ni mtambuka linalohitaji ushirikiano wa karibu kati ya pande zote mbili hatuna budi kutekeleza kwani mashirikiano katika sekta ya mazingira ni muhimu na kwakuwa limepewa kipaumbele katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kuhakikisha mazingira yanasimamiwa na kuhifadhiwa kwa ufanisi. 

Naye  Mwenyekiti wa Bodi kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira Zanzibar (ZEMA) Bi. Asha Ali Khatib alipozungumza alisema ni muhimu masuala ya mchakato wa ufanyaji wa  Tathmini ya Athari kwa Mazingira kuzingatiwa na wawekezaji  kuanzia hatua za awali hadi kukamilika kwa miradi ili kulinda mazingira huku akisistiza umuhimu wa kuimarisha ushirikishwaji wa jamii pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa ili kuhakikisha usimamizi na uhifadhi wa mazingira unafanyika kwa ufanisi.

Katika ziara hiyo, washiriki pia walipata wasilisho la kina kuhusu mchakato wa Tathmini ya athari kwa mazingira na jamii, mafanikio yaliyopatikana pamoja na changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wake kwa pande zote mbili yaliyotoa fursa ya majadiliano yenye kujenga kwa maendeleo endelevu ya mazingira.

Aidha, wajumbe hao walitembelea maeneo ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa Bandari ya Mpigaduri pamoja na Hoteli ya Verde iliyofanyiwa ufukiaji (reclamation) hali  iliyowasaidia washiriki kuona kwa karibu jinsi tathmini za mazingira zinavyotekelezwa katika miradi mikubwa na umuhimu wake katika kulinda rasilimali za asili.

Ziara hii ni kufuatia makubaliano ya awali yaliyowakutanisha katika kikao cha Tarehe 08/10/2025 chenye maazimio ya kuimarisha mashirikiano katika sekta ya Uhifdhi na Usimamizi wa Mazingira.









SERIKALI YASISITIZA UWAJIBIKAJI WA MAZINGIRA KWA VIWANDA NA WADAU WA TAKA HATARISHI

Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria za mazingira kwa sekta ya viwanda, kampuni za uteketezaji taka pamoja na wadau w...